Jumanne, 29 Aprili 2025

JAJI WILFRED DYANSOBERA WA MAHAKAMA KUU ASTAAFU, AAGWA KITAALUMA

Na NAOMI KITONKA- Mahakama, Dar es Salaam

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani jana tarehe 28 Aprili, 2025 aliongoza shauri maalum kwa ajili ya kumuaga kitaaluma Jaji wa Mahakama hiyo, Mhe. Wilfred Peter Dyansobera, ambaye amestaafu kwa mujibu wa sheria.

Shauri hilo lilifanyika katika Ukumbi namba moja (1) wa Mahakama Kuu jijini hapa na kuhudhuriwa na Viongozi na Wadau mbalimbali wakiwemo Majaji wa Mahakama Kuu.

Akizungumza wakati wa kuendesha shauri hilo, oMhe. Dkt. Siyani alisema kuwa jambo hilo ni muhimu kwa sababu linatoa nafasi kwa Mawakili wa Serikali na Mawakili binafsi kuelezea jinsi wanavyowafahamu na kuwapima Majaji wanaostaafu kwa ajili ya wengine kujifunza kupitia sifa zao.

“Mahakama katika utendaji wake inathamini utendaji kazi wa Majaji na kujituma kwao katika kukamilisha majukumu ya kimahakama na hata pale wanapostaafu kwa mujibu wa sheria tunawapa nafasi Majaji na watoa haki wengine wajifunze kupitia wengine pale sifa zao zinapotajwa na Wadau mbalimbali wa Mahakama,” alisema.

Akizungumza katika moja ya mawasilisho yaliyotolewa, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi aliwakumbusha Majaji na Mahakimu kufanya wajibu wao kwa kufuata taratibu na sheria zilizopo kwa mifano na kujifunza kwa vitendo ili kutimiza wajibu mkuu wa Mahakama na kumaliza vizuri utumishi wao.

“Tunakupongeza kwa kumaliza muda wako wa utumishi ukiwa na afya njema na katika kipindi chote utakumbukwa kama mtafiti mzuri wa sheria, Mwalimu, mchapakazi, kaka, mwajibikaji na tunaamini kwamba hautaenda kulala na badala yake utaendeleza ile ari ya uchapakazi uliyoionyesha mahali hapa,” aliongeza Mhe. Maghimbi.

Alieleza kuwa wanatambua bidii kubwa ya Mhe. Dyansobera katika kutetea na kutimiza majukumu ya kimahakama kwa kusimamia haki kwa Wananchi ikiwemo kutoa maamuzi ambayo yanaendelea kusaidia kuamua kesi nyingine.

Akizungumza wakati wa shauri hilo, Mhe. Dyansobera aliwashukuru wote kwa malezi mema, uongozi thabiti na mazingira bora ya kazi yaliyochangia zoezi la upatikanaji haki kufanyika kwa urahisi, huku akisisitiza kuzingatia umuhimu wa matokeo ya kazi na siyo muda mrefu mtu anaotumia kufanya kazi.

Naye Wakili wa Serikali, Bw. Camilius Lugina alitoa pongezi na kwa upande wao akisema, “Mahakama imefanya jambo jema na la heshima sana kwa kuwaaga Majaji wanaostaafu kwa sababu ni ishara ya kutambua mchango wao mkubwa kwa Mahakama na namna taratibu za Mahakama zinavyosaidia kurahisisha zoezi muhimu la utoaji haki ambalo ni jukumu kuu la Mahakama.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Chama cha Sheria Tanganyika (TLS), Wakili Ipilinga Panya alimpongeza Jaji Dyansobera kwa kutenda kazi kwa uadilifu na weledi na mchango wake ulioacha alama ya kudumu katika Tasnia ya Sheria Tanzania.

Zoezi hilo la kuwaaga kitaaluma Majaji wastaafu linalofanyika kwa mujibu wa Walaka Na. 1 wa Mwaka 2006 wa Jaji Mkuu na kuongozwa na Jaji Kiongozi lilihudhuriwa na Majaji wa Mahakama Kuu, Wasajili wa Mahakama Kuu, Watendaji, baadhi ya watumishi wa Mahakama na Wadau mbalimbali.


Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Wilfred Peter Dyansobera alipokuwa akiagwa jana tarehe 28 Aprili 2025.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akizungumza jambo katika shauri la kuagwa kitaaluma kwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Wilfred Peter Dyansobela iliyofanyika jana tarehe 28 Aprili 2025 katika ukumbi wa Mahakama Kuu Dar es Salaam.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akitoa wasilisho wakati wa shauri hilo.

Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Familia ya Jaji Dyansobela.


Jaji Kiongozi Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mhe. Wilfred Peter Dyansobela (aliyeketi wa pili kutoka kulia waliokaa) pamoja na baadhi ya Majaji wa Mahakama Kuu walioshiriki katika shauri hilo.

Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama walioshiriki katika hafla hiyo.

Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Msajili wa Mahakama Kuu, Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama Kuu.

Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Watumishi wa Mahakama Hiyo.


Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama.

Picha na BAKARI MTAULA-Dar es Salaam

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni