Jumatano, 30 Aprili 2025

MFUMO WA KODI UTUMIE TEKNOLOJIA YA KISASA; JAJI MKUU

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ameshauri mfumo wa kodi nchini kutumia teknolojia ya kisasa ili kuondoa changamoto zinazojitokeza katika kukusanya mapato.

Mhe. Prof. Juma ametoa ushauri huo leo tarehe 30 Aprili, 2025 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini hapa alipokutana na Tume ya Rais ya Maboresho ya Kodi kwa ajili ya kupata maoni yake kuhusiana na suala hilo.

‘Mfumo wa kodi lazima utumie teknolojia ya kisasa, hatuwezi kuuepuka. Teknolojia ya kisasa ndiyo njia bora zaidi ya kukwepa tamaduni nyingi zilizopo za watu kukutana katika kushughulikia masuala ya kodi,’ amesema.

Amewaambia wajumbe wa Tume hiyo, wakiongozwa na Mwenyekiti, ambaye alikuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Mhe. Balozi Ombeni Sefue, kuwa kuna mambo mengi ambayo unaweza kufanya kama ukiwekeza kwenye teknolojia.

Jaji Mkuu ameeleza kuwa kila kitu ndani ya Mahakama ya Tanzania kipo kwenye teknolojia na kuna data nyingi, ikiwemo hukumu mbalimbali ambazo zimepakiwa kwenye mfumo wa TanzLii.

‘Tuliwaomba wataalam wa teknolojia watumie akili mnemba, wajaribu kuangalia kwenye hukumu hizo changamoto zilizopo kwenye masuala ya kikodi. Takribani dakika 10 majibu yalipatikana…

‘Akili Mnemba inaweza kuwa na msaada sana, hizi changamoto zinaweza kuondoka, hasa tukiweza kupunguza makutano ya mtu kwa mtu kwa sababu binadamu tunakuwa na mitazamo na tamaduni zetu, ukiziingiza kwenye ukusanyanji wa kodi huwezi kufanikiwa,’ amesema.

Mhe. Prof. Juma amebainisha kuwa uwekezaji mkubwa uliofanyika kwenye teknolojia haujatumika kikamilifu kwa kuzingatia kuwa hata Mamlaka ya Mapato Tanzaania-TRA-wana data nyingi na wanaweza kutumia Akili Mnemba wakapata majibu na suluhisho la changamoto zilizopo.

Ameiambia Tume hiyo kuwa kazi yao inahitaji kuwa na fikra pana kwa sababu usuluhishi mwingi kama kurekebisha sheria umeshafanyika, hivyo njia bora ni matumizi ya teknolojia ambayo yatapunguza changamoto zilizopo.

Jaji Mkuu ameeleza kuwa kila Mtanzania ni mlipa kodi kwa njia moja au nyingine, hivyo mapendekezo yao kama Tume yatagusa maisha ya mtu bonafsi na uchumi wa nchi kwa ujumla.

Mhe. Prof. Juma ameeleza kuwa kama Kiongozi wa Mhimili, alipata pia nafasi ya kuzungumza na Majaji wa Mahakama ya Rufani, hasa wale waliowahi kuwa Wenyeviti katika Mabaraza ya Kodi ili kupata maoni yao jinsi ya kuboresha mfumo wa kodi nchini na changamoto wanazoziona.

Katika maoni yao, Majaji hao wamebainisha, pamoja na mambo mengine, kuangalia upya njia zinazotumika kuingiza bidhaa na Maofisa Forodha kuwepo kwenye maeneo ya madini, wafanyabiashara wadogo kulipa kodi rafiki na kuweka mud awa TRA kujibu mapingamizi.

Jaji Mkuu pia alikutana na Jaji aliyewahi kuwa Wakili kwenye mashauri ya kodi kupata maoni yake kuhusu suala hilo na kubainisha changamoto kadhaa, ikiwemo utatuzi wa mgogoero wa kodi kuchukua muda mrefu unapoteza imani ya walipa kodi.

Alieleza kuwa kwa kuwa Bodi ya Rufaa ya Kodi pamoja na Baraza la Rufaa la Kodi kuwa chini na Wizara ya Fedha na wajumbe wake kuteuliwa na Waziri wa Fedha huathiri muonekano wa Taasisi hizo kuwa huru mbele ya macho ya mlipa kodi.

Kadhalika, Mhe. Prof. Juma alipata maoni kutoka kwa wafanyabiashara wenye shule binafsi na kubainisha kuwa Watumishi wa umma ni wakali kupindukia wanaposhughulikia masuala ya kodi na watendaji wa Mamlaka ya Mapato Tanzania kutokuwa waadilifu.

Wakizungumza baada ya maoni hayo, Wajumbe wa Tume wamempongeza Jaji Mkuu kwa maoni hayo chanya aliyotoa na kuunga mkono mapendekezo aliyoyatoa, hususan matumizi ya teknolojia katika kutatua changamoto za kikodi na kwamba wanatakiwa kufikiri kwa upana kabla ya kutoa mapendekezo yao kwenye suala hilo.

Kabla ya mazungumzo hayo, wajumbe wa Tume hiyo walitembelea Ofisi ya Jaji Mkuu kujionea mambo mbalimbali, ikiwemo picha za Majaji Wakuu waliowahi kuhuduma mahakamani kabla na baada ya uhuru.

 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-juu na chini-akizungumza alipokutana na Tume ya Rais ya Maboresho ya Kodi Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 30 Aprili, 2025.


Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Maboresho ya Kodi, Mhe. Balozi Ombeni Sefue akitoa maelezo ya awali baada ya Tume yake kukutana na Jaji  Mkuu.

Makamishna na Wajumbe wa Tume wakimsiliza Jaji Mkuu-hayupo kwenye picha. Picha chini ni Wajumbe wa Sekretarieti ya Tume hiyo.

Kikao kinaendelea.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Tume, Mhe. Balozi Ombeni Sefue kabla ya mazungumzo yao. Picha chini ni Makamishna wa Tume wakiwa kwenye picha ya pamoja.

Makamishna wa Tume wakizungumza na Jaji Mkuu-wa pili kushoto. Picha chini Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwaonesha picha za Majaji Wakuu waliowahi kuhuduma mahakamani kabla na baada ya uhuru.

Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Maboresho ya Kodi, Mhe. Balozi Ombeni Sefue akisaini kitabu cha wageni alipokuwa kwenye ofisi ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni