Na INNOCENT KANSHA-Mahakama
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 28 Aprili, 2025
amefungua mafunzo elekezi kwa Majaji watano (5) wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania
walioaminiwa na waliteuliwa kuwatumikia wananchi hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Majaji hao ni pamoja na Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki
Feleshi, Mhe. Latifa Mansoor, Mhe. George Masaju, Mhe. Dkt. Deo Nangela na Mhe.
Prof. Agatho John Ubena.
Aidha Mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo na ujuzi katika
utoaji wa haki pamoja na kuwapatia muongozo na nyenzo muhimu ili kurahisisha
utendaji wao wa kazi katika Mahakama ya Rufani.
Akitoa
hutuba ya ufunguzi wa mafunzo hayo yatakayo fanyika kwa muda wa siku tano yanayofanyika
katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) mkoani Tanga Mhe. Prof. Juma
amewakumbusha Majaji hao kuwa moja ya sababu ya kutoa mafunzo hayo ni
kuwatayarisha kutofanya makosa juu ya dhamira ya dhati ya kutoa haki kwa
wananchi pale wanapofika mbele yao.
“Akawakumbusha
Majaji hao, kwa kutoa mfano wa maneno yaliyoandikwa na Lord Denning akasema,
umuhimu wa uadilifu katika utoaji wa haki, hili ni jambo muhimu sana na haki
inaanzia kwenye nafsi yako wewe yaani ndani, ukiwa na nafsi yenye kutenda haki
siku zote utatafuta ukweli katika kila jambo unalolitolea maamuzi…
Na
hapa ninapozungumzia haki, haki ni stahiki yako kwa mujibu wa Katiba na sheria
huwezi kubakia ukisema nina haki nina haki, unaposema nina haki ni lazima
ueleze chanzo chake na kiini chake ambayo ni Katiba au sheria, haki haipatikani
tu hewani,” amesisitiza Jaji Mkuu Mhe. Prof. Juma.
Mhe.
Prof. Juma amesema Jaji au Hakimu anayetoa haki lazima awe na dhamira ndani ya
nafsi yake inayosimamia haki. Jaji Mkuu atolea mfano maneno ya Lord Denning
kwamba, hakuna tija ya kuwa na sheria nzuri na unaweza kuwa na sheria nzuri
kweli na zipo lakini sheria nzuri haitoshi kama mtekelezaji wa sheria hiyo hana
kiini cha utoaji wa haki.
Aidha,
Mhe. Prof. Juma ameongeza kuwa, maadili na utoaji haki siyo kwa Majaji na
Mahakimu pekee hata kwa maafisa Mahakama wengine kama Mawakili uadilifu ni kwa
wote, wengi huwa wanasahau kwamba sehemu kubwa ya haki inaanzia kwa Mawakili
anapomshauri mteja, anaposimamia shughuli yake.
Wakili
anapoanza kupoteza muda anamzungusha zungusha au anamwambia ukweli. Kwa mfano
haki inaweza kupatikana kwa kufuata taratibu chache lakini wakili anaweza
kuigeuza na kufanya biashara anaweza kupinda pinda maeneo mengi ilimradi apate
kipato zaidi. Vilevile, wakili huyo anaweza kutoa hoja ambazo siyo hoja za
kutenda haki, pengine hoja za kuwafurahisha wale wanaomlipa fedha na hilo ni
jambo lililoandikwa na Lord Denning.
Kwa
tafsiri isiyo rasmi, haitakuwa na maana au tija hata kidogo kama tutakuwa na sheria
sana kama zitasimamiwa na Majaji wabaya na wanasheria wasiokuwa waadilifu ama
wala rushwa. Hicho ndicho kiini cha kazi ya utoaji haki kwa watu. Vilevile Jaji
Mkuu Mhe. Prof. Juma akatoa rai na kuwakumbusha Majaji hao kutosahau kwamba wao
wanatoa huduma za umma.
“Huduma
za kimahakama ni huduma za umma kwa hiyo lazima tukubali kukosolewa sana kwa
haki au hata kusikuwa kwa haki kwa sababu unafanya kazi ya umma na
unapokosolewa usiichukulie kama suala binafsi, uchukulie kwamba ni sehemu ya
kazi yako. Kuna wengine hawataki kuelewa ukweli, kuna wengine hawaelewi kweli
na kuna wengine ambao hawataki ili shauri liishe wao linapoendelea ndiyo
wanapata faida,” amesema Jaji Mkuu.
Mhe.
Prof. Juma amesema, na mara nyingi maboresho yaliyo mengi yanatokana na
kukusolewa, kwamba kuna maeneo ambayo yanalalamikiwa sana lazima watu wake na
kuangalia kwa nini. Kwa mfano Mahakama ya Rufani imekuwa ikilalamikiwa sana kwamba
maamuzi mengi yamekuwa yakiengemea sana mbinu au kanuni za kiufundi badala ya
kuegemea kwenye haki. Jaji hawezi kukasilika anapokosolewa kwa hilo kwa sababu
ni ukweli kinachotakiwa kufanyika kutafuta namna ya kukwepa kutumia kanuni za kiufundi.
Na
kwa bahati nzuri sheria zimebadilishwa “overriding objectives” lakini baadhi
yetu bado tunakwepa hata kutumia sheria hizi zilizobadilishwa bado tunaenda
kwenye kanuni za kiufundi ambazo zinachukua muda mrefu sana katika utoaji wa
haki.
Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama ya
Rufani ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) Mhe.
Dkt. Paul Faustine Kihwelo amewapongeza Majaji wapya wa
Mahakama ya Rufani wanaoshiriki mafunzo hayo kwa kuaminiwa na kuteuliwa na Mhe.
Rais kuwatumikia wananchi.
Mafunzo
haya ni sehemu ya utekelezaji wa sera ya mafunzo ya Mahakama ya mwaka 2019,
vilevile sera ya mafunzo ya Taifa ambayo inamtaka mtumishi yeyote anapoteuliwa
katika nafasi mpya au kuajiriwa katika nafasi mpya anatakiwa kupata mafunzo
elekezi na pia sera hiyo imesisitizwa katika Mpango Mkakati wa Mahakama na
Mpango Mkakati wa Chuo.
“Mahakama
ya Tanzania ni moja ya Taasisi chache sana ambazo zinafanya vizuri sana katika
eneo la mafunzo kwa watumishi wa ngazi mbalimbali, hii ni kutokana na kweli
kwamba tumekuwa kupokea maombi mengi kutoka taasisi mbalimbali zikitaka kuja
kujifunza kupitia kwetu,” amesema Mkuu huyo wa Chuo.
Naye, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
Tanzania, Kanda ya Tanga Mhe. Katarina Revokati Mteule ameishukuru
Mahakama ya Tanzania kuamuru mafunzo hayo kufanyika Kanda ya Tanga kwani Chuo
cha Uongozi wa Mahakama kina Mamlaka pana kinaweza kufanya kazi mahali popote
katika nchi lakini bado Kanda ya Tanga kupitia Chuo cha IJA kimepata heshima
hiyo ya kipekee ya kuendesha mafunzo hayo elekezi kwa Majaji wa Rufani.
Akitoa
ujumbe mfupi wa wananchi wa Kanda ya Tanga kwa Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof.
Ibrahim Hamis Juma, Mhe. Mteule amesema wanaTanga wanampongeza kwa maboresho
makubwa yaliyofanya na Mahakama hasa ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano
(TEHAMA).
Aidha,
siku ambayo waraka ulitolewa ukitaka kesi zote zisikilizwe kwa njia ya mtandao
haraka sana Kanda ilichukua hatua kwa sababu jiografia ya Tanga ni ya kipekee
kulinganisha na maeneo mengine ya nchi. Tanga ina wilaya nane na Mahakama za
wilaya nane zote zipo mbali sana na inapopatikana Mahakama Kuu, amesema Mhe.
Mteule
“Nikichulia
mfano wa Wilaya ya Kilindi iliyopo zaidi ya kilometa 250 kutoka Tanga mjini
ambapo wananchi wanasafiri umbali mrefu na miundombinu ya barabara siyo rafiki,
hivyo kuanza matumizi ya kusikiliza kesi kwa njia ya mtandao kumetoa fursa ya
kuwapunguzia wananchi hawa gharama kubwa za uendeshaji wa kesi na kuokoa muda mwingi
uliokuwa unapotea, sambamba na hilo imekuwa faraja kwao nakunitaka nikushuru
sana kwa niaba yao Mhe. Jaji Mkuu,” amesema kwa bashasha Mhe. Jaji Mfawidhi
huyo.
Majaji wanne kati ya hao watano, waliteuliwa na Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Dkt. Samia Suluhu Hassan, mnamo tarehe 10
Januari, 2025 huku mmoja ambaye alikuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Jaji
Dkt. Eliezer Feleshi aliteuliwa mnamo tarehe 14 Agosti, 2024. Wengine wanne ni Mhe.
Latifa Mansoor, Mhe. George Masaju, Mhe. Dkt. Deo Nangela, na Mhe. Prof. Agatho
John Ubena.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akifungua mafunzo elekezi kwa Majaji watano (5) wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania leo tarehe 28 Aprili, 2025 yanayofanyika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) mkoani Tanga.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akifungua mafunzo elekezi kwa Majaji watano (5) wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania leo tarehe 28 Aprili, 2025 yanayofanyika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) mkoani Tanga.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akitoa mada ya wajibu wa Majaji wa Mahakama ya Rufani katika msingi wa kukuza maboresho ya teknolojia mahakamani kwa Majaji Mahakama ya Rufani (hawapo pichani)
Jaji wa Mahakama ya Rufani ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) Mhe. Dkt. Paul Faustine Kihwelo akifafanua namna Chuo hicho kinavyotekeleza Mpango Mkakati na sera ya Mafunzo kwa watumishi wa kada mbalimbali.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga Mhe. Katarina Revokati Mteule akitoa shukrani za wanaKanda ya Tanga kwa Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma jitihada za kuboresha miundombinu hasa ya TEHAMA inavyosaidia wananchi kupata haki.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa neno la pongezi kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani kwa kuaminiwa na kuteuliwa kwao.
Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania Mhe. George Helbert akiongoza hafla hiyo ya uzinduzi wa mafunzo elekezi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni