Alhamisi, 10 Aprili 2025

SIASA MWIKO KWA WATUMISHI WA MAHAKAMA; JAJI MKUU

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewakumbusha Watumishi wa Mahakama katazo la kisheria linalowazuia kujihusisha na masuala ya siasa.

Mhe. Prof. Juma ametoa angalizo hilo leo tarehe 10 Aprili, 2025 alipokuwa anafungua Kikao cha siku mbili cha Baraza la Wafanyakazi Taifa kinachofanyika katika Ukumbi wa PSSF jijini Dodoma.

‘Tukumbushane, ukijitokeza kuwania nafasi ya kugombea ngazi yoyote katika uchaguzi ujao na ukakosa, hutarudi katika utumishi wa Mahakama. Tulifanya hivyo katika uchaguzi Mkuu uliopita,’ Jaji Mkuu ameonya.

 Mhe. Prof. Juma amebainisha kuwa katazo la ushiriki katika shughuli za kisiasa kwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu, Hakimu wa ngazi yoyote; zimefafanuliwa kwa kina na Kanuni za Maadili ambazo amewaomba wazisome tena na tena.

Amewakumbusha pia maelekezo ya Ibara ya 113A kuhusu uanachama katika vyama vya siasa, ambayo yanasema, “Itakuwa ni marufuku kwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu, Hakimu wa ngazi yoyote kujiunga na chama chochote cha siasa, isipokuwa tu kwamba atakuwa na haki ya kupiga kura iliyotajwa katika Ibara ya 5 ya Katiba hii.”

Jaji Mkuu amefafanua kuwa ingawa Kanuni za kimaadili kupiga marufuku ushiriki katika siasa zimejielekeza kwa Majaji, Wasajili, Mahakimu na Wasaidizi wa Majaji, Watumishi wezeshi wa Mahakama wamebeba taswira na sura ya Mahakama kutoshiriki katika siasa.

‘Tunapaswa kujiepusha na siasa kwani kufanya hivyo tukiwa Watumishi inapelekea Wadau na Wananchi kupoteza imani na Mahakama yao kwa kuamini kuwa haki haiwezi kutendeka kwa sababu Mahakama inayo itikadi ya chama fulani…

 ‘…Nafahamu kuwa zipo jitihada kubwa katika mitandao ya kijamii kujaribu kutuhusisha na siasa, lakini kipimo na nafasi yako na namna unavyojitokeza, unavyoongea na unavyotoa huduma,’ Mhe. Prof. Juma amesema.

Jaji Mkuu amewataka Watumishi wote kujizuia kuonesha hisia zao kwa vyama wanavyovipenda au wagombea wanaowapenda na kwamba lazima wajipange mapema kuwahudumia wateja watakaofika mahakamani kuhusiana na masuala yanayohusu uchaguzi.

‘Ni vema tukaanza kujipanga mapema kuzifahamu sheria na kanuni za uchaguzi wa 2025 ili tuweze kutekeleza kazi zetu kwa ufanisi na ueledi mkubwa. Tukijipanga mapema tutajiepusha kuwa sehemu ya walalamikiwa katika masuala ya uchaguzi na badala yake tutabaki kuwa chombo kinachoaminiwa cha kutoa maamuzi katika mashauri ya uchaguzi endapo yatakuwepo,’ amesema.

Mhe. Prof. Juma ametumia fursa hiyo kuhimiza Majaji na Mahakimu kusikiliza na kuamua kwa haraka na katika misingi ya haki mashauri yatokanayo na taratibu mbalimbali za uchaguzi.

Amekumbushia kuwa katika uchaguzi Mkuu ujao, Majaji, Wasajili, Mahakimu na Watumishi wa Mahakama ni sehemu muhimu ya utatuzi wa migogoro ya uchaguzi.

Jaji Mkuu amebainisha pia kuwa kama raia, Watumishi wa Mahakama wanayo haki ya kikatiba kuwachagua Viongozi. Hivyo ametoa rai kwa Watumishi wa Mahakama kutumia haki hiyo ambayo wamepewa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-juu na chini-ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Taifa akizungumza wakati anafungua kikao cha Baraza hilo.




Katibu wa Baraza hilo, Bw. Hezra Kyando akitoa utambulizho wa Wajumbe wa Baraza ambao wamehudhuria kikao hicho.


Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo akifuatilia yaliyokuwa yanajiri wakati wa Kikao hicho.


Makamishna na Watumishi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama nao wamehudhuria kikao hicho.


Sehemu ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- wakifuatilia kinachojiri kwenye Kikao hicho.



Sehemu nyingine ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- wakifuatilia kinachojiri kwenye Kikao hicho.



Sehemu nyingine ya tatu ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- wakifuatilia kinachojiri kwenye Kikao hicho.



Sehemu nyingine ya nne ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- wakifuatilia kinachojiri kwenye Kikao hicho.


Sehemu nyingine ya tano ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- wakifuatilia kinachojiri kwenye Kikao hicho.



Sehemu nyingine ya sita ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- wakifuatilia kinachojiri kwenye Kikao hicho.



Sehemu nyingine ya saba ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- wakifuatilia kinachojiri kwenye Kikao hicho.


Sehemu nyingine ya nane ya Wajumbe wa Baraza-juu na chini- wakifuatilia kinachojiri kwenye Kikao hicho.



Wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama wakifuatilia kinachoendelea. Picha chini ni Wajumbe kutoka Mahakama ya Rufani.


Wajumbe wa Baraza kutoka Mahakama Kuu, Masjala Kuu nao walikuwepo kwenye Kikao.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni