Na INNOCENT KANSHA - Mahakama
Jaji
Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 15 Mei, 2025
amezindua
rasmi Mfumo wa Mafunzo kwa Njia ya Mtandao (e-Learning
Platform) pamoja na kukabidhi jengo la kisasa la Media Studio itakayotumika
kuandaa mitaala ya kufundishia katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto
(IJA).
Uzinduzi
huo umefanyika kwa njia ya mkutano mtandao wakati Mhe. Prof. Juma akiwa ofisini
kwake jijini Dar es Salaam huku akiambatana na Msajili Mkuu wa Mahakama Mhe.
Eva Nkya pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel, huku Viongozi na Maafisa
wengine waandamizi wa Mahakama wakifuatilia kwa njia hiyo ya mkutano mtandao
kutokea Dar es salaam, Dodoma na Lushoto.
“Ni faraja kubwa kwamba uzinduzi huu unafanyika kwa njia ya mtandao, jambo linaloendana kikamilifu na dhamira ya Mahakama ya Tanzania kutumia teknolojia katika nyanja zote za utoaji huduma na kuonesha kwa vitendo kuwa Mahakama yetu ni taasisi inayoendana na mabadiliko ya kidijitali,” amesema Jaji Mkuu.
Katika
hotuba yake, Mhe. Prof. Juma amesema kuwa mfumo huo unakwenda kuwezesha
watumishi wengi wa Mahakama kupata mafunzo mbalimbali bila kikwazo cha kifedha,
gharama na muda. Mfumo unampa msomaji uhuru wa kupanga muda unaomfaa kwa kusoma
pamoja na kuchagua mazingira rafiki ya kusoma.
Aidha, Mhe.
Prof. Juma amebainisha faida nyingi za Mfumo
wa Mafunzo kwa Njia ya Mtandao (e-Learning Platform) kama vile, urahisi wa kufikisha mafunzo kwa wasomaji wengi na
kwa muda mfupi na kuwa mada zote
zinapakiwa kwenye mfumo na zinapatikana muda wowote kwa njia ya mtandao,
inapotokea kunakuwa na uhitaji wa mafunzo ya aina yeyote ni rahisi sana
kuwafanya wasomaji wengi waweze kusoma na kumaliza mada zao ndani ya muda mfupi
tofauti na mafunzo yanayotolewa ana kwa ana ambapo
ingewalazimu wakufunzi kuwazungukia wasomaji/wanafunzi
maeneo walipo au kuwakusanya sehemu moja na kuwapatia mafunzo.
Vilevile,
faida nyingine ni urahisi wa kufanya mabadiliko ya mtaala Inapotokea kunakuwa na mabadiliko yeyote ya mtaala au sheria au
chochote katika mada, inakuwa rahisi kufanya mabadiliko kwenye mfumo,na
mbadiliko hayo kuwafikia walengwa papo hapo.
“Ni dhahiri shahiri kuwa kutakuwa
na unafuu wa gharama za utoaji mafunzo Mafunzo haya yanapunguza gharama kwa
upande wa rasilimali fedha, muda na nafasi,” ameongeza Jaji Mkuu.
Jaji Mkuu amesema, sambamba na ujenzi wa Mfumo huo, pia umefanyika ukarabati mkubwa wa jengo lililopo Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kulifanya kuwa Media studio ya kisasa yenye vifaa vya TEHAMA. Studio hiyo ni maalum kwa ajili ya uzalishaji wa mada mbalimbali za kujifunzia, zitakazobadilishwa kuwa katika mfumo wa kieletroniki na kupakiwa kwenye Mfumo wa mafunzo kwa njia ya mtandao kwa ajili ya matumizi ya wanufaika wa mafunzo yatakayotolewa kwa njia hiyo ya masafa.
Aidha, Mhe. Prof. Juma ameongeza kuwa, Mahakama imejipanga kikamilifu kuutumia mfumo huu ili uweze kuleta tija katika kubadili utendaji kazi wa Watumishi. Hivyo, uwekezaji wa Mfumo huu utaboresha huduma za Mahakama, kwa kuwa watumishi wengi watafikiwa na mafunzo kwa wakati pasipo kujali utofauti wa kijiografia na hivyo kupunguza mlundikano wa mashauri, kuongeza uwazi katika utoaji wa haki, na kuimarisha imani ya wananchi.
“Nitoe rai kwa Mtendaji Mkuu na Msajili Mkuu wa Mahakama kuwa,
ushirikiano baina ya Mahakama na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA)
uendelee ili kuhakikisha matumizi ya Mfumo yanakuwa endelevu kwa kufanya kazi kwa pamoja na kazi ya kujenga umahiri
wa watumishi na wadau
inakuwa endelevu,” amesisitiza Jaji Mkuu.
Vilevile, Mhe. Prof. Juma amesema kwamba, hali ya Watumishi kukosa mafunzo kutokana na changamoto ya ufinyu wa bajeti itaondolewa na jukwaa hilo na kuhakikisha uwezo, ujuzi na umahiri wa Watumishi na wadau wa Mahakama unaimarika.
“Sote tunajua kuwa Mahakama ilikuwa inaandaa Mipango ya Mafunzo ya kila mwaka, lakini kwa sababu za ufinyu wa bajeti, mipango hiyo ilikuwa inatekelezwa kwa kiwango kidogo sana. Hili linakwenda kumalizwa na uwepo wa mfumo huu kwa kuwafikia watumishi wengi kwa wakati mmoja na kuwa, hakutakuwa na vizuizi vya kijiografia, muda au rasilimali. Hivyo, kuendelea kufanya kazi kwa pamoja kutawezesha lengo la ujenzi wa Mfumo kufikiwa kwa haraka,” amesema Jaji Mkuu huyo.
Vilevile
Mhe. Prof. Juma amesema kuwa mfumo huo utaiwezesha IJA kutoa mafunzo ya muda
mrefu ya ngazi ya Stashahada (Diploma) na Astashahada (Cheti) ya Sheria na
hivyo kuwarahisishia watu kujifunza
elimu ya sheria popote walipo.
Aidha
Jaji Mkuu ametoa wito kwa Uongozi wa Mahakama na wa IJA kuhakikisha wana
usimamia vizuri mfumo huo uwe endelevu ikizingatiwa kuwa umegharimu kiasi cha
shilingi bilioni 1.36 za Kitanzania.
Wakati
huo huo, Jaji Mkuu amezindua mafunzo ya kundi la kwanza la Washiriki 25 ambao
ni Naibu Wasajili 5, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa mikoa 5 na Mahakimu Wakazi
Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya 15 wanaochukua mafunzo ya kiuongozi kupitia
mada ya "Enhancing Leadership and Practical Skills for Registrars, Deputy
Registrars, and Magistrates in-charge.
Awali,
Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa
Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo akitoa taarifa fupi ya ujenzi wa mradi
huo, ameuelezea mfumo huo ulijengwa kwa kusema kuwa umejengwa ili kutatua
changamoto ya watumishi wengi wa Mahakama kukosa mafunzo kwa sababu za kifedha,
umbali na muda.
Pia
amesema kuwa mfumo huo ambao tayari una mada tatu, unamuwezesha mwanafunzi
kujisomea mwenyewe ndani ya mwezi mmoja na unasahihisha wenyewe mitihani na
majaribio.
Aidha,
Mhe. Dkt. Kihwelo amesema kuwa, mfumo huo pamoja na studio ni sehemu ya
utekelezaji wa Mpango mkakati wa Mahakama katika awamu ya pili ya Maboresho ya
Mahakama na umefadhiliwa na Serikali ya Tanzania kupitia Benki ya Dunia.
Jukwaa
hilo la kufundishia mtandaoni lilijengwa na wataalamu wa Teknolojia ya Habari
na Mawasiliano (TEHAMA) kutoka Mahakama ya Tanzania, IJA, Chuo Kikuu Huria cha
Tanzania (OUT) na Chuo cha Serikali za Mitaa (Hombolo).
“Ni
imani
kuwa mfumo huu utakuwa chachu ya mabadiliko ya kiutendaji, kwa kusaidia
kuimarisha weledi wa watumishi wetu na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa kazi
za Mahakama kwa kuwa Watumishi watapata fursa ya kupatiwa mafunzo mbalimbali
kwa gharama nafuu na kuwafikia wengi kwa wakati mmoja,”
ameongeza Jaji Kihwelo.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya akifuatilia mkutano mtandao huo
(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni