Ijumaa, 2 Mei 2025

JINSI MAHAKAMA SPORT ILIVYOWASAMBARATISHA WAPINZANI MEI MOSI 2025

  • Yabeba ndoo 4, medali mbili

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Timu ya Mahakama ya Tanzania, maarufu Mahakama Sports, imeshiriki kwa mafanikio makubwa kwenye mashindano ya Mei Mosi kwa mwaka 2025 yaliyofanyika mkoani Singida na kufanikiwa kupata makombe manne na medali kadhaa katika michezo mbalimbali.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana tarehe 1 Mei, 2025 na Mwenyekiti wa Mahakama Sports, Wilson Dede, Timu hiyo ilishiriki katika michezo ya mpira wa miguu, netboli, riadha, karata, draft, bao, dats na baiskeli.

Anaeleza kuwa Timu ya Mahakama iliingia kambini Singida kuanzia tarehe 14 Aprili, 2025, ikiwa na washiriki 47, wakiwemo Viongozi na kupangwa kwenye makundi mbalimbali.

Timu ya Mahakama Sports imefanya vizuri katika upande wa karata Wanawake na kuibuka mshindi wa kwanza na kuzawadiwa kikombe. Kadhalika, kwenye upande wa baiskeli na bao Wanawake, Mahakama Sports ilifanya vizuri pia na kufanikiwa kuwa mshindi wa pili, hivyo kuzoa vikombe viwili.

Mwenyekiti Dede anaeleza pia kuwa Mahakama Sports ilifanikiwa kutimua vumbi kwenye mchezo wa riadha kwa upande wa Wanaume na Wanawake mita 200 na kufanikiwa kupata medali mbili baada ya kushika nafasi ya tatu kwa kila upande.

Pamoja na makombe hayo matatu, Mahakama Sports ilishiriki katika Bonanza kubwa la OSHA lililofanyika mkoani Singida tarehe 26 Aprili, 2025 ikiwa na michezo mbalimbali. Bonanza hilo lilijumuisha Timu 12 kutoka Wizara, Idara na Taasisi mbalimbali za Serikali na Mashirika yaliyokuwa kwenye mashindano ya Mei Mosi 2025.

Katika Bonanza hilo, Timu ya Mpira wa Miguu ya Mahakama Sports ilishiriki na kufanikiwa kuwasambaratisha wapinzani wote na kuwa mabingwa wa bonanza hilo, hivyo kuzawadiwa kikombe cha mshindi wa kwanza.

Katika mashindano ya Mei Mosi, Mwenyekiti Dede anaeleza kuwa Timu ya Mahakama ilishiriki pia kwenye michezo ya Mpira wa Miguu na Mikono.

‘Katika mchezo wa mpira wa miguu, Mahakama tulikuwa kundi "B" lenye timu sita, ambazo ni Mahakama, TRA, U-DOM, Utumishi, Afya na Maji. Upande wa mchezo wa mera wa mikono tulikuwa kundi "A" lenye timu za Mahakama, Afya, Maliasili, Tume ya Ushirika, MSD na Fedha,’ amesema.

Mwenyekiti Dede anaeleza kuwa katika mchezo wa mpira wa miguu, Mahakama ilicheza mechi tano na kuishia kwenye makundi, hivyo kushindwa kusonga mbele.

Anaeleza pia kuwa kwa upande wa netbali, Mahakama ilifanikiwa kuingia hatua ya nane bora ambapo ilicheza na Wizara ya Mambo ya Ndani na kupoteza mchezo, hivyo kushidwa kuendelea na mashindano katika hatua iliyofuata.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi kombe Malkia Nondo baada ya kuibuka mshindi wa kwanza wa Mchezo wa Karata Wanawake. 


Ushahidi huu hapa, makombe manne iliyozoa Mahakama Sports kwenye mashindano ya Mei Mosi mwaka 2025.


Mfukuza upeo wa Mahakama Sporst Atugonza Yusta Tibendelanda akiwa na moja ya makombe hayo. Picha chini ni mfukuza upepo mwingine 
Mwajabu Gwire akiwa na kombe alilonyakua baada ya kuwa mshindi wa pili kwenye mchezo wa baiskeli.


Mshambuliaji hatari wa Timu ya Mpira wa Miguu wa Mahakama Sports, Martin Mapinduzi akifurahia medali yake.


Ushindi ni raha kwa kweli, au wewe unaonaje.


Sehemu ya Timu ya Mahakama Sports na Viongozi wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kuibuka washindi kwenye michezo mbalimbali.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni