Na Christopher Msagati- Mahakama, Manyara
Wajumbe
wa Chama cha Majaji na Mahakimu Nchini (JMAT) tawi la Manyara wamekumbushana
juu ya taratibu na kanuni za uandishi bora wa Hukumu.
Akifungua
mkutano huo, Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora
ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama hicho kwa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara katika
mafunzo yaliyoambatana na Mkutano wa Chama hicho uliofanyika tarehe 9 Mai, 2025
katika Ukumbi wa Wazi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.
Mhe.
Kamuzora aliwasisitiza Majaji na Mahakimu kuzingatia miongozo mbalimbali
inayotolewa katika kufanikisha kazi zao za kila siku kuanzia usikilizaji wa
mashauri mpaka utoaji wa maamuzi.
“Hii
miongozo na kanuni zinazotolewa, zimeandaliwa ili zituwezeshe kuzingatia
taratibu zinazostahili ili kuwa na hukumu bora ambazo zitaleta tija kwa wadaawa
wetu. Hivyo ni muhimu kuzingatia na kufuata kanuni hizi,” alisema Mhe.
Kamuzora.
Naye,
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza wakati wa
kutoa Mada aliwaeleza wajumbe kuwa miongozo ya uandishi bora wa Hukumu husaidia
katika kuleta uwazi ambao huonekana kwa wadaawa na uwazi huo husaidia kupunguza
malalamiko au kutokuridhika katika maamuzi yanayotolewa.
“Kanuni
hizi zikifuatwa vizuri, zitawasaidia nyinyi waheshimiwa Majaji na Mahakimu kuwa
na uwazi miongoni mwa wadaawa wenu. Vile vile matumizi ya kanuni hizi huongeza
usawa na kuwa na mfanano wa utaratibu katika uandishi wa hukumu zetu,” alisema
Mhe. Kahyoza.
Akichangia
mada katika mafunzo na Mkutano huo, Hakimu Mkazi Mahakama ya Mwanzo Haydom Mhe.
Zena Mgalula aliushukuru uongozi wa JMAT Tawi la Manyara kwa kuandaa Mkutano na
Mafunzo hayo ambayo yatawapa weledi zaidi katika kuandika hukumu zenye
kuzingatia kanuni na miongozo.
“kwa
kweli tunashukuru uongozi wa JMAT kwa kuamua kuleta mafunzo haya Katikati ya
mkutano huu kwani yatatufaa sana katika uboreshaji wa uandishi wa hukumu zetu,”
alisema Mhe. Mgalula.
Katika
upande mwingine wajumbe wa JMAT Tawi la Manyara walitumia mkutano huo kujadili
masuala yao ambayo yatawasaidia katika kazi zao za kila siku lakini pia masuala
mbalimbali ambayo yanapaswa kufanywa na JMAT katika jamii inayowazunguka.
Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha JMAT Mahakama Kuu Kanda ya Manyara akifungua mkutano huo ulioambatana na mafunzo kwa Maafisa Mahakama hao wa Kanda hiyo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza (katikati) akiwa pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara katika mkutano huo
Sehemu ya Maafisa Mahakama walioshiriki mafunzo ya JMAT mkoani Manyara wakifuatilia mawasilisho ya mafunzo hayo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni