Jumatano, 14 Mei 2025

MAHAKAMA YA TANZANIA KUIMARISHA USIMAMIZI WA MAHAKAMA ZA WATOTO

Na ASHA JUMA –Mahakama, Morogoro

Katika juhudi za kuimarisha utoaji wa haki kwenye kesi za Watoto nchini, Mahakama ya Tanzania imeandaa kikao kazi maalum kupitia na kuboresha mwongozo wa usimamizi na ukaguzi wa Mahakama za Watoto.

Lengo la maboresho hay oni kuhakikisha kuwa haki za Watoto zinalindwa kwa mujibu wa viwango vya kitaifa na kimataifa.

Aidha, kikao cha siku tano kinachofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro kimekusudia kutathmini ufanisi wa uendeshaji wa Mahakama hizo, pamoja na kuandaa orodha ya vipengele muhimu vitakavyotumika katika ukaguzi wa Mahakama za Watoto kote nchini.

Kikao hicho kinahudhuriwa na Jaji wa Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Arusha, Mhe. Nyigulila Mwaseba ambaye ni Mwenyekiti na Maofisa wengine kutoka maeneo mbalimbali nchini. Kikao hicho pia kinahusisha Maofisa wa ndani wa Mahakama, wakiwemo Majaji na Mahakimu.

Ushirikiano huu unalenga kuhakikisha kuwa Mahakama za Watoto zinakuwa na mazingira rafiki na kwamba mashauri yanayowahusu Watoto yanashughulikiwa kwa weledi na kwa kuzingatia haki zao za msingi.

Muongozo wa awali wa usimamizi na ukaguzi wa uendeshaji wa Mahakama za Watoto ulifanyiwa marekebisho mwaka 2019 na sasa unafanyiwa mapitio ili kujumuisha vipengele mahususi vinavyohitajika kuzingatiwa katika ukaguzi wa Mahakama za Watoto.

Hii ni sehemu ya juhudi za Mahakama ya Tanzania kuhakikisha kuwa mfumo wa utoaji haki kwa Watoto unakuwa wa haki, wa haraka na unaozingatia maslahi bora ya Mtoto.

Mahakama ya Tanzania imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kuimarisha haki za Watoto, ikiwemo kuanzisha Mahakama za Watoto katika Mikoa mbalimbali na kutoa mafunzo kwa Majaji na Mahakimu kuhusu usikilizaji wa mashauri ya Watoto.

Kupitia kikao kazi hicho, Mahakama ya Tanzania inaendelea kuonesha dhamira yake ya dhati ya kuhakikisha kuwa haki za Watoto zinalindwa na kuendelezwa na kuimarisha mifumo ya usimamizi na ukaguzi wa Mahakama za Watoto nchini.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha, Mhe. Nyigulila Mwaseba (katikati) ambaye ni Mwenyekiti wa kikao kazi akiwa katika picha pamoja na Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Usimamizi, Ukaguzi wa Huduma za Kimahakama, Mrejesho kwa Umma na Maadili, Mhe. Karol Mashauri (kushoto) na Naibu Msajili   Mahakama Kuu, Masjala Kuu anayeshughulika Masuala ya Watoto, Mhe. Mwajabu Mvungi (kulia).

Maofisa wa kikao kazi-juu na picha mbili chini- wakiwa wanajadili masuala mbalimbali.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha, Mhe. Nyigulila Mwaseba (katikati) ambaye ni Mwenyekiti wa kikao kazi, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Usimamizi, Ukaguzi wa Huduma za Kimahakama, Mrejesho kwa Umma na Maadili, Mhe. Karol Mashauri (kushoto) na Naibu Msajili   Mahakama Kuu, Masjala Kuu anayeshughulika Masuala ya Watoto, Mhe. Mwajabu Mvungi (kulia) wakiwa pamoja na Maofisa wa kikao kazi-juu na chini.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni