Ijumaa, 16 Mei 2025

MANYARA YAANZISHA HUDUMA YA NIULIZE MIMI

Na Christopher Msagati – Mahakama, Manyara

Mahakama Kuu Kanda ya Manyara imekuja na mbinu mpya ya kuwahudumia wateja wanaofika Mahakama Kuu kusikiliza mashauri yao, mbinu hiyo ambayo imebuniwa inawawezesha watumishi wa Mahakama kuvaa makoti maalumu ambayo yana maneno ya “Niulize Mimi” na “Ask Me” katika eneo la kifuani na mgongoni. Aidha maneno hayo yanaonekana kirahisi na wateja ambao wanafika mahakamani na hawajui pa kwenda ili kupata huduma wanazozihitaji.

Akizungumza na watumishi wa Mahakama Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, Mhe. John Kahyoza ambaye pia ni mbunifu wa wazo hilo, aliwasihi watumishi kuendelee na kazi ya kuwahudumia wateja kwa kujitahidi kuzungumza na wateja wanaofika mahakamani ili kuwasaidia wateja hao wapate huduma kwa haraka lakini pasipo kubabaika.

“Wateja wengi wanaofika mahakamani hususani kwa mara ya kwanza, huwa wanapata shida kujua pa kuelekea ili waweze kupata huduma. Nawaelekeza kuvaa makoti haya na kupita katika eneo wanalokaa wateja wakati wakisubiri muda wa kusikilizwa kwa mashauri yao na kuwasikiliza matatizo na muweze kuwaelekeza mahali watakapopata huduma stahiki,” alisema Mhe. Kahyoza.

Naye, Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara, Mhe. Bernard Mpepo alitumia fursa hiyo kutoa Elimu kwa Wananchi wanaofika mahakamani kila siku ya Alhamisi kuwatambulisha watumishi walio na zamu ya kuwahudumia wananchi kwa wiki ambao ni Bw. Shadrack Aron na Bi. Ombeni Kazyoba ambao ni Wasaidizi wa Kumbukumbu kutoka Mahakama Kuu Manyara.

“Tumeanza huduma hii ya kuwahudumia wateja, hivyo hawa waliovaa makoti haya watakuwa wanapita na kuwasikiliza shida zenu, muwe wawazi na msiogope kusema changamoto mlizo nazo” alisema Mhe. Mpepo.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, Bi. Nyanzobe Hemedi akitoa ufafanuzi juu ya matumizi ya makoti hayo, alisema namna ambavyo ofisi yake ilivyofanikisha uratibu wa ubunifu huo.

“Ofisi ya Mtendaji wa Mahakama, imegharamia ushonaji wa Makoti hayo na uwekaji wa hayo maandishi yanayoonekana. Vile vile tunaratibu ratiba ya watumishi ambao watakuwa wanavaa makoti hayo kila wiki kwa lengo la kuwasikiliza na kuwahudumia wateja wetu wanaofika hapa”, alisema Bi. Nyanzobe.

Katika upande mwingine, wananchi wanaofika Mahakama Kuu Manyara wakiwakilishwa na Bw. Bakari Issa wameipongeza Mahakama Kuu Manyara kwa kubuni mbinu hiyo ambayo wanaona kwao itakuwa ya msaada kupata huduma kirahisi.

“Kwa kweli sisi wananchi wa kawaida tulio wengi, huwa tunapata hofu na mashaka tunapofika mahakamani kwa kuwa hatujui pa kuanzia, ubunifu wenu ni mzuri mno na kwa kweli mnastahili kupongezwa kwa sababu kuanzia sasa hatutapata tena shida ya kujua namna ya kupata huduma kwa kuwa tutakuwa tunawaona watu wa kuwauliza kwa kuwa pia wanakuja mpaka hapa katika eneo tulilokaa” alisema Bw. Bakari.

Kwa sasa Mahakama Kuu Manyara imeanza shughuli hii kwa kuwa na makoti hayo mawili ambayo yatakuwa yanavaliwa kwa zamu kila wiki na watumishi wawili ambao watakuwa wamepangwa kwenye ratiba ili waweze kuwahudumia wateja wanaofika mahakamani.

Aidha, makoti hayo yamepewa jina maarufu la “Niulize Mimi”. Vilevile Uongozi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara umeahidi kuendelea kubuni mbinu zaidi za kuwahudumia wateja wao ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha Malengo na Nguzo za Mpango Mkakati wa Mahakama zinatimia kwa ufasaha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza akizungumza na watumishi wa Mahakama kuwaeleza juu ya matumizi ya Makoti ya “Niulize Mimi” yatakayovaliwa na watumishi ambao watakuwa wanasikiliza shida za wateja wanaofika Mahakamani kila siku.

Wasaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Manyara Bi Ombeni Kazyoba na Bw. Shadrack Aron wakiwa wamevaa makoti ya “NIULIZE MIMI” wakiendelea na zoezi la kuwahudumia wateja waliofika katika Mahakama Kuu Manyara.

Baadhi ya wananchi wakiwasikiliza watumishi wa Mahakama waliokuwa wakiwapa huduma ya maelekezo katika eneo la kusubiria wateja katika viwanja vya Mahakama Kuu Manyara

Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemedi akieleza namna ambavyo ofisi yake imeratibu upatikanaji wa huduma ya “Niulize Mimi” huduma ambayo inamsaidia mteja kupata maelekezo ya namna ambavyo atahudumiwa.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo (wa kwanza upande wa kulia) akiwatambulisha watumishi waliovaa makoti ya “Niulize Mimi” kwa wananchi waliofika mahakamani ili waweze kuwahudumia.

Wasaidizi wa Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Manyara Bi. Ombeni Kazyoba na Bw. Shadrack Aron wakiwa wamevaa makoti ya “Niulize Mimi” wakiwa tayari kabisa kuwahudumia wateja waliofika Mahakama Kuu ya Manyara kwa ajili ya kusikiliza mashauri yao.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni