Na Christopher Msagati – Mahakama, Manyara
Mahakama
Kuu Kanda ya Manyara imekuja na mbinu mpya ya kuwahudumia wateja wanaofika Mahakama
Kuu kusikiliza mashauri yao, mbinu hiyo ambayo imebuniwa inawawezesha watumishi
wa Mahakama kuvaa makoti maalumu ambayo yana maneno ya “Niulize Mimi” na “Ask Me”
katika eneo la kifuani na mgongoni. Aidha maneno hayo yanaonekana kirahisi na
wateja ambao wanafika mahakamani na hawajui pa kwenda ili kupata huduma
wanazozihitaji.
Akizungumza
na watumishi wa Mahakama Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, Mhe.
John Kahyoza ambaye pia ni mbunifu wa wazo hilo, aliwasihi watumishi kuendelee
na kazi ya kuwahudumia wateja kwa kujitahidi kuzungumza na wateja wanaofika mahakamani
ili kuwasaidia wateja hao wapate huduma kwa haraka lakini pasipo kubabaika.
“Wateja
wengi wanaofika mahakamani hususani kwa mara ya kwanza, huwa wanapata shida
kujua pa kuelekea ili waweze kupata huduma. Nawaelekeza kuvaa makoti haya na
kupita katika eneo wanalokaa wateja wakati wakisubiri muda wa kusikilizwa kwa
mashauri yao na kuwasikiliza matatizo na muweze kuwaelekeza mahali watakapopata
huduma stahiki,” alisema Mhe. Kahyoza.
Naye,
Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara, Mhe. Bernard Mpepo alitumia fursa hiyo
kutoa Elimu kwa Wananchi wanaofika mahakamani kila siku ya Alhamisi kuwatambulisha
watumishi walio na zamu ya kuwahudumia wananchi kwa wiki ambao ni Bw. Shadrack
Aron na Bi. Ombeni Kazyoba ambao ni Wasaidizi wa Kumbukumbu kutoka Mahakama Kuu
Manyara.
“Tumeanza
huduma hii ya kuwahudumia wateja, hivyo hawa waliovaa makoti haya watakuwa
wanapita na kuwasikiliza shida zenu, muwe wawazi na msiogope kusema changamoto
mlizo nazo” alisema Mhe. Mpepo.
Kwa
upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, Bi. Nyanzobe Hemedi
akitoa ufafanuzi juu ya matumizi ya makoti hayo, alisema namna ambavyo ofisi
yake ilivyofanikisha uratibu wa ubunifu huo.
“Ofisi
ya Mtendaji wa Mahakama, imegharamia ushonaji wa Makoti hayo na uwekaji wa hayo
maandishi yanayoonekana. Vile vile tunaratibu ratiba ya watumishi ambao
watakuwa wanavaa makoti hayo kila wiki kwa lengo la kuwasikiliza na kuwahudumia
wateja wetu wanaofika hapa”, alisema Bi. Nyanzobe.
Katika
upande mwingine, wananchi wanaofika Mahakama Kuu Manyara wakiwakilishwa na Bw.
Bakari Issa wameipongeza Mahakama Kuu Manyara kwa kubuni mbinu hiyo ambayo
wanaona kwao itakuwa ya msaada kupata huduma kirahisi.
“Kwa
kweli sisi wananchi wa kawaida tulio wengi, huwa tunapata hofu na mashaka
tunapofika mahakamani kwa kuwa hatujui pa kuanzia, ubunifu wenu ni mzuri mno na
kwa kweli mnastahili kupongezwa kwa sababu kuanzia sasa hatutapata tena shida
ya kujua namna ya kupata huduma kwa kuwa tutakuwa tunawaona watu wa kuwauliza
kwa kuwa pia wanakuja mpaka hapa katika eneo tulilokaa” alisema Bw. Bakari.
Kwa
sasa Mahakama Kuu Manyara imeanza shughuli hii kwa kuwa na makoti hayo mawili
ambayo yatakuwa yanavaliwa kwa zamu kila wiki na watumishi wawili ambao watakuwa
wamepangwa kwenye ratiba ili waweze kuwahudumia wateja wanaofika mahakamani.
Aidha,
makoti hayo yamepewa jina maarufu la “Niulize
Mimi”. Vilevile Uongozi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara umeahidi
kuendelea kubuni mbinu zaidi za kuwahudumia wateja wao ikiwa ni sehemu ya
kuhakikisha Malengo na Nguzo za Mpango Mkakati wa Mahakama zinatimia kwa
ufasaha.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza akizungumza na
watumishi wa Mahakama kuwaeleza juu ya matumizi ya Makoti ya “Niulize Mimi” yatakayovaliwa
na watumishi ambao watakuwa wanasikiliza shida za wateja wanaofika Mahakamani
kila siku.
Wasaidizi
wa Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Manyara Bi Ombeni Kazyoba na Bw. Shadrack Aron
wakiwa wamevaa makoti ya “NIULIZE MIMI” wakiendelea na zoezi la kuwahudumia
wateja waliofika katika Mahakama Kuu Manyara.
Baadhi
ya wananchi wakiwasikiliza watumishi wa Mahakama waliokuwa wakiwapa huduma ya
maelekezo katika eneo la kusubiria wateja katika viwanja vya Mahakama Kuu
Manyara
Mtendaji
wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemedi akieleza namna ambavyo
ofisi yake imeratibu upatikanaji wa huduma ya “Niulize Mimi” huduma ambayo
inamsaidia mteja kupata maelekezo ya namna ambavyo atahudumiwa.
Naibu
Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo (wa kwanza upande
wa kulia) akiwatambulisha watumishi waliovaa makoti ya “Niulize Mimi” kwa wananchi waliofika mahakamani ili waweze
kuwahudumia.
Wasaidizi
wa Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Manyara Bi. Ombeni Kazyoba na Bw. Shadrack Aron
wakiwa wamevaa makoti ya “Niulize Mimi” wakiwa tayari kabisa kuwahudumia wateja
waliofika Mahakama Kuu ya Manyara kwa ajili ya kusikiliza mashauri yao.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni