Ijumaa, 9 Mei 2025

MSAJILI MKUU ASHIRIKI MKUTANO WA KAMATI YA WIPO YA MAENDELEO NA MILIKI BUNIFU

  •   Aeleza mafanikio ya ushirikiano kwa kipindi cha miaka sita

Na INNOCENT KANSHA na MAGRETH KINABO - Mahakama

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya jana tarehe 8 Mei, 2025 ameungana na Nchi wanachama na Mabalozi takribani 193 kushiriki mkutano wa Kamati ya Maendeleo  ‘Miliki Binifu’ ya Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) alioshiriki kwa njia ya mkutano mtandao akiwa Ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Akiuelezea ujumbe huo wa nchi wanachama wa shirika hilo wa Mabara yote Mhe. Nkya amesema Mahakama ya Tanzania imenufaika kwa kiwango kikubwa kutokana na kuwa sehemu ya shirika hilo la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) amebainisha kwamba, kupitia mashirikiano hayo,imewezesha kuwaongezea uelewa mkubwa wa masuala ya Miliki Bunifu kwa Maafisa Mahakama na kuongeza njia za kutatua migogoro inayotokana na kazi za miliki bunifu.

Aidha, Mhe. Nkya ametaja mafanikio mengine ni kutoa mafunzo kwa Maafisa Mahakama watapatao takribani 1,200 yaliyotokana programu ya Shirika hilo ya kubadilishana uzoefu.

“Takribani Maafisa Mahakama 404 walifanikiwa kushiriki mafunzo kwa njia ya masafa na kufuzu mafunzo ya sheria za haki bunifu na zaidi ya Maafisa 300 walishiriki makongomano ya Miliki Bunifu  kupitia Shirika hilo na kuwajenga uelewa mpana wa namna ya kuzitekeleza sheria zinazohusu  masuala ya Miliki Bunifu,” amesisitiza Msajili Mkuu.

Mafanikio mengine Mahakama ya Tanzania, iliyoyapata ni kwamba Majaji na Mahakimu   80  wakiwemo Majaji wa Mahakama ya Rufani, walipata walishiriki warsha za miliki bunifu kwa nyakati tofauti, ambapo Majaji hao hutoa maamuzi katika Mahakama ya ngazi ya mwisho ya utoaji wa haki nchini Tanzania.

Aidha, Mhe. Nkya amesema, kupitia ushiriki wa Tanzania Mahakama imeendelea kuwa mchangiaji mkubwa duniani katika utoaji wa maamuzi kuhusu miliki bunifu. Kuanzia mwaka 2019 jumla ya Majaji wapato 76 wamekuwa wakishiriki kwenye mkutano wa mwaka wa jukwaa la Majaji wa Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) ili kujiongezea uelewa na uzoefu kutoka kwa mamlaka zingine zinazotatua migogoro ya miliki bunifu.

Mbali na mafunzo ya mara kwa mara ya miliki bunifu, Mhe. Nkya amesema, ushirikiano umeisaidia Mahakama ya Tanzania kuandaa   miongozo ya kufundishia, mfano Mahakama imeandaa machapisho maalum ya kuendeshea mafunzo, kuandaa mkusanyiko wa vitabu vya maamuzi ya mashauri yahusuyo miliki bunifu, Vitabu Miongozo ambavyo vipo kwenye hatua ya mwisho ya maandalizi.

“Nyaraka hizo muhimu zitasaidia kutoa mwongozo na hadidu rejea kwa Maafisa Mahakama na zitachangia kukuza maendeleo ya taaluma na pia kusaidia ulinganifu wa tafsiri na kupunguza maamuzi yasiyoendani na kusaidia kujiamini kwa watoa maamuzi yanayohusu miliki bunifu,” ameongeza Msajili Mkuu.

Vilevile, Mahakama ya Tanzania mnamo mwaka 2022 ilisaini makubaliano na Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) ya kutoa na kusambaza maamuzi yatokanayo na mashauri ya miliki bunifu ili kuyachapisha kwenye kanzi data ya Shiriki ijulikanayo kama (WIPO Lex). Mpaka sasa ni maamuzi 41 ya mashauri ya miliki bunifu yamekwisha chapishwa ama kupandishwa kwenye mtandao huo wa Shirika na maamuzi mengine 39 yanafanyiwa mapitio kabla ya kuzichapisha.

Mhe. Nkya amesema, eneo lingine la ushirikianao ni kukuza matumizi na taratibu za usuluhishi, kupitia utaratibu huo wa WIPO na Mahakama imewezesha Majaji na Mahakimu wapatao 245 wameshafuzu mafunzo ya usuluhishi na upatanishi kwa njia masafa na Maafisa Mahakama wengine 159 wanendelea  kusoma kozi  maalum ya usuluhishi

“Mafanikio hayo ya usuluhishi na upatanishi yamewezesha Mahakama  kusuluhisha mashauri 26 ya miliki bunifu kwa. Aidha Majaji wa Kitanzania wanane,”  wameteuliwa kuwa wasuluhishi wa WIPO  ameongeza Msajili Mkuu.

Aidha, Mhe Nkya amesema kupitia program hizo mbalimbali za kuwajengea uwezo za shirika la WIPO zimewasidia Majaji na Mahakimu kuongeza uwezo na ujuzi wa kutosha wa kutoa haki kwa weledi na ufanisi katika eneo la mashauri ya miliki bunifu.

“Majaji na Mahakimu nchi nzima kwa sasa wanasikiliza mashauri ya miliki bunifu kwa uelewa, utaalum mkubwa na kwa kujiamini, hivyo kuchangia ufanisi na mashauri kuamriwa kwa wakati na kuondoa migongano katika kushughulikia migogoro ya miliki bunifu,” ameongeza Msajili Mkuu.

Vilevile, Mhe. Nkya amesema, ushirikiano huo umechangia kukuza ajenda ya maendeleo ya Taifa, kwani Mahakama yenye uwezo wa kutatua migogoro ya miliki bunifu kwa uthabiti na kwa kuzingatia sheria kunakuza ustawi na kuongeza imani kwa wananchi dhidi ya mfumo wa utoaji haki.

“Kwa kufanya hivyo inachangia uvumbuzi, kulinda ubunifu na kuhimiza uwekezaji wa ndani na wa nje ya nchi. Kuna nyakati miliki bunifu ilionekana kama masuala ya kiufundi na kutoyatilia mkazo, lakini kwa sasa yanatambulika kama nguzo ya kimkakati katika mageuzi ya kiuchumi nchini Tanzania,” amesema Mhe. Nkya. 

Kwa upande mwingine, kuhusu majadiliano ya nchi wanachama ilielezwa kuwa  kikao hicho kina malengo mbalimbali,  ikiwemo kujadiliana masuala ya maendeleo ya Nchi Wanachama, kubadilishana uzoefu kuhusu masuala ya Miliki Bunifu (IP), kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya nchi uanachama,  kuangalia maamuzi  yanayotolewa kuhusu suala hilo na kuendeleza program ya utoaji  elimu  kwa ajili ya kujengeana uwezo wa  kwenye  elimu na ujuzi juu Milki Bunifu

Katika mkutano huo, wa siku tano mambo mengine yaliyojadiliwa ni kuendana sambamba na mabadiliko ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kushughulikia mashauri yanayuhusu Miliki Bunifu kupitia uzoefu wa nchi  mfano; China, Ujerumani, India na nyinginezo. Pia kuangalia maamuzi ya Mahakama ya Juu nchini China (Supreme Court) na uzoefu wa Mahakama ya Juu ya Latvia.

Halikadhalika kutoa masaada kwa Majaji wanaoshughulikia mashauri ya IP, kutoa mwuongozo kwa Mabaraza ya Usuluhishi wa Migogoro ya Viwanda, Majaji wapya waeleweshe juu ya   masuala ya Milki Bunifu kutoka kwa wazoefu wa jambo hilo, kuangalia mikataba inayohusu Milki Bunifu  ikiwemo utoaji wa mafunzo kwa njia ya masafa.

Mambo mengine yaliyojadiliwa ni  kuangalia masuala ya Haki Miliki ya Bunifu  ya mtu, (Copy Rights), mizozo ya utumiaji  wa chapa za miliki ya mtu mwingine, mashauri yanayohusu mali za viwanda, utangazaji haramu wa matangazo ya kibiashara,  program (software), alama ya biashara na filamu(video), ikiwa ni hatua ya kuhakikisha utoaji wa haki za Milki Bunifu   unafanyika kwa viwango vinavyotakiwa.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya jana tarehe 8 Mei, 2025 ameungana na Nchi wanachama na Mabalozi takribani 193 kushiriki mkutano wa Kamati ya Maendeleo  ‘Miliki Binifu’ ya Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) kwa njia ya mkutano mtandao akiwa Ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya(kushoto) jana tarehe 8 Mei, 2025 ameungana na Nchi wanachama na Mabalozi takribani 193 kushiriki mkutano wa Kamati ya Maendeleo  ‘Miliki Binifu’ ya Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) uliofanyika kwa njia ya mkutano mtandao akiwa Ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.Kulia ni Mratibu  wa Shughuli za  WIPO Mahakama ya Tanzania.

Moja ya kazi zilizoandaliwa na Mratibu  wa Shughuli za  WIPO Mahakama ya Tanzania, Mhe.Upendo Ngitiri kwenye Mkutano huo.




  
Washiriki wengine wa Kamati hiyo.

Sehemu ya Mawasilisho mbalimbali kwenye mkutano huo


                    Sehemu ya Mawasilisho mbalimbali kwenye mkutano huo
     


(PICHA NA INNOCENT KANSHA- Mahakama)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni