Ijumaa, 4 Julai 2025

JAJI MFAWIDHI IRINGA AHITIMISHA ZIARA YA UKAGUZI NJOMBE

  • Ahitimisha kwa kukagua Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi Njombe
  • Amtaka Mkandarasi kuandaa mpango wa kumaliza mradi huo kwa wakati

Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru amehitimisha ziara ya ukaguzi wa Mahakama za Mkoa na Wilaya ya Njombe na baadhi ya Mahakama za mwanzo zilizo ndani ya Kanda ya Iringa huku akiwasisitiza watumishi wa Mahakama hizo kufanya kazi kwa kuzingatia maadili na kuiishi salamu ya Mahakama ya Tanzania inayojengwa na maneno ya Uadilifu, Weledi na Uwajibikaji.

Akizungumza na watumishi wa Mahakama hizo kwa nyakati tofauti alipotembelea Mahakama za Wilaya na alipohitimisha ziara ya ukaguzi wa robo ya nne  ya mwaka wa fedha 2024/2025 iliyofanyika mkoani Njombe, Mhe. Ndunguru aliwapongeza pia watumishi kwa utendaji kazi mzuri.

“Hii ni ziara ya ukaguzi wa kawaida ambao nimekuja kufanya kwa mujibu wa miongozo ya ukaguzi ya Mahakama ya Tanzania na kuona utendaji kazi wenu maana kama kukagua ningetumia hata mifumo ya TEHAMA kujua idadi ya mashauri na nikajua Hakimu yupi ana mashauri mengi yenye mlundikano ila nawasisitiza watumishi wote muishi kwenye dira ya Mahakama ya Tanzania haswa kujiepusha na vitendo vya utovu wa maadili hasa vitendo vya kupokea rushwa,” alisema Mhe.Ndunguru.

Jaji Ndunguru aliwasisitiza watumishi hao kufanya kazi kwa bidii, kushirikiana kwa upendo na umoja huku akiwasisitiza wawe na utaratibu wa kujisomea na kujiendeleza kielimu ili waweze kutimiza malengo yao huku akiwasisitiza watumishi kutunza afya zao hasa kuweka utaratibu wa kufanya mazoezi maana afya ni mtaji. Vilevile aliwataka watumishi wawe angalau mara moja au mbili kwa mwaka waweze kuwa na utaratibu wa kwenda kutembelea vivutio vya utalii wa ndani ili kujifunza mambo mengi ya nchi yetu.

 Kwa upande wa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe.Bernazitha Maziku   kwa nyakati tofauti akiwa Wilaya ya Wanging’ombe na Njombe alikiri kuwa utendaji kazi wa watumishi wa Mahakama hizo ni mzuri na unaridhisha kwa kiwango kikubwa na taarifa zao za hali ya mashauri katika Wilaya hizo zinavutia kutokana na kasi ya uondoshaji wa mashauri mahakamani.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa akizungumza na watumishi hao aliwashukuru watumishi wote katika Mkoa wa Njombe kwa kuendelea kuimarisha taswira Chanya ya Mahakama kwa jamii.

“Ni muhimu kila mtumishi kuwa muadilifu kwa kuwa mmeaminiwa na kupewa nafasi mnazotumikia hivyo, kuweni na weledi na uwajibikaji kwa kuwa kila mmoja ni mbobezi katika kada yake,” alisema Bi. Mkongwa.

Baada ya kikao hicho cha kuwaaga watumishi baada ya kuhitimisha ziara hiyo ya ukaguzi Mhe. Ndunguru aliogozana na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa, Naibu Msajili wa Mahakama kuu Kanda ya Iringa, Mhe.Bernazitha Maziku, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama pamoja na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Njombe, Mhe. Matilda Kayombo walitembelea Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe kinachoendelea kujengwa.

Baada ya kufika kwenye kituo cha utoaji haki Njombe kinachojengwa chini ya kampuni ya Shadong Mhe. Ndunguru alipokea taarifa fupi ya utekelezaji wa ujenzi ambapo ilibainishwa kuwa umefikia asilimia 81.5 kwa sasa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru (wa pili kushoto) akizungumza jambo na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Wilaya ya Njombe (hawapo katika picha). Wa kwanza kushoto ni Naibu Msajiri wa Mahakama kuu Kanda ya  Iringa , Mhe. Bernazitha Maziku, wa pili kulia ni Mtendaji wa Mahakama kuu kanda ya Iringa,Bi,Melea Mkongwa na wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru (wa pili kushoto) akiendelea kuzungumza na watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi na Wilaya ya Njombe. Wa kwanza kushoto ni Naibu Msajiri wa Mahakama kuu Kanda ya  Iringa , Mhe. Bernazitha Maziku, wa pili kulia ni Mtendaji wa Mahakama kuu kanda ya Iringa,Bi,Melea Mkongwa na wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama.

Baadhi ya
 watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe na Mahakama ya Wilaya Njombe wakimsikiliza Mhe. Dunstan Ndunguru (hayupo katika picha) alipokuwa akizungumza nao.


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru (katikati) na viongozi wengine Mahakama Iringa na Njombe wakiwa katika  
 picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Mkoa wa Njombe na Wilaya ya Njombe. 

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru pamoja na viongozi wengine wa Kanda hiyo wakifuatilia taarifa fupi ya utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe.

Ukaguzi ukiendelea.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya viongozi wa Mahakama Iringa na Njombe pamoja na mafundi katika eneo la Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe.  

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama- Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni