Ijumaa, 4 Julai 2025

JAJI MKUU ASISITIZA MAMBO SITA KWA CHAMA CHA MAWAKILI WA SERIKALI

Na FAUSTINE KAPAMA na ARAFA RUSHEKE-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju leo tarehe 4 Julai, 2025 amekutana na Viongozi wa Chama cha Mawakili wa Serikali na kuhimiza Wanachama kuzingatia mambo sita wanapotekeleza majukumu yao, ikiwemo kuisaidia Mahakama katika kufikia uamuzi wa haki.

Mambo hayo yaliyosisitizwa na Mhe. Masaju alipokutana na Viongozi hao ofisini kwake kwenye Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma ni umahiri (competence), uadilifu (integrity), umakini (proactive), ubunifu (creativity), uzalendo wa kitaifa (national patriotism) na kujali haki (sensitive to justice).

Viongozi hao ni Bavoo Junus (Rais), Debora Mcharo (Makamu wa Rais), Addo November (Mwenyekiti), Selestina Kunambi (Makamu Mwenyekiti) na Rashid Mohamed Said (Katibu).

Akizungumzia na Viongozi hao, Mhe. Masaju amesema kuwa ili Wanachama wa Chama cha Mawakili wa Serikali waweze kutekeleza majukumu yao kwa mafanikio makubwa wanatakiwa kuzingatia na kuyaishi mambo hayo sita.

Kuhusu suala ya umahiri, Jaji Mkuu ameeleza kuwa hilo limekuwa changamoto kubwa katika utumishi wa umma na kwamba watu wengine wanaamini ili kuwa mahiri lazima uwe na shahada nyingi.

‘Hapa ndipo tunapopotea, watu tutalazimika kusoma shahada hizi, lakini shahada yenyewe haikuletei umahiri. Tumejichanganya sana kwenye eneo hili, wakati fulani tunaenda kusoma kwa sababu ya vyeo. Tusome ili tuwe na hizi shahada, lakini zituwezeshe basi kuwa mahiri kwenye hilo eneo,’ amesema.

Mhe. Masaju amewaeleza Viongozi hao kuwa umahiri wa hali ya juu unahitajika kwa Wanasheria waliopo kwenye sekta ya umma katika kushiriki kwenye majukumu ya kusimamia utawala wa sheria, mikataba, kuendesha mashauri na kuishauri Serikali katika masuala mbalimbali.

Jaji Mkuu ameeleza pia kuwa suala la uadilifu ni jambo la msingi katika utumishi wa umma, hivyo amewasihi Wanachama wa Chama hicho kwenda kuwatumikia wananchi kwa kufuata misingi hiyo.

Akizungumzia suala la umakini, Mhe. Masaju amesema kuwa jambo hilo nalo limekuwa changamoto kwenye sekta ya sheria, hivyo Wanasheria wanatakiwa kujiongeza kwani mtu anaweza kujua majukumu yake na changamoto zilizopo, lakini hawezi kuchukua hatua mpaka asubiri mtu mwingine.

‘Kuna mambo mengi yanayotukabili, tusipokuwa makini tutakwama. Siku hizi kila kitu mpaka tusukumwe, tunapaswa kuwa wabunifu kwani changamoto ni nyingi. Lazima tuwe wabunifu kushughulikia hizi changamoto ili utumishi wetu ufanikiwe,’ Jaji Mkuu amesema.

Jambo jingine ambalo Wanachama wa Chama cha Mawakili wa Serikali wanatakiwa kuzingatia ni uzalendo kwa Taifa kwani wanabeba maslahi ya nchi. Mhe. Masaju amesema kuwa haitoshi kuwa mwadilifu, lazima pia Mwanachma aweke mbele maslahi ya umma.

Jaji Mkuu pia aliwaeleza Viongozi hao kuwa Wanachama wa Chama cha Mawakili wa Serikali wanatakiwa kujua wanajiandaa namna gani wanapoenda mahakamani, wanatoa ushauri gani wa kisheria kwenye maeneo mbalimbali, wanaguswa namna gani kwa watu wanaoonewa, wanafanya nini na nafasi yao ni ipi.

Akizungumza wakati wa ugeni huu, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani amewahimiza Wanachama wa Chama hicho kuendeleza utamaduni na mahusiano mazuri yaliyopo kati ya Mawakili wa Serikali na Mahakimu.

Naye Rais wa Chama hicho, kwa niaba ya Viongozi wenzake, alimshukuru Jaji Mkuu kwa kuwapa fursa ya kukutana naye kwa madhumuni ya kujitambulisha na kumpongeza kwa kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kushika wadhifa huo.

Kiongozi huyo alitumia fursa hiyo kukitambulisha Chama kwa Jaji Mkuu kwani bado nikichanga na mdau mkubwa kwa Mahakama. Aliomba ushirikiano wa Mahakama ya Tanzania kwenye maeneo mbalimbali, ikiwemo mafunzo.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju-juu na chini- akisisitiza jambo alipokuwa anazungumza na Viongozi wa Chama cha Mawakili wa Serikali alipokutana nao ofisini kwake kwenye jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 4 Julai, 2025.


Rais wa Chama cha Mawakili wa Serikali, Bw. Bavoo Junus akieleza jambo wakati Viongozi wa Chama hicho walipokutana na Jaji Mkuu ofisini kwake jijini Dodoma. 

Viongozi wa Mahakama ya Tanzania waliohudhuria kikao hicho. Kutoka kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya na Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert.

Viongozi wa Chama cha Mawakili wa Serikali. Kutoka kushoto ni Bavoo Junus (Rais), Debora Mcharo (Makamu wa Rais), Addo November (Mwenyekiti) na Selestina Kunambi (Makamu Mwenyekiti).

Kikao kikiendelea. Kiongozi wa kwanza kushoto ni Katibu wa Chama cha Mawakili wa Serikali, Bw.  Rashid Mohamed Said.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju-katikati-akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani-kulia na Rais wa Chama cha Mawakili wa Serikali, Bw. Bavoo Junus. Picha chini akiwa na Viongozi wengine wa Chama hicho.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni