Jumatatu, 7 Julai 2025

JAJI MFAWIDHI MTWARA AFANYA ZIARA YA UKAGUZI

Na HUBERT MAANGA-Mahakama, Mtwara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki hivi karibuni alifanya ziara kukagua utendaji kazi katika Mahakama za Mkoa wa Mtwara.

Katika ziara hiyo, Jaji Mfawidhi aliambatana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Bw. Yusuph Msawanga pamoja na Viongozi wengine.

Miongoni mwa Mahakama zilizokaguliwa ni Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mahakama za Wilaya Tandahimba, Newala, Nanyumbu na Masasi na Mahakama za Mwanzo Mahuta, Kitangali, Chikundi na Nanyumbu.

Katika ziara yake, Mhe. Kakolaki alikutana na watumishi na kupokea taarifa za utendaji kazi, kusikiliza changamoto zinazowakabili na kutoa maelekezo mbalimbali. Aidha, katika kila Mahakama ya Wilaya, aliongea na Mahakimu na kusisitizia utendaji wenye uadilifu.

Katika vikao na watumishi, Jaji Mfawidhi aliwapongeza kwa utendaji kazi mzuri hasa kumaliza mashauri kwa wakati, kutokuwa na mlundikano wa mashauri, kuzingatia unadhifu na ubunifu wa kuhifadhi nakala laini za hukumu na mwenendo wa mashauri kwa Mahakama za Mwanzo.

"Kwa mwenendo huu, huduma ya Mahakama itazidi kuonekana bora na kuzidi kuvutia wateja, kwa maana mteja atakapo pata haki yake na kuridhika na huduma yetu, atawashawishi hata wengine kuiamini Mahakama katika utoaji haki," alisema Jaji Mfawidhi.

Aidha, aliwapongeza Mahakimu kwa mafunzo yanayotolewa redioni na sehemu nyingine juu ya matumizi ya mifumo na manufaa yake, huku akiwasihi kuendelea kuwapa elimu wananchi.

Vilevile, aliwataka kuendelea kuwaelewesha wananchi kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA-katika usikilizaji mashauri na jinsi gani inavyosaidia kuondoa gharama, kupunguza muda kuwezesha wateja kuendelea na shughuli nyingine.

Katika kutekeleza maagizo ya Jaji Mkuu, aliwataka Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kuendelea kuchapa kesi zote kwenye mfumo ili kurahisisha upatikanaji wa nakala laini za mienendo ya mashauri.

Akizungumzia hali ya majengo ya Mahakama na vyombo vya usafiri, Mhe. Kakolaki aliagiza majengo yatunzwe kwa kutumia fedha za ndani zinazopatikana, magari na pikipiki yafanyiwe matengenezo mara kwa mara ili yaendelee kutumika kwa muda mrefu.

Aidha, Jaji Mfawidhi alihimiza Mahakama za Wilaya kuhakikisha maeneo yote ya Mahakama ambayo hayana hati miliki yanapatiwa ili kurahisha kuombea miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama.

Wakati wa ziara yake, Jaji Mfawidhi alikagua miradi miwili ya ujenzi ya Mahakama za Mwanzo Kitangari na Chikundi yanayoendelea katika Mkoa wa Mtwara na kuridhika na kasi na usimamizi wa ujenzi wa miradi hiyo.

Kadhalika, Mhe. Kakolaki alitembelea Magereza ya Lilungu, Newala na Masasi ambapo alipokea taarifa na kusikiliza changamoto za Wafungwa na Mahabusu na kuwashauri kujifunza na  kukuza vipaji vya elimu ya ujasiriamali kwa manufaa yao watakaporudi uraiani.

Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Masasi wakimpokea Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (wapili kushoto) akiteta machache na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Nanyumbu.

Hakimu Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Tandahimba, Mhe. Joseph Waruku (kulia) akiwasilisha taarifa ya Mahakama ya Wilaya Tandahimba mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akipanda mti katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Mahuta wilayani Tandahimba.

Ukaguzi wa ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Kitangari iliyopo Wilaya ya Newala kwa hatua iliyofikia hadi sasa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kulia) akizungumza na watumishi wa Mahakama ya Wilaya na Mkoa Mtwara.

Jopo la Wadau katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati), wakilitembelea Gereza la Lilungu.

Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Masasi katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (wa pili kulia).

Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Kitangari katika picha ya pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (wa tano kushoto) alipoitembelea Mahakama hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni