Jumamosi, 5 Julai 2025

JAJI MKUU, MAHAKAMA WAKABIDHIWA TUZO

  • Kutokana na mchango kwenye upatikanaji juzuu za sheria zaidi ya 400

Na FAUSTINE KAPAMA na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama, Dodoma 

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari amekabidhi Tuzo maalum kwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju na Mahakama ya Tanzania kutokana na mchango waliotoa kufanikisha upatikanaji wa Juzuu za Sheria 446 zilizofanyiwa urekebu.

Hafla ya kukabidhi Tuzo pamoja na nakala 20 ya Juzuu hizo ilifanyika katika Ofisi ya Jaji Mkuu iliyopo kwenye Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma na kuhudhuriwa na Viongozi kadhaa wa Mahakama, akiwemo Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya. 

Mwanasheria Mkuu wa Serikali aliabatana na Viongozi mbalimbali kutoka Ofisi yake kwenye hafla hiyo, wakiwemo Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi na Mwandishi Mkuu wa Sheria, Bw. Onorius Njole. Mhe. Masaju alipokea Tuzo ya Mahakama pamoja na Juzuu hizo kwa niaba ya Mahakama ya Tanzania.

Akizunguza katika hafla hiyo, Jaji Mkuu aliishukuru Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kutambua mchango wake binafsi na wa Mahakama ya Tanzania kwa ujumla katika kufanikisha zoezi la upatikanaji wa Juzuu hizo.

Alielezea namna yeye binafsi alivyoshiriki tangu akiwa katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na baadaye Ikulu na pia Mahakama ilivyotoa mchango wake kwenye hatua mbalimbali kufanikisha upatikanaji wa Juzuu hizo.

"Sisi ni watumiaji wakubwa wa Juzuu kama hizi maana mambo yote ya kisheria huishia mahakamani. Kwa hiyo, juzuu hizi ni muhimu sana kwetu," alisema.

Mhe. Masaju alisema kuwa ushirikiano uliopo kati ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mahakama udumu kwani ofisi hiyo ni Wadau wakubwa. 

Kabla ya kukabidhi Tuzo na Juzuu hizo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali alimweleza Jaji Mkuu kuwa wamefanya zoezi la urekebu wa sheria mbalimbali na baada ya kukamilisha zilizinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kutamka kuwa sheria hizo zitaanza kutumika kuanzia tarehe 1 Julai, 2025.

"Mpango wetu ulikuwa tukukabidhi kabla ya tarehe 1 Julai, 2025. Kutokana na mwingiliano wa majukumu pale bungeni mwishoni tulishindwa kukukabidhi mapema," alisema. 

Akizungumzia zoezi la urekebu wa sheria hizo, Mwandishi Mkuu wa Sheria alieleza kuwa seti waliyoleta ina Juzuu 20 zenye Sheria 446 na wameingiza marekebisho yote mpaka ya Mwezi Desemba 2023 na wanakamilisha marekebisho mengine ya mwaka 2024, ikiwemo Sheria za Uchaguzi. 

Alimweleza Jaji Mkuu kuwa zoezi hilo limekuwa la muda mrefu kama yeye anavyofahamu na amekuwa akiwasaidia kwenye kila hatua. Bw. Njole alisema pia kuwa zoezi hilo limefanywa na Watalaam wa ndani na uchapishaji umefanywa na kampuni ya Kitanzania. 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju-kushoto-akipokea moja ya tuzo zilizowasilishwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari. Kulia anashuhudia Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi. Picha chini, Jaji Mkuu akipokea moja ya nakala za Juzuu zilizowasilishwa kwake. 




Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju akizungumza kwenye hafla hiyo.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari-juu na chini-akitoa maelezo mafupi kabla ya kukabidhi Tuzo na Juzuu hizo kwa Jaji Mkuu, huku Viongozi wengine wakifuatilia kilichokuwa kinajiri. 



Mwandishi Mkuu wa Sheria, Bw. Onorius Njole akieleza mchakato wa upatikanaji wa Juzuu hizo ulivyokuwa.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju-kushoto-akiwa katika picha ya pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari baada ya hafla hiyo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju-katikati-akiwa na katika picha ya pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani-kushoto-na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju-katikati-akiwa na Viongozi wa Mahakama ya Tanzania na sehemu ya ujumbe kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

 Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju-katikati-akiwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani-wa nne kushoto- pamoja na ujumbe kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni