Jumatano, 6 Agosti 2025

IJA, MAHKAMA ZANZIBAR ZASAINI MAKUBALIANO YA KUWAJENGEA UWEZO MAAFISA MAHAKAMA NA WATUMISHI

Na Yusufu Ahmadi- IJA

Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) na Mahkama ya Zanzibar zimesaini Hati ya Makubaliano  (MoU) ikiwa ni hatua muhimu katika kuimarisha ufanisi na uwezo wa Maafisa wa Mahakama na maafisa wengine wakiwemo Makadhi kupitia mafunzo, utafiti na uendelezaji wa uwezo wa kitaasisi.

Makubaliano hayo yamesainiwa leo tarehe 5 Agosti 2025 Chuoni Lushoto baina ya Maafisa wa Chuo na wa Mahkama ya Zanzibar na kushuhudiwa na Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla pamoja na Mkuu wa Chuo ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo.

Miongoni mwa maeneo ya makubaliano hayo ni kutoa mafunzo kwa maafisa wa Mahkama na wengineo wa Mahkama ya  Zanzibar,  kuandaa na kutoa mafunzo ya uongozi na usimamizi, na kukuza uwezo wa utafiti wa kisheria na uvumbuzi katika utendaji wa Mahakama.

Maeneo mengine ni kutoa mafunzo endelevu ya Kimahakama, mafunzo ya muda mrefu na mfupi kwa watendaji wa Mahkama ya Zanzibar pamoja na kuandaa kwa pamoja warsha, makongamano, semina na mikutano ya kitaaluma.

Akizungumzia utiaji saini huo Mhe. Dkt. Kihwelo amesema kuwa Chuo kitahakikisha makubaliano hayo yanafikia malengo yake kwa kutoa mafunzo kwa makundi yaliyokusudiwa katika makubaliano hayo.

Pia ameongeza: “Makubaliano haya ni sehemu ya Chuo kuimarisha upatikanaji wa haki kwa kuwajengea uwezo maafisa wenzetu wa Mahkama na makundi mengine na hivyo kuimarisha ufanisi wa utendaji.”

Kwa upande wake, Mhe. Abdalla ameelezea imani yake kuwa makubaliano haya yatazaa matunda.

“Ni matarajio yangu na Mahkama ya Zanzibar kwamba mashirikiano haya yatazaa matunda kwa maslahi ya Mahkama, Chuo na Tanzania kwa ujumla,” amesema Mhe. Abdalla.

Pia ameongeza kuwa IJA na Mahkama ya Zanzibar vimekuwa na ushirikiano kwa miaka mingi na kwamba makubaliano haya ni sehemu ya kurasimisha ushirikiano huo uliyodumu kwa muda mrefu.

Awali, Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo ya Mahkama ya Zanzibar ambaye pia ni Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Khadija Shamte Mzee amebainisha kuwa walifanya tathminii ili kujua ni maeneo gani ya mafunzo wao hawako vizuri, na hivyo kuamua kuingia makubaliano na IJA ili kuwezesha maeneo hayo.

Makubaliano hayo yameshuhudiwa na wajumbe wengine wa Mahkama ya Zanzibar na Wajumbe wa Menejimenti ya Chuo.

 Wajumbe wa IJA wakiwa katika hafla hiyo ya utiaji saini.

 

Maafisa wa IJA na wa Mahkama ya Zanzibar wakisaini hati za makubaliano

Mkuu wa Chuo Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo akizungumza katika hafla hiyo.

Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo ya Mahkama ya Zanzibar ambaye pia ni Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Khadija Shamte Mzee akisema jambo.


Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla akizungumza katika hafla hiyo

Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa  Menejimenti ya IJA.

Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Mahkama ya Zanzibar wakati wa hafla ya kusaini Hati ya Makubaliano (MoU) baina ya IJA na Mahkama hiyo ya Zanzibar. Kushoto ni  Mkuu wa Chuo Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo na kulia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo ya Mahkama ya Zanzibar ambaye pia ni Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Khadija Shamte Mzee.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni