Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama
Kituo Jumuishi cha
Masuala ya Familia Temeke jana tarehe 6 Agosti, 2025 kilikutana na Wawakilishi
wa Mabenki Mkoa wa Dar es salaam kujadili na kupata uelewa wa pamoja kuhusu
marekebisho ya kanuni yaliyofanywa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kwa
Msimamizi wa Mirathi kufungua akaunti moja maalum ya kuhifadhi fedha za
marehemu wakati wa usikilizaji wa mashauri ya mirathi.
Kutokana na marekebisho
hayo, fedha za mirathi zitakuwa zinawekwa katika akaunti maalum inayoitwa ‘Special
Mirathi Account’ badala ya kuwekwa katika akaunti ya mirathi ya Mahakama kwa
utaratibu wa awali.
Msimamizi wa Mirathi atafungua
akaunti hiyo itakayopokea fedha za mirathi za kutoka Taasisi mbalimbali za
fedha badala ya fedha hizo kuwekwa katika akaunti ya mirathi mahakamani.
Akizungumza wakati
anafungua majadiliano hayo, Jaji Mfawidhi, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa aliwaeleza
Wadau hao kuwa kabla ya marekebisho ya Kanuni za Mirathi, kupitia Tangazo la
serikali Na 429 la 2025, fedha za mirathi kutoka Taasisi za fedha zilikuwa zikiwekwa
katika akaunti moja ya Mahakama inayoitwa ‘Judiciary Mirathi Account.’
Alieleza kuwa kufuatia
marekebisho hayo wameona ni vema wakakutana na Wadau hao muhimu wa Mahakama
hiyo ili kujadiliana na kuwa na uelewa wa pamoja namna ya utekelezaji, kwani
kwa sasa takwa la kisheria kwa Msimamizi wa Mirathi ni kufungua akaunti maalum
inayoitwa ‘Special Mirathi Account’ katika benki yoyote atakayoona inafaa kwa
ajili ya kuhifadhi fedha za marehemu zitakazotoka katika taasisi nyingine za
fedha, ikiwemo mabenki.
Jaji Mfawidhi alisema
kuwa maoni ya Wadau hao ni muhimu kwa sababu yatasaidia kuweka utaratibu ambao
ni sahihi ili mnufaika asiweze kupata changamoto yoyote na pia itasaidia
kuondoa tofauti kati ya Taasisi moja na nyingine au benki moja na nyingine
wakati wa utekelezaji wa marekebisho ya kanuni hizo.
‘Leo hii Mwenyezi Mungu
ametujalia tupo hai, lakini hatuwezi kujua kesho tutakuwa hatupo. Kwa hiyo,
tukiweka mifumo thabiti itatusaidia. Tukiondoka lazima tutaacha mali na moja ya
mali ni fedha kwenye akaunti zetu ndani ya mabenki mbambali. Jambo la kujiuliza
ni kwamba usimamizi wa hizo fedha utakuwaje ili wanufaika wazipate,’ alisema.
Alibainisha kuwa hapo
awali mtu akifariki na kuteuliwa Msimamizi wa Mirathi, Msajili wa Mahakama Kuu
au Hakimu Mfawidhi katika Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mwanzo walikuwa
wanaandika barua kuomba kufunga akaunti na fedha katika mabenki kuhamishwa kwenda
katika akaunti ya Mahakama.
‘Lakini, kutokana na
mabadiliko ya Kanuni za Mirathi, kupitia Tangazo la Serikali Na 429 la 2025,
kwa sasa fedha hizo zitakuwa hazipelekwi tena katika akaunti hiyo ya Mahakama.
Msimamizi wa Mirathi anatakiwa kufungua akaunti moja maalum ya mirathi
itakayopokea fedha toka taasisi nyingine kama mabenki mbalimbali, hata kama
marehemu atakuwa na akaunti zaidi ya moja kwenye benki tofauti,’ Mhe. Mnyukwa
alisema.
Jaji Mfawidhi aliwaeleza
Wadau hao kuwa walikuwa wanakutana na changamoto nyingi wakati wa kuendesha
akaunti moja ya Judiciary Mirathi Account, ikiwemo kutokujua mapema fedha
zilizoingizwa zinatoka kwa marehemu yupi.
‘Ukimwandikia barua
Msimamizi wa Mirathi kufunga akaunti ya fedha za marehemu kwenye mabenki, fedha
zinaweza kuingia kwenye akaunti yetu, lakini kwa haraka tunaweza tusigundue ni
za marehemu yupi...
‘Mkumbuke tunahudumia
wakazi wote wa Mkoa wa Dar es Salaam, tuna Mahakama za Mwanzo, Mahakama za
Wilaya na Mahakama Kuu na kwa siku moja zinaweza kutoka amri zaidi ya kumi na
fedha zinaingia kwenye kapu moja,’ Mhe. Mnyukwa aliwaeleza Wadau hao.
Wakati wa majadiliano
hayo, Kituo Jumuishi kilijadiliana na Wadau kwa kina ili kupata uelewa wa
pamoja wa namna ya ufunguaji wa akaunti husika kwa kila marehemu anaefunguliwa
maombi ya mirathi, usalama wa fedha za mirathi hiyo na namna ya kukabiliana na changamoto
zinazoweza jitokeza katika utaratibu huo mpya.
Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa [juu na chini] akizungumza wakati anafungua majadiliano na Wawakilishi wa Mabenki Mkoa wa Dar es Salaam kujadili na kupata uelewa wa pamoja kuhusu marekebisho ya kanuni kwa Msimamizi wa Mirathi kufungua akaunti moja ya kuhifadhi fedha za marehemu wakati wa usikilizaji wa mashauri ya mirathi.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni