Jumamosi, 23 Agosti 2025

WANANCHI KIGOMA WAVUTIWA KUSIKILIZA HUKUMU KWA NJIA YA MAHAKAMA MTANDAO

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Zaidi ya wananchi 50 walikusanyika katika viunga vya Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma kusikiliza hukumu ya Shauri la Jinai na. 5546 ya mwaka 2024 Jamhuri dhidi ya Athuman Francis Msabila na watumishi wenzake 10 walioshitakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma kwa makosa nane yaliyotendeka katika ofisi ya umma.

Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yametumika vema katika kuhakikisha wananchi wote wanapata fursa sawa ya kusikiliza usomwaji wa hukumu hiyo huku wakiwa wameketi katika viti vya kupumzikia wateja wanaposubiria huduma za kimahakama.

Akisoma hukumu hiyo tarehe 21 Agosti, 2025 kwenye ukumbi wa Mahakama ya wazi katika Jengo la Mahakama Kuu Kigoma, Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Misana Majula alitumia Mahakama Mtandao (Virtual Court) ili wananchi waliokosa nafasi katika ukumbi wa wazi nao walipata fursa ya kusikiliza kwa ufasaha hukumu iliyosomwa takribani saa 6 mahakamani hapo.

Aidha, Mhe. Majula, alibainisha kuwa washitakiwa 11 walishtakiwa mahakamani hapo kwa makosa nane na upande wa mashtaka uliweza kuthibitisha makosa mawili bila kuacha shaka katika kosa la utakatishaji fedha za shilingi za Kitanzania milioni 463.5 na kosa la kugushi nyaraka kati ya makosa nane waliyoshtakiwa nayo.

Aidha, Mahakama hiyo imewatia hatiani Mshtakiwa nambari moja aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji, Bw. Athumani Francis Msabila na Mshtakiwa namba tano aliyekuwa Mhasibu wa Halmashauri ya Manispaa Kigoma Ujiji, Bw. Salum Juma Said na kutoa adhabu ya kifungo cha miaka 20 jela kwa kosa la utakatishaji fedha na la kugushi, ambapo washtakiwa wote wanne (4), yaani namba moja, nne, tano na 10, ni aliyekuwa Afisa Uchumi na Mipango, Bw. Frednand Filimbi na Afisa mipango Frank Nguvumali wamehukumiwa kifungo cha miaka miwili Jela na adhabu zote zitakwenda kwa pamoja kwa washtakiwa wawili wa kosa la kwanza.

Hakimu huyo aliendelea kubainisha akisoma hukumu hiyo kuwa, Washtakiwa saba (7) kati ya 11 katika kesi hiyo, upande wa mashtaka umeshindwa kuthibitisha kosa dhidi yao katika makosa yote nane, hivyo, Mahakama hiyo imeshindwa kuwatia hatiani na imewaachia huru bila masharti yoyote na majina ya washtakiwa hao ni Bw. Moses Zahuye,  Bw. Joel Shirima, Jema Mbilinyi, Kombe Kabichi na Bayaga Ntamasambilo kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma.

Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) sasa ni dhahiri na ni nyenzo muhimu ndani ya Mahakama ya Tanzania. Hatua hiyo inadhihirishwa na jitihada mbalimbali ambazo zinaendelea kufanywa na Mahakama zote nchini ikiwemo Mahakama Kuu Kigoma kutumia teknolojia katika kuwahudumia wananchi katika mashauri yote ya rufaa, maombi pamoja na mashauri yenye mvuto wa kisiasa kwa wananchi.

Picha ya wananchi wakifuatilia kwa makini hukumu  ikisomwa na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Misana Majula kwa njia ya Runinga iliyopo katika eneo la kusubiria huduma kwa wateja wanaofika mahakamani kupata huduma mbalimbali.


Sehemu ya  wananchi waliokuwa wakifuatilia usomwaji wa hukumu kwa njia ya Runinga iliyokuwa ikionesha picha mjongeo kutoka ukumbi wa Mahakama ya Wazi uliopo katika Jengo la Mahakama Kuu Kigoma tarehe 21 Agosti, 2025.


Picha ya wananchi waliofika katika ukumbi wa Mahakama ya Wazi kushuhudia kusomwa kwa hukumu ya watumishi 11 wa Halimashauri ya  Manispaa Kigoma Ujiji wakiongozwa na aliyekuwa Mkurugenzi, Bw. Athumani Francis Msabila.

Picha ya kiti cha mamlaka ya Mahakama kilichotumiwa na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Misana Majula alipokuwa akisoma hukumu ya kesi ya jinai katika ukumbi wa Mahakama ya Wazi akiwa ameunganishwa na vifaa vya TEHAMA ili kutoa fursa kwa wananchi waliokuwa katika eneo la nje ya ukumbi huo kufuatilia hukumu hiyo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni