· Jaji Kiongozi naye asema Machifu wana
mchango mkubwa katika usuluhishi wa migogoro
Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Jaji
wa Mahakama ya Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija ametoa
rai kwa Machifu nchini kuendelea kuwa mabalozi wa utoaji elimu ya Mahakama kwa
jamii.
Mhe.
Mwarija alieleza hayo tarehe 16 Septemba, 2025 wakati Machifu kutoka Mikoa
ya Kusini walipomtembelea Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ofisini kwake Makao
Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.
Jaji
Mwarija alisema kuwa, suala la utoaji elimu ya Mahakama ni muhimu kuzingatiwa
ambapo alisema, “kuna desturi moja ya watu wetu, mtu anayeshinda kesi
ananyamaza kimya, anayeshindwa anapiga kelele kwahiyo ukiona Mahakama
inalaumiwa mara nyingi ni wale ambao wameshindwa kesi kwa mujibu wa sheria
kabisa lakini wale walioshinda hawatokezi wakisema kuna haki mahakamani, kwa
hiyo sasa nyie kwa vile mpo karibu zaidi na jamii ni muhimu mlisemee hilo na kuelimisha
jamii ili kujua kuwa Mahakama inafanya kazi kwa mujibu wa sheria.”
Mhe.
Mwarija alisema, sasa hivi, Mahakama ina Mahakimu hadi wa Mahakama za Mwanzo
ambao wana Shahada za Sheria kwahiyo wapo karibu zaidi na kule ambako Machifu wapo
hivyo inapotokea kwamba wanahitaji kujifunza kuhusu jambo fulani hasa kuhusu masuala
ya haki inawezekana kwa wakati wowote.
Aliongeza
kwa kuwaomba Machifu hao kuendelea kuwa macho ya Mahakama na kushiriki kutoa
baadhi ya mitazamo hasi ya jamii kwa Mhimili huo.
Akizungumzia
kuhusu Kongamano la Machifu wa Mikoa ya Kusini, Mhe. Mwarija amewapongeza
Machifu hao na kusema kwamba wamefanya vizuri na kurudisha mshikamano baina yao
na kwamba Mahakama pia ipo tayari kushirikiana nao.
Kadhalika,
Mhe. Mwarija aliwasihi Machifu hao kuendelea kusimamia maadili ya vijana kwa
kuwa yanaporomoka kwa kiasi kikubwa.
“Maadili
ya vijana kwakweli yanaporomoka sana labda sio vijana tu lakini hata watu
wazima kwa hiyo sasa kazi ya Machifu inazidi kuwa ni ya muhimu sana na naunga
mkono kama mlivyosema mtambulike kisheria, nadhani Jaji Mkuu yupo kwenye nafasi
nzuri ya kusaidia kuhimiza hili ili mamlaka husika ziweze kusaidia katika
hili,” alisema Jaji Mwarija.
Aidha,
Mhe. Mwarija aliwapongeza Machifu hao kwa kuwa na maono mpaka ya kuanzisha
Asasi ambapo alisema kwamba ni hatua nzuri kwani Machifu wa sasa wanakwenda
kulingana na mazingira ya sasa tofauti na wale wa zamani.
“Niseme
tu kwamba ugeni huu ambao umetutembelea ni wa baraka sana na muhimu pia kwetu
Mahakama kwa sababu ya majukumu ya Machifu wanakuwa sehemu ya wadau wetu wa
haki kwa sababu wanasimamia maadili ya jamii, utamaduni na hata kulinda
mazingira,” alisema Jaji Mwarija.
Akitoa
neno wakati wa mazungumzo kati ya Machifu hao na Jaji Mkuu, kwa upande wake Jaji
Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani alisema
kuwa mchango wa Machifu katika kuhakikisha kwamba jamii zinakaa kwa amani na
usalama ni mkubwa na haupaswi kuupuzwa.
“Sisi
kama Mahakama tumeanza kushirikiana nao japo si kwa ukubwa sana lakini tumeanza
kuwatambua, Kituo chetu kile cha Usuluhishi Mahakama Kuu Dar es Salaam kwa
miaka kama miwili sasa mfululizo kimekuwa kikiwatambua Viongozi wa jadi na
Machifu wanaofanya vizuri kwenye usuluhishi,” alisema Jaji Kiongozi.
Aliongeza
kwa kutoa mfano wa mwaka jana Mahakama ilipata Machifu wawili ambapo mmoja ni
Chifu wa Morogoro (Kingalu) ambaye anafanikiwa kwa kiasi kikubwa kwenye
usuluhishi na mwingine ni wa Lindi ambaye kwa kiasi kikubwa alifanya usuluhishi
kusababisha Mahakama ya Mwanzo kukosa kesi.
“Kwakweli
usuluhishi ambao ndio hasa Viongozi wetu wa asili na Machifu wamekuwa
wakiufanya una nafasi kubwa sana ya kuleta utulivu tofauti kabisa na sisi
tunavyosikiliza mashauri, sisi tunaposikiliza mashauri mmoja tu atashinda na
mwingine atashindwa hakuna nafasi ya kutoka sawa ‘draw’ na hiyo inatengeneza
uadui, aliyeshindwa atatengeneza uadui kwa Hakimu lakini pia kwa yule
aliyeshinda,” alisema Mhe. Dkt. Siyani.
Kadhalika,
Jaji Kiongozi alisema kwamba, Machifu wanafanya kazi kubwa ambayo inatakiwa
kutambulika zaidi kwa kuwa historia ya nchi pia inaonesha mchango wao hivyo ni
muhimu kuangalia namna ya kuwatumia vizuri zaidi bila kuleta mgongano wa
majukumu.
Kadhalika,
Mhe. Dkt. Siyani alitoa rai kwa Machifu hao kuendelea kutoa elimu na kuangalia
namna ambavyo wanaweza kufanya kazi zao katika mazingira ya sasa bila kuleta
mgongano ya kuonesha kwamba pengine wanaingilia majukumu ya Mahakama au
kuingilia majukumu ya Mabaraza ya Kata.
Machifu
hao kutoka Mikoa ya Kusini inayojumuisha mikoa ya Lindi, Ruvuma, Mtwara,
Iringa, Morogoro, Njombe, Rukwa, Songwe na Mbeya waliongozwa na Mkurugenzi
Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Akida Wabu (AWADEF), Prince Ibrahim Samata
ambaye pamoja na mambo mengine alimueleza Jaji Mkuu kwamba lengo la kuanzisha
Shirika hilo kuwa ni kuhifadhi urithi wa kitamaduni wa Tanzania, uhifadhi na
utunzaji wa mazingira, utawala bora, kukuza maendeleo endelevu na kuwezesha
kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha maisha ya Watanzania.
“Tumepanga
kufanya Semina ya kuwajengea uwezo Machifu wa Mikoa hiyo ya kusini ambayo
itakusanya Machifu takribani 200 kutoka kwenye mikoa hiyo tisa ili pamoja na
mambo mengine kuwajengea uwezo katika masuala ya uongozi, masuala ya maadili,
masuala ya malezi na makuzi na kuwaongezea uelewa juu ya mifumo ya Taasisi
mbalimbali zinavyofanya kazi ikiwemo Mahakama kama Chombo cha haki ambacho
kimeendelea kuaminiwa na Watanzania tangu enzi hizo na enzi hizi,” alisema
Prince Samata.
Ugeni
wa Machifu hao umekuwa na faida kwa Mahakama kufuatia Mahakama kupatiwa ardhi
ya hekari 56 wilayani Ikungi ambayo imetolewa na Chifu Adamu Gwau wa Wilaya
hiyo na Machifu wengine wa Mikoa ya Kusini nao wameahidi kutoa ardhi kwa
Mahakama kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ili kuwafikia wananchi hadi katika
ngazi za Kata.
Jaji wa Mahakama ya Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija akizungumza na sehemu ya Machifu kutoka Mikoa ya Kusini (hawapo katika picha) wakati Machifu hao walipomtembelea Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania tarehe 16 Septemba, 2025 ofisini kwako Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akizungumza na sehemu ya Machifu kutoka Mikoa ya Kusini (hawapo katika picha) wakati Machifu hao walipomtembelea Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania tarehe 16 Septemba, 2025 ofisini kwako Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Mazungumzo kati ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Machifu kutoka Mikoa ya Kusini yakiendelea wakati Machifu hao walipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma tarehe 16 Septemba, 2025.
Picha ya pamoja na Machifu. Katikati ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija, wa pili kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa kwanza kushoto ni Chifu Mkuu wa Wayao Tanzania na Mwenyekiti wa Asasi ya Maendeleo ya Akida Wabu (AWADEF), Chifu Saad Wabu Mussa Mitondo II na wa kwanza kulia ni Chifu wa Wilaya ya Ikungi-Singida, Bw. Adam Gwau.
(Picha na MARY GWERA, Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni