Jumatatu, 22 Septemba 2025

WATUMISHI MAHAKAMA LINDI WAPATA ELIMU YA AFYA YA AKILI

Na. Hilary Lorry – Mahakama, Lindi

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi, Mahakama ya Wilaya ya Lindi pamoja na Mahakama ya Mwanzo Lindi mjini wameshiriki mafunzo maalum ya afya ya akili yaliyoandaliwa kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kukabiliana na changamoto ya afya ya akili.

Mafunzo hayo yametolewa na mtaalamu wa afya ya akili, Dkt. Monica Gloria katika ukumbi wa wazi wa Mahakama ya Hakimu MKazi Lindi tarehe 19 Septemba, 2025.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela amewataka watumishi hao kuyazingatia watakayo fundishwa na daktari huyo bingwa wa Afya ya akili kwani suala la changamoto ya afya ya akili limekuwa likiwasumbua watu wengi.

“Natamani kila moja asikilize kwa umakini mambo yote yatakayofundishwa hapa ili tujijengee uwezo wa kukabili changamoto za afya ya akili, naamini elimu hii itatusaidia kukabili changamoto za afya ya akili mahala pa kazi, katika familia zetu na hata kwa jamii inayotuzunguka” alisema Mtendaji huyo”.

Kwa upande wake, Dkt. Monica amebainisha kuwa changamoto ya  afya ya akili ni ya kweli  na  imekuwa ikiathiri utendaji kazi wa watumishi wengi katika maeneo mbalimbali hasa katika kutekeleza majukumu yao.

Vilevile Dkt. Monica alifundisha mambo yanayoweza kupelekea mtu kuwa na changamoto ya afya ya akili, dalili/ishara za changamoto ya afya ya akili na jinsi ya kukabili changamoto ya afya ya akili pamoja na  njia tano zinazoweza kusaidia  kukabiliana na msongo ambao unapelekea changamoto ya afya ya akili, njia hizo ni kuishi  (Five A’S ambazo ni  Avoid, Act, Alter, Accept And Adopt) akifafanua  vipengele hivyo alisema tunatakiwa  kujiepusha na mambo yanayosababisha Msongo, kufanya mambo yatakayo kuepusha na msongo wa mawazo, kuzungumza  mambo yanayokusababishia msongo kwa mtu unayemwamini,kukubaliana na hali na mazingiza na mwisho kuishi katika hali yako kwakuzingatia mazingira yako. 

“Tukifanikiwa kuishi mambo hayo matano basi tutakuwa tumefanikiwa kupambana na tatizo la afya ya akili,” ameeleza Dkt. Monica, huku akihamasisha watumishi hao kujijengea tabia ya kujitambua na kutafuta msaada mapema pindi wanapohisi mabadiliko katika afya ya akili.

Uongozi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi umeweka bayana kuwa Mafunzo haya yatakuwa endelevu na sehemu ya mikakati ya kuboresha ustawi wa watumishi na kuongeza ufanisi katika utendaji wa kazi. 

Daktari kutoka hospitali ya Rufaa ya Sokoine Lindi Bi. Monica Gloria (aliyesimama mbele) akitoa elimu ya afya ya akili kwa watumishi wa Mahakama ya Lindi (hawapo kwenye picha).


Msaidizi wa Kumbukumbu Mwandamizi Bw. Selemani Chikumba (aliyesimama) akitoa neno la shukrani kwa niaba ya watumishi baada ya Mafunzo.

Watumishi wa Mahakama ya Lindi wakifuatilia kwa makini Mafunzo ya Afya ya akili yaliyowasilishwa Dkt. Monica.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip godfrey Mbeyela (kushoto) akiwa na Hakimu Mkazi Mahakama ya Wilaya ya Lindi Mhe.Khalfan O. Khalfan (kulia) wakifuatilia mafunzo hayo.

Hakimu Mkazi Mahakama ya Wilaya ya Lindi Mhe. Khalfan O.Khalfan Akichangia mada wakati wa Mafunzo.


Mkaguzi wa ndani Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bw. Faustine Peter Alo (benchi la pili kutoka mbele kushoto) akiuliza jambo wakati wa Mafunzo.

















Hakuna maoni:

Chapisha Maoni