Ijumaa, 3 Oktoba 2025

MAHAKAMA KANDA YA MOSHI YATATUA CHANGAMOTO ZA WAFUNGWA, MAHABUSU WA MAGEREZA YA SAME, ROMBO

·      Watuma salamu za shukrani kwa Jaji Mkuu kufuatia hatua ya kuhakikisha watuhumiwa wote Mahakama za Mwanzo kudhaminiwa au kujidhamini

·       Wasifu hatua ya kupatiwa nakala za hukumu na mienendo kwa wakati

·       Wakoshwa na uendeshaji wa mashauri kwa Mahakama Mtandao

Na PAUL PASCAL, Mahakama-Moshi

Mahakama Kuu Kanda ya Moshi imefanikiwa kutatua changamoto ya utoaji wa mienendo ya mashauri na nakala za hukumu kwa wafungwa na wadaawa wote katika mashauri yaliomalizika na yanayoendelea kumalizika kwa asilimia 100 na kusaidia kupunguza malalamiko kwa kiasi kikubwa.

Hayo yalibainishwa hivi karibuni wakati wa ziara ya ukaguzi wa Mahakama za Wilaya na Magereza ya Wilaya za Same na Rombo kwa Robo ya kwanza ya Mwaka wa Fedha 2025/2026 iliyofanywa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella.

Akitoa salamu za ukaribisho wakati wa ukaguzi huo pamoja na kusoma taarifa fupi ya Gereza la Wilaya Same, Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Same, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Ipyana Thomson Mwakyusa alisema kuwa, mpaka kufikia tarehe 29 Septemba, 2025 Gereza hilo lilikuwa na jumla ya wafungwa na mahabusu 90 ambapo wafungwa ni 74 wanaume wakiwa 72 na wanawake wawili na mahabusu ni 16 pekee.

“Gereza hili lina uwezo wa kubeba wafungwa na mahabusu 160, kwa takwimu hizo za wafungwa na mahabusu nilizotoa, nikiri mbele kuwa Gereza letu linamudu kuwahudumia wananchi hawa kipekee niwapongeze kwa kasi ya umalizaji mashauri pamoja na kuwa na utaratibu mzuri wa dhamana uliowekwa kupitia maelekezo ya Mhe Jaji Mkuu mambo haya ndio yametusaidia kupunguza mlundikano wa mahabusu katika gereza letu hakika mnastahili pongezi,” alisema Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Mwakyusa.

Aidha, Mkuu huyo wa Gereza alimuomba Jaji Mfawidhi kufikisha salamu za pongezi kwa Jaji Mkuu kwani kwa kipindi kifupi tangu ameteuliwa wameanza kuona kasi yake na ya wasaidizi wake katika kumaliza changamoto zilizokuwa zinawakabili kubwa likiwa ni mlundikano wa mahabusu.

Kadhalika, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Mwakyusa alimshukuru Jaji Mfawidhi wa Kanda ya Moshi pamoja na Viongozi alioambatana nao kwa kufanya ukaguzi katika Gereza hilo na kusema kuwa, hiyo ni ishara ya wazi ya kwamba wako pamoja katika kuwahudumia wananchi.

Mara baada ya ukaribisho huo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt Lillian Mongella alipata fursa ya kuzungumza na Wafungwa na Mahabusu wa Wilaya ya Same na kuwaeleza lengo la ugeni wao pamoja na msafara wote wa alioambatana nao.

“Ndugu zangu kwanza niwape pole kwa haya yote mnayoyapitia pia niwatie moyo kwa kuwa yote haya ni sehemu ya mapito ya maisha yetu sisi wanadamu niwajuze tu tuko pamoja nanyi kwa wakati wote ndio maana leo tumeona ni vema kufika mbele yenu tukiambatana safu nzima ya wahusika katika mnyororo wa utoaji haki jinai ili tuweze kuwajulia hali, kuona mazingira yenu huku pamoja na kujadiliana endapo kuna kikwazo chochote katika majukumu yetu niwaombe tuambizane mambo yote tunayoyaona kama kikwazo kwenu katika zoezi zima la upatikanaji haki niwaahidi yote yatakayosemwa hapa tunakwenda kuyatatua mimi pamoja na timu yangu,” alisema Mhe. Dkt. Mongella.

Akizungumza kwa niaba ya Wafungwa na Mahabusu wa Gereza la Wilaya Same mmoja wa Wafungwa alisema, “binafsi niwapongeze Mahakama kwani kwa sasa hakuna ucheleweshaji wa nakala za hukumu, hakuna kupelekwa mahabusu kwa makosa madogo madogo na kujazana magerezani pasipo sababu hatua hii mliochukua kiukweli ni utunzaji wa haki za kibinadamu, sisi wafungwa wa Same hatuna lalamiko la kucheleweshewa nakala zetu hivyo tumeweza kukata rufaa zetu tunasubiria haki itendeke asanteni kwa kututembelea.”

Katika ziara ya ukaguzi Gereza la Wilaya ya Same Jaji Mfawidhi aliambatana na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi, Mhe. Sekela Mwaiseje, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi, Bi Maria Itala, Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mhe Chrisanta Chitanda, Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo zilizoko Wilaya ya Same, Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Same pamoja na Waendesha Mashtaka wa Wilaya hiyo.

Katika hatua nyingine, naye Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi, Mhe. Adrian Kilimi aliongoza ukaguzi katika Gereza la Wilaya Rombo tarehe 01 Oktoba, 2025 ambapo walitembelea na kukagua Gereza hilo pamoja na kusomewa na kupokea risala ya Wafungwa na Mahabusu iliyobainisha kuridhishwa kwao kwa utendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi.

Akisoma Risala ya Wafungwa na Mahabusu wa Gereza la Wilaya Rombo, Mwakili wa Wafungwa alibainisha juu ya uwepo wa Wafungwa na Mahabusu 116 kwenye Gereza hilo na kwamba lina uwezo wa kubeba Wafungwa na Mahabusu 270.

Aidha, Mfungwa huyo alilalamikia juu ya tabia ya kubambikiwa kesi iliyoshamiri katika Wilaya ya Rombo ambapo alisema,  “Mhe Jaji tunashukuru kwa ujio wako, kiukweli kwa upande wa Mahakama hatuna lalamiko lolote dhidi yenu kilio chetu ni kwa Polisi wanatubambikia kesi ambazo hatujatenda na kuweka mashahidi wa uwongo nitawasilisha orodha ya wanaolalamikia kitendo hicho, tunawashukuru Mahakama kwa kuboresha huduma zenu hatudai nakala ya hukumu wala hatubabaishwi kwa namna yoyote tunapofika mahakamani,” alisema Mfungwa huyo.

Kwa upande wake Mkuu wa Gereza la Wilaya Rombo, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Omary Gunda alibainisha changamoto zinazokabili Gereza hilo kwa sasa ni changamoto ya mtandao kwa eneo hilo.

“Tunashukuru Mahakama imetupatia TV ya kisasa kwa ajili ya kesi za mtandaoni ila tunashindwa kuitumia ipasavyo kwa kuwa tu hatuna mkongo wa taifa katika eneo letu, vilevile naleta kwako ombi la kupatiwa kontena maalum kwa ajili ya matumizi ya chumba cha kusikilizia kesi kwa njia ya mtandao kama ambavyo mmefanya kwa Gereza Kuu la Karanga naamini na sisi Rombo mtatuboreshea kwa namna hiyo,” alisema SSP Gunda.

Akihitimisha kwa kujibu hoja mbalimbali pamoja na kuazimia mambo yaliojadiliwa katika ukaguzi huo, Mhe. Kilimi alisema, “ndugu zangu kwanza nishukuru kwa mapokezi na ushirikiano mliouonyesha, pili niahidi yote tuliojadili tunayakwenda kuyafanyia kazi lakini pia yote tulioazimia hapa kwa pamoja naamini tumeridhika.”

Aidha Jaji Kilimi aliwapongeza kwa mazingira safi ya Gereza hilo na kusema kuwa, hiyo ni ishara ya wazi kuwa wanarekebika na kuwaahidi kuwa Mahakama itafanyia kazi maombi yote yaliyowasilishwa na Wafungwa na Mahakama hao na kupata majibu haraka iwezekenavyo.

Katika ziara hiyo Jaji Kilimi aliambatana na Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt Casian Mshomba, Kaimu Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Rombo, Mhe. Innocent Nyella, Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo zilizoko Wilaya ya Rombo, Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Rombo pamoja na Waendesha Mashtaka Wilaya ya Rombo.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe Dkt. Lillian Mongella  akisaini katika kitabu cha wageni alipowasili hivi karibuni katika Gereza la Wilaya Same kwa ajili ya ukaguzi.


Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Same, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Ipyana Thomson Mwakyusa (aliyesimama) akisoma taarifa ya Gereza la Wilaya Same mbele ya Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe Dkt. Lillian Mongella mara baada ya kuwasili gerezani hapo kwa ajili ya kufanya ukaguzi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe Dkt. Lillian Mongella (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya  watumishi wa Mahakama Kuu na wadau wa Mahakama walioshiriki katika zoezi la ukaguzi wa Gereza la Wilaya Same uliofanyika hivi karibuni.


Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi, Mhe.Adrian Kilimi  akisaini katika kitabu cha wageni alipowasili katika Gereza la Wilaya ya Rombo  hivi karibuni kwa ajili ya ukaguzi.


Mkuu wa Gereza la Wilaya Rombo, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Omary Gunda (aliyesimama) akisoma taarifa ya Gereza hilo mbele ya Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Adrian Kilimi mara baada ya kuwasili gerezani hapo hivi karibuni kwa ajili kufanya ukaguzi.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Adrian Kilimi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya  watumishi wa Mahakama Kuu na wadau wa Mahakama walioshiriki katika zoezi la ukaguzi wa Gereza la Wilaya Rombo uliofanyika hivi karibuni.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni