Jumatano, 1 Oktoba 2025

MAJAJI, MAHAKIMU WAJENGEWA UWEZO KUKABILIANA NA UHALIFU UNAOVUKA MIPAKA

Na YUSUFU AHMADI-IJA, Dar es Salaam

Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Italia (Sant’Anna School of Advanced Studies -Scuola) kimeanza kutoa mafunzo ya siku tatu kwa Majaji, Mahakimu wa ngazi mbalimbali na Waendesha Mashtaka wa Tanzania kuhusu ushirikiano wa kimataifa katika kukabiliana na makosa ya jinai yanayovuka mipaka.

Mafunzo hayo yanayofadhiliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ya Italia yalifunguliwa tarehe 29 Septemba, 2025 na Balozi wa Italia nchini Tanzania, Mhe. Giuseppe Sean Coppola na yanafanyika Mahakama Kuu – Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke mkoani Dar es Salaam. Wawezeshaji wa mafunzo hayo ni Majaji kutoka Tanzania pamoja na Wahadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Italia.

Lengo la mafunzo hayo ni kuimarisha uelewa na uwezo wa Maofisa hao katika kushughulikia makosa hayo ya jinai hususani maeneo ya ushirikiano wa kimahakama juu ya urejeshaji wa watuhumiwa  na kusaidiana kisheria kati ya nchi mbalimbali.

Katika neno lake la utangulizi, Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa amebainisha kuwa umuhimu wa mafunzo hayo ni kuimarisha mifumo ya ushirikiano wa kimataifa katika kushughulikia upelelezi na uendeshaji wa mashauri ya uharifu yanayovuka mipaka.

“Mafunzo haya yatawapatia washiriki kuhusu namna nchi na vyombo vyao, zinaweza kushirikiana katika kushughulikia uhalifu wa kuvuka mipaka unaoharibu amani ya dunia, usalama, uchumi na maendeleo ya jamii,” amesema.

Katika hotuba yake ya ufunguzi,  Balozi  Coppola alisema kuwa kupitia mafunzo hayo washiriki wa Tanzania na Italia watatoka na uelewa wa pamoja katika kushughulia uhalifu huo, akibainisha kuwa nchi yake ni miongoni wa waathirika wakubwa.

“Mtandao wa uhalifu unaouvuka mipaka ni tatizo kubwa duniani na umekuwa na athari kubwa kwa jamii, hivyo tunahitaji kuimarisha ushirikiano kati ya Majaji, Mahakimu na Waendesha Mashtaka wa Tanzania na Italia, ili tuwe na uelewa mmoja wa jinsi ya kukabiliana na mtandao huo,” amesema Balozi Coppola.

Pia ameishukuru Serikali ya Tanzania na Uongozi wa IJA kwa kushirikiana pamoja katika kufanikisha mafunzo hayo.

Ufunguzi huo umehudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Mradi wa Utawala wa Sheria na Ushirikiano wa Mahakama ambaye pia ni  Profesa Msaizidi wa Scuola Lorenzo Gasbarri pamoja na viongozi wengine.

 Changamoto za uhalifu wa kuvuka mipaka

Kwa mujibu wa takwimu, makosa ya usafirishaji haramu wa binadamu, dawa za kulevya, utakatishaji wa fedha, ugaidi, biashara haramu ya silaha na ujangili, na uhalifu mitandaoni yameongeza kutokana na maendeleo ya teknolojia na uhuru wa watu kuvuka mipaka..

Hivyo kupitia mafunzo hayo na ukubwa wa changamoto hiyo, IJA pamoja na Scuola ambacho ni miongoni mwa Vyuo Vikuu vya Umma vyenye kuheshimika nchini Italia, vinakuwa sehemu ya kuunga mkono sera na mikakati ya Serikali na Jumuiya za Kimataifa katika mapambaop dhidi ya uhalifu wa kimataifa kwa kuimarisha mifumo ya haki jinai.

Balozi wa Italia nchini Tanzania Giuseppe Sean Coppola akizungumza wakati anafungua mafunzo ya siku tatu kwa Majaji, Mahakimu wa ngazi mbalimbali na Waendesha Mashtaka wa Tanzania kuhusu ushirikiano wa kimataifa katika kukabiliana na makosa ya jinai yanayovuka mipaka.

Balozi wa Italia nchini Tanzania Giuseppe Sean Coppola (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo. Kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, MheMwanabaraka Mnyukwa na kulia ni Mkurugenzi wa Mradi wa Utawala wa Sheria na Ushirikiano wa Mahakama ambaye pia ni Profesa Msaizidi wa Scuola, Lorenzo Gasbarri.

Mkurugenzi wa Mradi wa Utawala wa Sheria na Ushirikiano wa Mahakama ambaye pia ni  Profesa Msaizidi wa Scuola Lorenzo Gasbarri akizungumza katika mafunzo hayo.

Balozi wa Italia nchini Tanzania Giuseppe Sean Coppola (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Wasajili, Mahakimu  wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo.

Sehemu ya washiriki wakiwa katika mafunzo hayo [juu na chini].



 Picha ya pamoja.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma







 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni