- Awataka Wahitimu hao kuleta tija kwa jamii kupitia elimu waliyopata
- Awasisitiza kujibidiisha kuendana na mabadiliko ya Ki-TEHAMA
- Awatahadharisha juu ya matumizi ya Akili Unde kwamba itumike kwa uangalifu, kusaidia fikra, kujifunza na siyo kuchukua nafasi ya matumizi ya akili zao
- Akitaka Chuo kuhakikisha kuwa, elimu wanayopata wanafunzi inakuwa ya vitendo zaidi kuliko nadharia pekee
- Awashauri Wahitimu kila mmoja kwa imani yake kumtanguliza Mungu katika maisha ya kila siku
- Awasihi kutopuuza mchango wa Walimu, Wahadhiri, Wazazi na Walezi katika kila hatua ya maisha yao
Na MARY GWERA,
Mahakama-Lushoto
Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju ametoa rai kwa Wahitimu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kutumia elimu waliyoipata katika Chuo hicho kwa kuisaidia jamii kwa kutenda haki na kuleta mabadiliko chanya popote watakapokuwa.
Akizungumza leo katika Mahafali ya 25 ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto yaliyofanyika katika Ukumbi wa Nyalali uliopo Chuoni hapo, Mhe. Masaju amesema Fani ya Sheria waliyoichagua Wahitimu hao ni fani ya kutenda haki.
“Nawasihi mkawe watenda haki kwani haki huinua Taifa. Na hili nalielekeza si tu kwa wale watakaoajiriwa Mahakamani au kwenye utumishi wa umma bali linamgusa kila mmoja wenu kwani haki ni suala linalogusa kila eneo la maisha ya mwanadamu,” amesisitiza Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju amewataka pia Wahitimu hao kuwa, pamoja na ujuzi wa kitaaluma walioupata Chuoni hapo, Watanzania wanaamini wahitimu hao wamejengwa vilivyo kwenye misingi ya maadili mema.
“Kama ilivyoelezwa katika hotuba zilizotangulia, Chuo
hiki kimejizolea sifa ya kuzalisha wahitimu wenye ujuzi wa hali ya juu
kitaaluma lakini pia kuzalisha wahitimu wenye maadili bora na hivyo kuwa Chuo
cha mfano katika hilo,” amesema Jaji Mkuu.
Amewakumbusha Wahitimu
hao kuwa, mafanikio na ubora wao katika Fani ya Sheria waliyoingia yatategemea kuyashika na kuyatumia maarifa
mliyoyapata Chuoni hapo lakini zaidi kujitofautisha na wengine kwa kuwa na
maadili mema ambayo pia wamefundishwa vizuri katika Chuo hicho.
Mhe. Masaju amewaeleza Wahitimu hao kwamba, pamoja na mafunzo ya maadili waliyopata, ni vyema wakazingatia kile anachokiita ‘software’ nane za vitendea kazi muhimu vitakavyowaongoza katika kazi, masomo na maisha yao ya kila siku ambavyo ni Uadilifu (Integrity), Uwezo wa kutekeleza majukumu (Competency), Kuwiwa kuona haki inatendeka (Sensitivity to justice), Uwajibikaji (Accountability).
Ameongeza kuwa, vitendea kazi vingine ni Ubunifu (Creativity), Uchukuaji hatua kwa mapema ( Proactivity), Uzalendo wa Kitaifa (National Patriotism) na Uhalisia/ukweli usioegemea upande wowote (Objectivity).
“Tukiachia vitendea kazi tulivyozoea
kama vile kompyuta, karatasi, kalamu nk., zipo software nane za vitendea kazi
zitakazowaongoza katika majukumu yenu. Naziita “software” kwa sababu hizi ni
kama mfumo wa ndani (internal operating system) unaoongoza
namna mtu anavyofikiri, kufanya maamuzi, na kutenda kila siku kama ilivyo kwa
kompyuta. Endapo mtavitumia ipasavyo, mtakuwa mfano wa kuigwa katika jamii,”
amesisitiza.
Kadhalika, Jaji Mkuu amewausia wahitimu hao ni
kujibidiisha ili kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia yanayoendelea kwa kasi katika
zama hizi za Mapinduzi ya Nne ya Viwanda.
“Katika zama hizi, njia za kiasili za utendaji wa
shughuli mbalimbali, ikijumuisha shughuli za Serikali na binafsi, zimechukuliwa
na njia za kielektroniki za utekelezaji wa shughuli hizo, hususani Teknolojia
ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), ni imani yangu kwamba mmefundishwa masomo
yahusuyo matumizi ya TEHAMA kwa upana wake. Ninawasihi sana elimu hiyo isiishie
hapa Chuoni tu kwa kufaulu masomo yenu pekee, bali mjibidiishe kujielimisha
zaidi kwenye eneo hilo na muwe tayari kutumia maarifa na ujuzi mlionao kwenye
majukumu yenu yajayo kwani huko ndiko Taifa na Dunia nzima inakoelekea kwa sasa
kama si imeshafikia,” ameeleza.
Hata hivyo, Mhe. Masaju amewatahadharisha wahitimu hao
kuwa waangalifu katika matumizi ya Akili Unde, ambapo amesema, “Ninajua kwamba
baadhi yenu mmewahi kutumia au mnatumia programu za Akili Mnemba (Artificial
Intelligence) katika masomo yenu au kazi zenu. Akili Mnemba ni sehemu ya
matumizi ya TEHAMA lakini mnapaswa kutumia teknolojia hii kwa uangalifu mkubwa
mno kwani inaweza kudumaza uwezo wenu wa kufikiria na kuchambua mambo.”
Amesema, Akili Unde ina manufaa ikitumika vizuri
kusaidia njia za asili za kujifunza na kutafakari na siyo kuondoa njia hizo za
asili na badala yake kutegemea Akili Unde kupita kiasi ambayo itadumaza ukuaji
wa maarifa na ujuzi wa mtumiaji.
Hali kadhalika, Jaji Mkuu amewatahadharisha Wahitimu
hao kuhusu matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii hasa katika ulimwengu huu wa
utandawazi.
“Wengi wetu ni mashuhuda kwa siku za hivi karibuni
kumekuwa na matumizi yasiyo sahihi ya mitandao ya kijamii ambayo yamesababisha
vijana wengi kuiga au kupata ushawishi wa watu kutoka nje ya nchi na matokeo
yake ni kwamba wahanga wakubwa wa matumizi hayo mabaya ya mtandao ya kijamii
wamekuwa ni vijana. Hivyo ninawasihi sana wahitimu mtumie TEHAMA na mitandao ya
kijamii kwa masuala yenye tija kwenu na kwa Taifa kwa ujumla,” amesisitiza.
Aidha, Jaji Mkuu amekitaka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kuwa sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambapo amesema, “Itakumbukwa kwamba mwaka huu Tanzania imezindua Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050, wote tunafahamu kwamba ni muhimu kwa kila Taasisi ya Umma kupanga mipango yake na kuelekeza utendaji wake kwenye kufikia malengo ya Dira hiyo. Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.”
Mhe. Masaju ameeleza
kuwa, Dira hiyo ina Nguzo Tatu, Nguzo ya pili inahusu Uwezo wa Watu Na
Maendeleo a Jamii ambapo moja ya maeneo ya kipaumbele katika nguzo hii ni ‘Jamii
iliyoelimika, yenye Ujuzi na Inayopenda Kujifunza’ amesema, “kipaumbele hiki
kimejikita kwenye umuhimu wa kuendelea kuimarisha miundombinu ya kujifunzia na
kufundishia sambamba na ongezeko la idadi ya wanafunzi katika Taasisi za Elimu.”
Ameongeza kwamba,
Dira hiyo inaelekeza kuwa ni muhimu kuendelea kuboresha mfumo wa elimu na
mafunzo nchini ili kuendana na mabadiliko ya wakati ili kuwaandaa wahitimu
kukabiliana na ushindani katika dunia inayobadilika kwa kasi, hivyo Chuo
kinapaswa kuzingatia kikamilifu maelekezo hayo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo
ili kuwezesha Taifa kufikia malengo ya Dira hiyo ifikapo mwaka 2050.
Akizungumzia kuhusu uanzishaji wa Programu mpya chuoni, Jaji Mkuu amesisitiza kwamba, wakati Chuo hicho kinaendelea kutekeleza mkakati huo wazingatie pia malengo ya uanzishwaji wa Chuo hicho ili wasitoke nje ya malengo hayo bali wazidi kuyatekeleza kwa upana zaidi na kwa kuwafikia walengwa wengi zaidi kwakuwa Mahakama ya Tanzania na Wadau wa Sekta ya Sheria wana imani kubwa na Chuo hicho na wanakitegemea kama chombo cha kuendesha mafunzo yatakayoboresha utendaji kazi wa Mahakama na mfumo mzima wa utoaji haki nchini.
Katika hatua
nyingine, Mhe. Masaju amekiri kuwa, Mahakama ya Tanzania inajivunia utekelezaji
wa majukumu ya chuo hicho na kusema kuwa, “Nimefurahi kusikia kuwa Chuo
kimeendelea kufanya vizuri katika kutekeleza
majukumu ambayo kimepewa
na Sheria iliyokianzisha. Nawapongeza sana kwa hilo, Mahakama ya Tanzania inatambua
nafasi muhimu na ya kipekee ya Chuo hiki ambayo imebainishwa vema kwenye Sera
ya Mafunzo ya Mahakama ya mwaka 2019 kuwa ni chombo cha kutoa mafunzo na
kufanya tafiti kuhusu mafunzo ya kujengea uwezo watumishi wa Mahakama.
Jaji Mkuu amesema, Mahakama ya Tanzania itaendelea
kutoa ushirikiano wa kutosha kama
ambavyo imekuwa ikifanya siku zote na itajitahidi kutatua kero na changamoto
mbalimbali za Chuo ili kukiwezesha Chuo kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi
kwani ufanisi wa Chuo ndiyo ufanisi wa Mahakama ya Tanzania.
Hata hivyo, Mhe.
Masaju amesisitiza kwamba, Chuo kisijikite tu katika kutoa mafunzo kwa Majaji,
Mahakimu au Wanasheria pekee, bali kitoe mafunzo kwa Kada zote za watumishi wa
Mahakama. Hiyo ni
kwa sababu huduma bora kwa mwananchi hutokana na mchango wa kila kada, kuanzia Walinzi,
Wasaidizi wa Ofisi, Waandishi Waendesha Ofisi, Maafisa TEHAMA, Wahasibu, Madereva
na wengine.
Sambamba na kutoa
mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi wa Mahakama, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, ni wakati
sasa Chuo kuhakikisha kuwa, elimu
wanayopata wanafunzi inakuwa ya vitendo zaidi kuliko nadharia pekee.
“Katika kutekeleza mpango huo wa
kuwapatia wanafunzi elimu ya vitendo, nawahimiza kutumia rasilimali zilizopo
karibu na Chuo. Chuo kiendelee kuandaa utaratibu wa kuwapeleka wanafunzi
kufanya mafunzo ya vitendo katika Mahakama ya Wilaya ya Lushoto na Mahakama ya
Mwanzo Dochi, ambazo ziko karibu na Chuo, ili kupata fursa ya kujifunza moja
kwa moja kuhusu uendeshaji wa shughuli za kimahakama,” amesema Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju amesema kuwa, anatambua
changamoto zilizopo kwa sasa katika Mahakama hizo ambapo Jengo la Mahakama ya
Wilaya ya Lushoto lina ofisi mbili tu za Mahakimu na ukumbi mmoja wenye uwezo
wa kuchukua watu 30 pekee. Vivyo hivyo, Mahakama ya Mwanzo Dochi ina ofisi
mbili na ukumbi mmoja wenye uwezo wa kuchukua watu wasiozidi 50. Miundombinu hii,
kwa hali ilivyo, haina uwezo wa kuhimili idadi kubwa ya wanafunzi wa IJA, ambao
hufikia takribani 800 kwa mwaka.
“Hivyo basi, napenda kusisitiza
umuhimu wa kuharakisha ujenzi wa jengo jipya la Mahakama ya Wilaya ya Lushoto.
Nimejulishwa kuwa mkandarasi tayari amesaini mkataba na ujenzi unatarajiwa
kuanza mwezi Desemba mwaka huu. Hapa nisisitize ujenzi wa kumbi za Mahakama
uzingatie uhitaji mkubwa wa wanafunzi wa Chuo hiki kufanya mafuzo kwa vitendo, Jengo
hilo litakapokamilika, litaongeza kwa kiasi kikubwa uwezo wa kuwahudumia
wanafunzi wanaofanya mafunzo kwa vitendo na hivyo kuboresha zaidi ubora wa
mafunzo hayo,” amesisitiza.
Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Mhimili wa Mahakama,
amewashauri Wahitimu hao kumtanguliza Mwenyezi Mungu katika maisha yao ya kila
siku kwani ndiye atakayewafungulia milango ya neema na mafanikio na pia
kuwaongoza pale wanapokutana na changamoto mbalimbali za kimaisha au kitaaluma.
“Ninawaomba muwe watu wa ibada na kushika neno la
Mungu kwani hilo litawasaidia kuwa na maarifa zaidi na maadili mema na hivyo
kupata mafanikio katika kazi zenu au katika masomo ya elimu ya juu. Maandiko Matakatifu
ya Biblia na Quran yamezungumzia umuhimu wa kumcha Mungu katika maisha yetu ya
kila siku. Biblia Takatifu katika kitabu cha
Mithali 1:7 inasema: “Kumcha Bwana ni chanzo cha maarifa, bali wapumbavu
hudharau hekima na adabu,” ameeleza Mhe. Masaju.
Ameongeza huku akirejea Kitabu cha Quran Tukufu katika
Sura ya 65 Aya ya 3 inasema:“Na anayemcha
Mwenyezi Mungu, Humtengenezea njia ya kuokoka na Humpa riziki kwa mahali
asipotazamia.” Amesema Aya hizo za Vitabu Vitakatifu
zinaonyesha umuhimu wa kumcha Mwenyezi Mungu katika maisha ya mwanadamu.
Katika Mahafali hayo jumla ya wahitimu wa 286 wa Astashahada ya Msingi ya Sheria wametunukiwa vyeti, Wahitimu 241 wa Astashahada ya Sheria pamoja na Wahitimu 286 wa Stashahada ya Sheria wametunukiwa vyeti.
Aidha,
Jaji Mkuu amewatunuku zawadi za fedha na vyeti wanachuo bora
wanne kitaaluma kwa mwaka wa masomo 2024/2025 ambapo kwa upande wa Astashahada
ya Msingi ya Sheria ni Bw. Jofrey Mtimbuka (1) na Bw. Gidion Nyamhanga (2).
Kwa
upande wa Stashahada ya Sheria, wa kwanza ni Bw. Justine Sundi na wa pili ni
Bw. Boniface Malobo huku Bw. Wenselaus Zacharia akitunukiwa zawadi ya Jaji Mkuu fedha taslimu kiasi cha Tshs. 1,000,000/= kwa kupata wastani wa daraja ‘A’ katika masomo ya mwenendo wa mashauri ya madai
na jinai.
Wageni mbalimbali wamehudhuria mahafali hayo wakiwemo Majaji wa Rufani, Majaji Wafawidhi Tanga na Moshi, Mtendaji Mahakama Kuu Tanga, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Tanga na wengine kutoka Taasisi mbalimbali za Serikali, Taasisi binafsi, Viongozi wa Serikali za Mitaa pamoja na Viongozi wa Dini.
Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wahitimu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) katika Mahafali ya 25 ya Chuo hicho yaliyofanyika leo tarehe 28 Novemba, 2025 chuoni hapo.
Makundi mbalimbali ya Wahitimu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) wakisikiliza kwa makini hotuba ya Mgeni Rasmi Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 28 Novemba, 2025 wakati wa Mahafali ya 25 ya Chuo hicho.

Maandamano kuelekea ukumbi wa Nyalali tayari kwa ajili ya kusherehekea Mahafali ya 25 ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) leo tarehe 25 Novemba, 2025.
Sehemu ya Wahadhiri wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) wakiwa katika Mahafali ya 25 ya Chuo hicho leo tarehe 28 Novemba, 2025.













Hakuna maoni:
Chapisha Maoni