Jumatatu, 17 Novemba 2025

JIKITENI KATIKA KULETA MATOKEO YENYE TIJA- MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA


  • Mahakama ya Tanzania haitavumilia vitendo vya uvivu, uzembe, ubadhirifu, nidhamu mbovu

·        Mjiendeleze dunia inabadilika kwa kasi sana

Na. HABIBA MBARUKU – Mahakama, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel amewasisitiza Waajiriwa Wapya wa Mahakama katika kada mbalimbali kujituma katika kuleta matokeo yenye tija na kuweka wazi kuwa Mahakama ya Tanzania haitavumilii matukio ya uzembe, uvivu, ubadhirifu na nidhamu mbovu kwa watumishi wote wa Mahakama.

Prof. Ole Gabriel ameyasema hayo alipokua akifungua Mafunzo Elekezi kwa Watumishi Wapya wa Mahakama wa Kada Mbalimbali, yaliyofanyika leo tarehe 17 Novemba, 2025 katika ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa hotuba yake Prof. Ole Gabriel amewataka waajiriwa hao kujituma na kujiendeleza kielimu huku wakizingatia mabadiliko ya kasi ya dunia, huku akiwasisitiza na kuwashauri kujiendeleza katika kada tofauti na walizo nazo sasa.

“Ningeomba pia mjikite katika matokeo yenye tija, Mahakama hatuna uvumilivu na watu wavivu, wazembe, ubadhilifu na nidhamu mbovu , hayo manne hatuna huruma nayo, naomba sana mnapojitunza muhakikishe kwamba mnajiweka vizuri  katika hilo lakini pia mjiendeleze kwa sababu dunia inabadilika kwa kasi kubwa sana kama umeingia hapa na Diploma au Degree ya kwanza songa mbele jitahidi kujiendeleza zaidi na mimi nawashauri mfikiri suala linaloitwa Diagonal Career Development, siyo lazima uende vertical unaweza ukaongeza vitu vingine itakupa tija zaidi,” ameongeza Mtendaji Mkuu.

Akizungumza kuhusu matumizi ya TEHAMA Prof. Ole Gabriel amesema kuwa, Mahakama kwa sasa ni miongoni mwa Taasisi ambazo zimepiga hatua kubwa katika matumizi ya TEHAMA akiweza wazi mabadiliko makubwa ya matumizi ya TEHAMA katika Mahakama nchini na kuwataka waajiriwa wapya kujiendeleza kwa nguvu kubwa ili kuwa mahiri katika matumizi ya TEHAMA.

“Mahakama kwa sasa ni moja ya Taasisi ambazo zimepiga hatua kubwa sana kwenye matumizi ya TEHAMA, miaka ile tumezoea makaratasi yanatumika na vitu kama hivyo lakini kwa sasa Mahakama imejitanabaisha na ndio Taasisi ya kwanza nchini kwa matumizi ya TEHAMA nawaomba sana mjitahidi sana sana kujiendeleza kadri iwezekanayo, kuwa mahiri katika matumizi ya TEHAMA,” amesema Prof. Ole Gabriel.

Ameongeza kuwa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania inatoa fursa ya ajira ili kuongeza kasi ya utendaji wa watumishi kuwatumikia wananchi zaidi ya milioni 60 ambao wanategemea huduma ya Mahakama, na huku akieleza kuwa Mahakama ni chombo cha juu kabisa katika utoaji wa haki kama inavyoelezwa katika Ibara ya 107 A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan inatupa fursa ya ajira ili tuweze kuongeza utendaji wetu kwa kuwatumikia wananchi zaidi ya milioni 60 ya watanzania wanaotegemea Mahakama iwahudumie…

Mkumbuke pia kwamba, Mahakama ndiyo chombo cha juu kabisa katika utoaji wa haki Ibara ya 107 A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inafafanua. Usije Mahakama kwa kudai umekuja kutunza kumbukumbu, unapoingia Mahakama mara zote jifikirie kwamba na wewe unasaidia uendeshaji wa mashauri kwa ajili ya haki kupatikana hilo ndilo jukumu letu kubwa,” amesisitiza Prof. Ole Gabriel.

Aidha, Prof. Ole Gabriel amesisitiza mambo saba muhimu katika utendaji kazi huku akigusia kuhusu suala la umahiri katika kujifunza kasi ya teknolojia, kujifunza kuishi na watu wengine akiwataka mara zote kujiuliza kuhusu michango wanayotoa katika sehemu ambayo wapo, amewakumbusha kuhusu suala la kutunza muda kwa sababu mafanikio yoyote yale yanatokana na utunzaji wa muda

Vilevile, Prof. Ole Gabriel amewataka waajiriwa hao wapya kujiuliza kuwa wataifanyia nini Mahakama ya Tanzania na siyo Mahakama ya Tanzania itawafanyia nini, huku akiwataka kuwa tayari kufanya kazi mahali popote ndani na nje ya Tanzania akisema kuwa lipo tatizo la watu kupinga sehemu za kazi walizopangiwa.

Sambamba na hayo, Prof. Ole Gabriel ametoa tahadhari katika matumizi ya TEHAMA hasa katika matumizi ya mitandao ya kijamii akiwataka watumishi wapya kuwa makini wanapotumia mitandao ya kijamii, lakini pia wakizingatia namna ya uzungumzaji, uchapishaji wa maudhui mtandaoni, na uvaaji wa mavazi yenye maadili.

Ameongeza kuwa watumishi wapya wanapaswa kujali Itifaki, akieleza kuwa Itifaki ni kuhakikisha kuwa unafuata na kutekeleza utaratibu wa mila na desturi ya mahali husika, aidha amewasisitiza waajiriwa wapya kulipa kipaumbele suala la kuandaa mazingira mazuri baada ya kustaafu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick amesema kuwa mafunzo hayo yatakayodumu kuanzia tarehe 17 Novemba hadi tarehe 03 Disemba 2025, yatatoa fursa kwa waajiriwa wapya 474 kujifunza kuhusu Muundo wa Mahakama, sheria za utumishi wa umma, kanuni taratibu na miongozo iliyopo katika utumishi wa umma.

 Aidha, kujua utamaduni wa Mahakama ya Tanzania, historia ya Mahakama, Mpango Mkakati wa Mahakama, Dira ya Maendeleo ya Taifa 20250, majukumu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama, kuwaandaa waajiriwa wapya kiuwekezaji baada ya kustaafu, vilevile, mafunzo kwa ajili ya kutoa msongo wa Mawazo, jinsia, uzalendo, itifaki, mfumo wa kupima utendaji, utunzaji wa taarifa mbalimbali na maelekezo maalumu ya mifumo ya TEHAMA inayotumika na Mahakama kutoa huduma kwa wananchi.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel amewasisitiza Waajiriwa Wapya wa Mahakama katika kada mbalimbali kujituma katika kuleta matokeo yenye tija alipokuwa akifungua Mafunzo Elekezi ya siku tano kwa kada ya wasaidizi wa kumbukumbu wa Mahakama nchini.

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Beatrice Patrick akitoa ufafanuzi wa namna ya kushiriki mafunzo hayo elekezi kwa kada ya wasaidizi wa kumbukumbu 

Sehemu ya Waajiriwa Wapya wa Mahakama kwa kada ya wasaidizi wa kumbukumbu wakiwa ukumbini wakimsikiliza Mgeni rasmi aliyefungua mafunzo elekezi Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel. 



Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania 
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Waajiliwa wapya wa kada ya wasaidizi wa kumbukumbu wanaoshiriki mafunzo hayo elekezi Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Waajiliwa wapya wa kada ya wasaidizi wa kumbukumbu wanaoshiriki mafunzo hayo elekezi Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya Waajiliwa wapya wa kada ya wasaidizi wa kumbukumbu wanaoshiriki mafunzo hayo elekezi Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya sekretarieti ya mafunzo hayo.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa kwenye picha ya pamoja na waajiriwa wapya mbele ya Jengo la Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama) 

Habari Hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni