Jumatatu, 17 Novemba 2025

MSAJILI MKUU AFANYA ZIARA YA KIKAZI MKOANI MWANZA

Na. REHEMA AWET –Mahakama, Mwanza

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, amefanya ziara ya kikazi mkoani Mwanza kwa lengo la kukagua maendeleo ya miradi ya ujenzi wa miundombinu ya Mahakama na kusisitiza matumizi ya mifumo ya kidijitali kuwa sehemu ya miundombinu hiyo katika utoaji wa huduma za kimahakama.

Katika ziara hiyo, Mhe Nkya ametembelea na kukagua jengo linalokarabatiwa litakalotumika kama Mahakama Kuu–Kitengo cha Familia (Family Court), ambapo ameelezea kuridhishwa kwake na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa ukarabati huo.

Mhe. Nkya amesema uanzishwaji wa kitengo hicho utarahisisha upatikanaji wa huduma za kimahakama kwa wananchi wanaohusiana na mashauri ya kifamilia, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Mahakama ya Tanzania kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.

Aidha, Msajili Mkuu ametembelea Mahakama ya Wilaya ya Nyamagana, ambako amekutana na watumishi wa mahakama hiyo na kusisitiza umuhimu wa kutumia Mfumo wa Usimamizi wa Mashauri kwa njia ya Kielektroniki (eCMS) ili kuongeza uwazi, ufanisi na kasi katika utoaji wa haki.

Mhe. Nkya pia ametembelea Mahakama ya Mwanzo Kisesa, iliyopata uharibifu baada ya kuchomwa moto kufuatia vurugu zilizotokea baada ya uchaguzi Mkuu. Akiwa katika eneo hilo, ameelezea dhamira ya Mahakama kuhakikisha huduma zinarejea haraka kwa wananchi huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wadau wote katika kulinda mali na miundombinu ya Mahakama.

Ziara hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa Mahakama ya Tanzania wa kuimarisha miundombinu, kuendeleza matumizi ya teknolojia, na kuhakikisha utoaji wa haki unafanyika kwa wakati, kwa uwazi na kwa gharama nafuu.

Msimamizi wa Mradi Mha. Daniel (kwanza kulia) akitoa taarifa ya Maendeleo ya mradi kwa Msajili Mkuu wa Mahakama Mhe. Eva Nkya(pili kulia). Wengine katika picha ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza Mhe. Crisencia Kisongo(tatu kulia), Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Nyamagana Mhe. Ramla Shehagilo(kwanza kushoto)

Msajili Mkuu wa Mahakama, Mhe. Eva Nkya (Pili kulia) akitoa ushauri kuhusu maboresho yanayofanyika katika ukarabati wa Mahakama Kuu kitengo cha familia. Wengine katika picha ni Mhandisi msimamizi wa mradi Bw. Daniel (kwanza kulia), Katibu wa Msajili Kuu wa Mahakama Mhe Jovin Bishanga (tatu kulia) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza Mhe. CrIsencia Kisongo.

Muonekano wa Jengo la Mahakama kuu Kanda ya Mwanza kitengo cha familia linalofanyiwa ukarabati.

Muonekano wa Jengo la Mahakama kuu Kanda ya Mwanza kitengo cha familia linalofanyiwa ukarabati.


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya (wa nne kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Kisesa Wilayani Magu Mkoa wa Mwanza iliyochomwa moto baada ya vurugu za uchaguzi mkuu, alipokuwa kwenye ziara ya kikazi mkoani Mwanza kwa lengo la kukagu miundombinu ya Mahakama, wengine ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza Mhe. Crisencia Kisongo(tano kulia), Katibu wa Msajili Mkuu wa Mahakama Mhe. Dkt.Jovine Bishanga (kwanza kushoto) wakiwa na baadhi ya watumishi wa Mahakama 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni