Jumatatu, 17 Novemba 2025

MAHAKAMA YA WILAYA MBEYA YAWAAGA WASTAAFU

Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya

Mahakama ya Wilaya Mbeya hivi karibuni Novemba, 2025 ilifanya hafla ya kuwaaga watumishi wastaafu wa Mahakama ikiwa ni ishara ya kuwaenzi kwa utumishi wao uliotukuka na kuwapongeza kwa jitihada zao za kulitumikia Taifa kwa kipindi chote cha utumishi wao.

Akizungumza katika hafla hiyo Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Said Kalunde aliipongeza Mahakama ya Wilaya ya Mbeya kwa kuandaa hafla hiyo.

“Niwapongeze sana Mahakama ya Wilaya Mbeya kwa kufanikisha kufanya jambo hili kubwa na muhimu la kuona thamani ya wenzetu tuliokuwa nao katika utumishi kuwaaga kwa pamoja kwa kuwaandalia hafla hii,” alisema Mhe. Kalunde.

Mhe. Kalunde aliongezea kuwa, hafla hiyo ina lengo la kutambua mchango wa watumishi hao wastaafu ambao kwa kipindi chote walikuwa waadilifu na wachapakazi ambao waliitumikia Mahakama, Serikali na Taifa kwa ujumla.

“Ndugu zetu mnaondoka katika utumishi wa Umma tunaomba tuendeleze undugu wetu na upendo wetu, pale mtakapokuwa na shughuli zenu msisite kutualika nasi pia tutaendelea kuwashirikisha kwenye shughuli zetu na tunawaomba mjumuike nasi” aliongezea Mhe. Kalunde

Akitoa neno la shukurani mmoja wa wastaafu hao, Afisa Hesabu Mahakama ya Wilaya Mbeya Bi. Magreth Kasanga alisema mioyo yao ina furaha isiyo kifani kama wastaafu walioutumikia Umma na Taifa kwa ujumla kwa uadilifu na mioyo ya kujituma kwa zaidi ya miaka 30 hadi kufikia hatua hiyo.

“Tunashukuru sana kwa upendo wenu wa dhati mliotuonesha viongozi wetu na watumishi wenzetu tuliokuwa pamoja kwenye majukumu mbalimbali ya kiutumishi, kwa hakika sisi siyo wakamilifu tunaomba radhi kwa yale tuliyowakosea mtusamehe nasi pia kwa umoja wetu kwa mioyo yetu mikunjufu tumewasameheni nyote,” alisema Bi. Magreth Kasanga.

Bi. Kasanga aliongeza kuwa angependa kutoa nasaha fupi kwa watumishi wanaoendelea na utumishi wa Umma, waendelee kuchapa kazi kwa bidii na kuwa wastahmilivu wanapokumbana na changamoto mbalimbali za kazini.

“Ninawasihi watumishi wenzangu ambao mnaendelea na utumishi wa Umma muendelee kuchapa kazi kwa bidii, uaminifu na uadilifu katika kuutumikia Umma wa Watanzania, muwe na uvumilivu, hekima, busara wakati wote muwapo kwenye majukumu yenu, nimalizie kwa kusema ukiona nyani kazeeka kakwepa mishale mingi” aliongezea Bi. Kasanga.

Hafla hiyo iliyoandaliwa na Mahakama ya Wilaya Mbeya ikishirikiana na Mahakama zake za mwanzo, hafla ambayo ilihudhuriwa pia na wawakilishi kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mawakili wa Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, Madalali wa Mahakama pamoja na ndugu na jamaa wa karibu wa waagwa hao.

Watumishi hao walioagwa katika hafla hiyo walikuwa ni Bi. Magreth Kasanga Afisa hesabu Mahakama ya Wilaya Mbeya, Bi. Leah Mwakaguta Msaidizi wa ofisi Mahakama ya Wilaya Mbeya, Bi. Siyoni Kasunga Msaidizi wa kumbukumbu Mahakama ya mwanzo Mwanjelwa, Bi. Eugenia Mataula msaidizi wa ofisi Mahakama ya mwanzo Mbalizi na Bi. Tabu Msaidizi wa Hesabu Mahakama ya Mwanzo Uyole.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Said Kalunde akitoa hotuba ya kuwapongeza watumishi wastaafu wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya wakati wa kuwaaga kwenye hafla hiyo.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Said Kalunde aliyevalia tisheti nyeupe (katikati) akifuatilia shughuli ya hafla ya kuwaaga watumishi wastaafu, wengine ni Jaji wa Mahakama kuu ya kanda ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo(kulia) Jaji wa Mahakama kuu ya kanda ya Mbeya Mhe. Victoria Nongwa (wa pili kulia), Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Mbeya Mhe. Aziza Temu (wa pili kushoto) na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba.



Sehemu ya Watumishi wastaafu ambao walikuwa wanaagwa kwenye hafla hiyo
Sehemu ya Watumishi wastaafu ambao walikuwa wanaagwa kwenye hafla hiyo

Sehemu ya Watumishi wastaafu ambao walitunukiwa vyeti na kuagwa kwenye hafla hiyo
Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Said Kalunde aliyevalia tisheti nyeupe akimtunuku cheti moja ya mtumishi mstaafu wakati wa hafla hiyo.


Sehemu ya Watumishi wastaafu ambao walikuwa wanaagwa kwenye hafla hiyo


Sehemu ya Burudani ikiendelea wakati wa hafla hiyo ya kuwaaga watumishi wastaafu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni