Jumatano, 19 Novemba 2025

KAMATI YA JAJI MKUU INAYOSHUGHULIKA NA MASUALA YA MABORESHO YAFANYA ZIARA MAHAKAMA SIMIYU

  •  Yaridhishwa na hatua za Miradi ya Ujenzi wa Mahakama inayoendelea mkoani humo 

Na NAUMI SHEKILINDI, Mahakama-Simiyu

Kamati ya Jaji Mkuu inayoshughulika na masuala ya maboresho imefanya ziara mkoani Simiyu hivi karibuni yenye lengo la kukagua miradi minne inayoendelea Mkoani humo.

Kamati hiyo iliongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe.Mustapha Ismail ambaye aliongozana na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Deo Nangela, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Mhe. Mariam Mchomba na Naibu Msajili Kitengo cha Maboresho ya Mahakama (JDU), Mhe. Hamza Adam.

Kamati hiyo ilitembelea miradi yote na kujionea maendeleo ya miradi hiyo pamoja na kutoa maoni yao ya nini kifanyike ili kuboresha majengo hayo kuwa ya kisasa zaidi na kuanza kutumika mapema.

Aidha, kamati iliridhishwa na shughuli za ujenzi zinazoendelea na kusisitiza kuwa dosari ndogondogo zinazosababisha jengo lisianze kutumika mapema zirekebishwe kwa uharaka ili majengo yaanze kufanya kazi.

Mhe. Ismail alisisitiza wahusika wa utawala kuangalia motisha za watumishi kwa namna watakavyoona inafaa ili kuendana na hadhi pamoja na  upya wa jengo, lengo likiwa ni kuwaongezea ari ya kazi watumishi wa Mahakama.

Mkoa wa Simiyu una jumla ya miradi minne inayoendelea ikiwa ni Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) ambayo imefikia asilimia 94 kukamilika, Mahakama ya Mwanzo Nyalikungu, Mhango na Lagangabilili ambayo ipo asilimia 100 ya ukamilishwaji.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu Bw. Gasto Kanyairita aliwashukuru kwa ujio wa Kamati hiyo na kuushukuru Uongozi wa Mahakama kwa ujumla kwa kuleta miradi ya ujenzi wa Mahakama Mkoani humo yenye manufaa kwa wananchi wa Simiyu pamoja na watumishi.

Ziara ya Kamati hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania wa kuimarisha miundombinu, kuendeleza matumizi ya teknolojia na kuhakikisha utoaji wa haki unafanyika mapema ipasavyo, kwa uwazi na kwa gharama nafuu.

Kamati ya Jaji Mkuu inayoshughulika na masuala ya maboresho ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe.Mustapha Ismail (wa pili kulia) wakisiliza taarifa ya maendeleo ya Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Simiyu kutoka kwa Mkandarasi wa Mradi huo wakati walitembelea mradi huo kwa lengo la kuukagua. 

Kamati ya Jaji Mkuu inayoshughulika na masuala ya maboresho ikiongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe.Mustapha Ismail (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja mbele ya jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Simiyu baada ya kulikagua. Wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Deo Nangela, wa pili kulia ni Jaji wa Kuu Kanda ya Iringa, Mhe. Mariam Mchomba, wa kwanza kulia ni Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu, Bw. Gasto Kanyairita, wa kwanza kushoto ni Hakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu, Mhe. Martha Mahumbuga. Waliosimama nyuma ni sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Simiyu.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni