· Asema hakuna Hukumu inayozidi Siku 90
Na HALIMA MNETE, Mahakama-Dodoma
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mheshimiwa Eva Kiaki
Nkya, leo amesema Mahakama imefanikiwa kupunguza mashauri sugu hadi kufikia
asilimia 4.5 yakilinganishwa na asilimia 21 miaka mitano iliyopita.
Mhe. Nkya aliyasema hayo jana tarehe 25 Novemba, 2025 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma wakati
akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa maboresho ya huduma za kimahakama wakati
wa ziara ya Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera aliyetembelea
Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma akiwa pamoja na Naibu Waziri,
Mhe. Zainab Katimba.
Akitoa taarifa hiyo, Msajili Mkuu alisema kuwa Mahakama
imeendelea kutekeleza mageuzi makubwa yenye lengo la kuharakisha upatikanaji wa
haki na kupunguza mlundikano wa mashauri nchini.
Kwa mujibu wa takwimu alizotoa, hadi kufikia mwisho wa mwezi
Oktoba mwaka huu, jumla ya mashauri 298,400 yalifunguliwa katika ngazi
mbalimbali za Mahakama na kati ya hayo 212,000 yamesikilizwa na kukamilika,
sawa na asilimia 71.1. Mashauri yanayoendelea ni 41,000, huku mashauri sugu (backlog)
yakiwa 1,951 pekee, sawa na asilimia 4.5, yakilinganishwa na asilimia 21 miaka
mitano iliyopita.
Msajili Mkuu alisema kuwa tangu kuanza kwa mwaka huu 2025
hakuna hukumu yoyote katika Mahakama zote nchini iliyozidi siku 90, kama
inavyoelekezwa na sheria, jambo linaloonesha ufanisi katika utoaji wa haki.
Akifafanua zaidi, alisema Mahakama imepunguza muda wa
wastani wa usikilizaji wa mashauri kutoka siku 554 kwa mwaka 2015 hadi siku 67
kwa sasa.
Aidha, alieleza kuwa, mashauri ya jinai ni asilimia 57 na
mashauri ya madai ni asilimia 43, huku Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani
zikiendelea na vikao maalum vya kumaliza mashauri ya kiuchumi, kodi na
biashara.
Kwa upande wa mashauri katika Mahakama za Chini, Msajili
Mkuu alisema kuwa, mashauri yote yanatarajiwa kukamilika mwishoni mwa Desemba
mwaka huu, isipokuwa yale ambayo siyo chini ya mamlaka ya Mahakama hizo na
kwamba lengo la kumaliza mashauri yote sugu nchini ni Juni 2026.
Katika eneo la huduma kwa wateja, alieleza kuwa Mahakama
imeimarisha mifumo ya upatikanaji wa taarifa na malalamiko kwa kutumia ‘Chatbot
ya WhatsApp 0754 500 400’, uwepo wa madawati ya huduma kwa mteja katika kila Mahakama,
tovuti ya Mahakama na Kituo cha huduma kwa wateja. Kwa mwaka huu maoni 2,445
yamepokelewa, ambapo 1,977 yameshughulikiwa.
Msajili Mkuu alihitimisha kwa kusema kuwa Mahakama
itaendelea kusimamia kikamilifu utekelezaji wa mikakati ya maboresho
iliyojiwekea ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma bora, za viwango na mapema
ipasavyo.
“Lengo letu ni kuwa Mahakama yenye ufanisi, uwazi na
inayomlinda mwananchi. Tutaendelea kusimamia kila hatua hadi pale mashauri yote
sugu yatakapomalizika ifikapo Juni 2026,” alisisitiza Mhe. Nkya.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mheshimiwa Eva Kiaki Nkya akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa maboresho ya huduma za kimahakama wakati wa ziara ya Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera alipotembelea Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma jana tarehe 25 Novemba, 2025 akiwa pamoja na Naibu Waziri, Mhe. Zainab Katimba (hawapo katika picha).
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera (katikati) akifurahia jambo na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba (kushoto) na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) wakati wa mazungumzo na watumishi wa Mahakama ya Tanzania yaliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma jana tarehe 25 Novemba, 2025.




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni