Ijumaa, 28 Novemba 2025

MAHAKIMU NANYUMBU WAENDESHA MAFUNZO YA USULUHISHI KWA WAJUMBE MABARAZA

Na SHARIFU MWAYA-Mahakama, Mtwara

Mahakama ya Tanzania katika Wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara, hivi karibuni iliendesha mafunzo kwa wajumbe wa Mabaraza ya Usuluhishi ya Kata ili kuimarisha uelewa na uwezo wa watendaji katika jamii kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Nanyumbu, Mhe. Asifiwe Jembe aliendesha mafunzo hayo kwa kushirikiana na Mahakimu Wakazi, Mhe. Delphina Charles, Lemister Mtoni na Aloyce Makendi

Wajumbe walioshiriki kwenye mafunzo hayo walitoka Kata ya Mangaka na Kilimanihewa na Mabaraza ya Usuluhishi ya Jumuiya za Kidini, Wasaidizi wa Kisheria, Ofisi ya Ustawi wa Jamii na Jeshi la Polisi – Dawati la Jinsia.

Akizungumza kwenye mafunzo hayo, Mhe. Jembe alisisitiza umuhimu wa kuzingatia taratibu za kisheria katika usuluhishi wa migogoro ya ndoa, pamoja na uelewa sahihi wa namna ya ujazaji wa nyaraka kwa Mabaraza hayo na kujikita katika majukumu yao kwa mujibu wa sheria, kanuni na miongozo iliyowekwa.

Alisisitiza pia umuhimu wa ushirikiano kati ya Mahakama, vyombo vya dola, Viongozi wa Dini na Wadau wengine katika kutoa suluhu za hiari, kuimarisha imani ya wananchi katika mifumo ya utatuzi wa migogoro na kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani.

Mafunzo haya yalilenga kuimarisha uelewa na uwezo wa watendaji wa usuluhishi katika ngazi ya jamii ili kuhakikisha migogoro inatatuliwa kwa haki, weledi, mapema ipasavyo na kwa njia ya amani.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Nanyumbu, Mhe. Asifiwe Jembe (kushoto) akizungumza na Wadau katika mafunzo yaliyoongozwa na Mahakimu wa Mahakama hiyo.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mangaka, Mhe. Aloyce Makendi (kushoto) akiendelea na mafunzo kwa jopo la washiriki.

Mahakimu wa Mahakama za Wilaya ya Nanyumbu katika picha ya pamoja na Viongozi wa Mabaraza na Wadau mbalimbali.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA- Mahakama, Dodoma

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni