Jumatatu, 8 Desemba 2025

TAWJA MBEYA YATOA ELIMU YA UKATILI WA KIJINSIA KWA WANAWAKE NA WATOTO

Na. DANIEL SICHULA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga amefungua mafunzo ya utoaji elimu ya kupinga ukatili wa kijinsia mitandaoni ikiwa ni maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto ikiwemo rushwa ya ngono.

Mhe. Tiganga amewakumbusha washiriki na wadau kwamba unyanyasaji wa kijinsia mitandaoni si suala la utani bali ni uzalilishaji mkubwa ambao umekuwa ukiathiri afya ya akili za wanajamii hasa vijana na watoto pia kutoa wito kwa wadau kusimama kidete kupinga ukatili wa kijinsia mitandaoni ili kutengeneza mazingira salama kwa kila mmoja wetu.

“Ni muhimu kukumbuka kuwa kuna madhara makubwa ya tabia na maneno yetu mitandaoni, kilichoandikwa mtandaoni kimeandikwa. Unaweza usione madhara yake leo lakini baadaye itakuathiri tu.  Inatupasa kutumia teknolojia na mitandao ya kijamii vizuri ili kuileta jamii pamoja kwenye mawasiliano chanya kuliko kutumia kama njia ya kuwaathiri wengine hasa vijana na watoto,’’ alisema Mhe. Tiganga.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Victoria Nongwa, alifafanua kauli mbiu ya mwaka 2025 katika maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto.

“Katika kuadhimisha siku ya kupinga ukatili wa kijinsia mitandaoni, tumejielekeza zaidi katika utoaji elimu ya uelewa kwa jamii juu ya ukatili wa kijinsia hasa ya rushwa ya ngono katika katika nyanja mbalimbali,’’ alisema Mhe. Nongwa

Aidha, alisema kuwa, utoaji elimu ya kupinga ukatili wa kijinsia kwa washiriki na wanafunzi wa kitivo cha sheria wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Mbeya (CUoM) elimu itakayotolewa ni kwa vitendo kwa kutumia Mahakama ya mfano (Mootcourt) ili kila mshiriki aweze kuelewa juu ya uendeshaji wa kesi za aina hiyo ya ukatili wa kijinsia.

Wakati huo huo, Mkuu wa Kitivo cha Sheria wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Mbeya Dkt. Abduraman Kaniki ameshukuru uongozi wa TAWJA Kupitia Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya kwa kuchagua Chuo hicho katika utoaji wa elimu ya kupinga ukatili wa kijinsia.

“Napenda kuwapongeza uongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya kutoa elimu hii kwa wanafunzi hawa, kwani watajifunza vitu vingi na kwakua elimu inatolewa kwa vitendo na kila mmoja wetu atashuhudia namna kesi zinavyoendeshwa mahakamani hakika hili ni darasa muhimu sana kwa wanafunzi wa sheria walioko hapa katika kupinga ukatili wa kijinsia mitandaoni na kuweza kutambua matumizi salama ya mitandao,” alisema Dkt. Kaniki.

Katika utoaji wa elimu hiyo TAWJA Kanda ya Mbeya imeshirikiana na wadau wa haki jinai wakiwemo Mahakimu, Mawakili wa Serikali, TAKUKURU, Dawati la jinsia, Mawakili wa Kujitegemea, Wahadhili pamoja na Maafisa Ustawi wa Jamii. 

Washiriki wa Mahakama ya Mfano (Mootcourt) pamoja na wadau katika utoaji wa elimu ya kupinga ukatili wa kijinsia walitunukiwa vyeti pamoja na vikombe vyenye ujumbe wa kupinga ukatili wa kijinsia mitandanoni.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau wa haki jinai waliotoe elimu ya kupinga ukatili wa kijinsia mitandaoni watatu kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Victoria Nongwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akifungua mafunzo ya kupinga ukatili wa kijinsia mitandaoni .

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Victoria Nongwa akifafanua jambo wakati wa utoaji elimu ya kupinga ukatili wa kijinsia mitandaoni.


Mawakili Msomi wa Kujitegemea Bw. Philip Mwakilima (kulia) alikuwa sehemu ya watoa elimu kwenye mafunzo hayo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akiwatunuku vyeti washiriki wa mafunzo hayo na kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Victoria Nongwa.
Sehemu ya wanafunzi wa CUoM wakisikiliza kwa makini wakati mahakama ya mfano (mootcourt) ikiendelea.




Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Mwanjelwa Mhe. Joyce P. Massawe akitambulisha uongozi wa Mahakama Mbeya.





 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni