Jumatano, 31 Desemba 2025

UJENZI WA MAHAKAMA MPYA YA WILAYA LUSHOTO WAIVA

Na FAUSTINEKAPAMA-Mahakama, Lushoto

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, leo tarehe 31 Desemba, 2025 amekabidhi kwa Mkandarasi Namis Cooperate Limited michoro na eneo itakapojengwa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto kwa gharama ya fedha za ndani Shilingi za Kitanzania Bilioni 4.272.

Makabidhiano hayo yalifuatiwa na utiaji saini wa mkataba wa ujenzi uliofanywa na Prof. Ole Gabriel, kwa upande wa Mahakama, na Bw. James Msumali, kwa niaba ya Mkandarasi.

Hafla hiyo imeshuhudiwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Lushoto, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, pamoja na Viongozi wengine.

Viongozi wengine waliokuwepo ni Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batlida Buriani, Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Mhe. Zephania Sumaye, Wabunge na wengine kutoka Taasisi mbalimbali, Mahakama ya Tanzania na Wadau.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mtendaji Mkuu amemtaka Mkandalasi kukamilisha mradi huo wa ujenzi ndani ya siku 395 kwa mujibu wa mkataba na kuonya kuwa hapatakuwepo na muda wa nyongeza.

‘Nimeshamwelekeza Mkandarasi kuwa inapofika tarehe 15 Februari, 2027 saa 4 asubuhi, tutakuwa hapa kwa ajili ya kupokea jengo letu zuri, nikuombe Waziri, Mkuu wa Mkoa na Viongozi wengine muwepo siku hiyo…

‘Hatutakuwa na muda wa nyongeza, hatutakuwa na nyogeza ya gharama na hatutakuwa na utani kwenye suala la kazi hii, ni kazi muhimu, wananchi wanasubiri Mahakama hii kwa shauku kubwa,’ amesema.

Prof. Ole Gabriel ameeleza kuwa Mahakama hiyo ni ya kisasa na yenye mfano kwani itakuwa kama maabara inayowawezesha Wanafunzi wanaosoma Sheria katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto kufanya mazoezi kwa vitendo.

Kwa upande wake, Mhe. Prof. Shemdoe amemtaka Mkandalasi kununua vifaa vya ujenzi ndani ya Wilaya ya Lushoto, ikiwemo mbao, misumari na vingine, jambo litakalowezesha fedha kuzunguka na kuwanufaisha wananchi wa eneo hilo.

Ameelekeza pia vijana waliopo katika maeneo ya karibu kupatiwa ajira kwenye mradi huo na kusisitiza kazi ya ujenzi kukamilika kwa wakati. Hivyo akamhimiza Mkandarasi kuweka mpango kazi ili kuhakikisha anakabidhi jengo hilo mwezi Februari, 2027.

‘Mimi kama Mbunge wa Jimbo hili, tutakwenda sambamba, nitahakikisha ninafuatilia kwa ukaribu sana. Sina wasiwasi na usimamizi wa jengo hili,’ amesema.

Naye Mkuu wa Mkoa ameeleza kuwa ujenzi wa Mahakama hiyo utasaidia wananchi kupata haki mapema ipasavyo na bila kutumia gharama.

Ametumia fursa hiyo kuwakumbusha wananchi waliojitokeza kushuhudia tukio la makabidhiano hayo kuwa Mahakama ya kwanza Tanganyika ilijengwa Tanga, hivyo ujenzi wa Mahakama hiyo mpya ya Wilaya ni kuendeleza historia katika Mkoa huo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Lushoto ameihakikishia Mahakama ya Tanzania kuwa uongozi wa Wilaya yake utakuwa bega kwa bega kuhakikisha usalama kuanzia kwenye vifaa vya ujenzi na kutoa ushirikiano wowote watakaouhitaji wakati wa utekelezaji wa mradi huo.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto, Bi. Victoria Chilewa, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha fedha za utekelezaji wa mradi huo.

Amesema kuwa ujenzi wa Mahakama hiyo utasaidia kuimarisha huduma za utawala bora na kusogeza huduma za utoaji haki karibu na wananchi. Amesema kuwa kama halmashauri wataendelea kutoa ushirikiano utakakaohitajika katika sekta zote.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel [kulia] akibadilishana na Mkandalasi nyaraka za ujenzi wa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto leo tarehe 31 Desemba, 2025 Lushoto Mkoani Tanga.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel [kulia] pamoja na Bw. James Msumali wakitia saini mkataba wa ujenzi wa Mahakama hiyo. Picha chini wakionesha mkataba huo.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Lushoto, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, akizungumza kwenye hafla ya makabidhiano ya mradi wa ujenzi wa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akifafanua jambo wakati wa hafla hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batlida Buriani akizungumza kwenye hafla hiyo. Picha chini ni Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Mhe. Zephania Sumaye.


Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto, Bi. Victoria Chilewa, akizungumza neno kwenye hafla hiyo. Picha chini ni Mkurugenzi wa Maendeleo na Usimamizi wa Miliki wa Mahakama ya Tanzania, Mhandisi Moses Lwiva akitoa maelezo mafupi ya mradi wa ujenzi wa Mahakama hiyo.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akiwaonesha Viongozi mbalimbali michoro na mwonekano wa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto.. Picha chini Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania akiwaonesha Viongozi sehemu Mahakama hiyo itakapojengwa.



Mwonekano wa sasa wa Mahakama ya Wilaya Lushoto [juu na chini].


Mwonekano wa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto mara ujenzi utakapokamilika tarehe 15 Februari, 2027.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni