Alhamisi, 1 Januari 2026

MAOMBI MANNE YA MAHAKAMA TAMISEMI

  • Waziri ayakubali, atoa maelekezo

Na FAUSTINEKAPAMA-Mahakama, Lushoto

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, ameyakubali maombi yaliyowasilishwa na Mahakama ya Tanzania, ikiwemo kusamehe tozo zinazotakiwa kulipwa wakati wa utekelezaji wa miradi ya ujenzi nchini.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, aliwasilisha maombi hayo jana tarehe 31 Desemba, 2025 kwenye hafla ya kukabidhi eneo itakapojengwa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto kwa gharama ya fedha za ndani Shilingi za Kitanzania Bilioni 4.272. Mhe. Prof. Shemdoe alikuwa Mgeni Rasmi kwenye hafla ya makabidhiano hayo iliyofanyika wilayani Lushoto.

Katika maombi hayo, Prof. Ole Gabriel, kwa niaba ya Jaji Mkuu, aliomba Mahakama isitozwe gharama sizizo za kisheria, ikiwemo zinazohusu utawala wa kihalmashauri, pale panapohitajika viwanja vya ujenzi wa majengo ya Mahakama, ama kwa ajili ya huduma za Mahakama au makazi.

Mtendaji Mkuu alimweleza Waziri kuwa huduma zitakazotolewa na Mahakama baada ya kutekeleza miradi ya ujenzi huo itawanufaisha wananchi wa halmashauri husika. ‘Tunakuomba Waziri, kama ikikupendeza, kusamehewa hizi gharama za kiutawala ili kazi nyingine ziweze kuendelea,’ alisema.

Prof. Ole Gabriel alitoa mfano katika Mkoa wa Tanga ambapo gharama za kiutawala kwenye halmashauri ni Shilingi za Kitanzania 250,970,000 kwa mchanganuo kwenye mabano kwa kila Wilaya za Korogwe [12m/=], Lushoto [10m/=] na Muheza kuna viwanja tisa [31,500,000/=].

Kwa upande wa Pangani kuna viwanja nane [14m/=], Tanga [3.9m/=], Handeni kuna viwanja 12 [22.99m/=], Mkinga [13m/=], Kilindi [24m/=] na pia kuna viwanja kwa ajili ya nyumba za Majaji ambavyo vinafanyiwa upembuzi [118m/=].

Ombi lingine linahusu utoaji wa viwanja kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama na nyumba za makazi kwa Majaji na Mahakimu. Prof. Ole Gabriel ameomba Wakuu wa Mikoa kuendelea kuratibu maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu TAMISEMI kushirikiana na Mahakama ya Tanzania na Wizara ya Fedha kuhakikisha Kata na Wilaya zote nchini zinapata majengo yake.

‘Haya maelekezo aliyatoa tarehe 5 Aprili, 2025 akiwa anazindua jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Naomba nikupe taarifa kwamba kuna pa kuanzia. Wapo Wakuu wa Mikoa watatu, Rukwa, Katavi na Tanga, ambao tayari wameshalibeba kidedea suala hili,’ amesema.

Ombi lingine linahusu Wakuu wa Mikoa kutenga fedha kwa ajili ya kuwezesha kufanyika kwa Kamati za Maadili za Mahakimu. Mtendaji Mkuu alimweleza Waziri kuwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya ni Wenyeviti wa Kamati hizo katika ngazi husika.

Amemuomba Waziri kushajirisha suala hilo ili Wakurugenzi ili watenge bajeti kwa ajili ya kuimarisha Kamati hizo na watambue kuwa zipo kwa mujibu wa Sheria, kwani pale haki inapotendeka, haki pia inatamalaki na ndiyo hasa Dira ya 2050 inavyoelekeza.

Ombi la nne linahusu ujenzi wa barabara itakayowezesha wananchi kufika kwa urahisi kwenye Mahakama hiyo mpya. Mtendaji Mkuu alimuomba Waziri kuwaelekeza TARURA kutengeneza barabara angalau kwa changalawe kwa kuanzia kabla ya kiwango cha lami ili kumwezesha Mkandarasi kuendelea na ujenzi.

Akijibu maombi hayo kwa kuanzia na suala la gharama za utawala, Prof. Shemdoe amemwelekeza Katibu Mkuu wa TAMISEMI kuona namna kama kufutwa kwa tozo hizo hakutavunja sheria. ‘Nadhani milioni 250 siyo fedha nyingi kihivyo, zinaweza kuondolewa na mambo mengine haya ya Mahakama yakaendelea,’ amesema.

Akizungumzia suala la Kamati za Maadili, Mhe. Prof. Shemdoe pia amemwelekeza Katibu Mkuu kutoa mwongozo kwa mamlaka za Serikali za Mitaa ili kutenga bajeti kuwawezesha Wakuu wa Mikoa na Wilaya kusimamia Kamati hizo kwa ajili ya watendaji wa Mahakama.

“Hili ni jambo la msingi ambalo lipo kisheria na lipo kwenye utaratibu wa kazi za Viongozi hawa. Naomba utoke waraka wa kuweza kuwaelekeza Wakurugenzi kutenga bajeti kwenye eneo hili,” amesema.

Kuhusu kuwepo kwa majengo ya Mahakama kwenye kila Kata na Wilaya, Waziri Shemdoe alisema kuwa tarehe 16 Desemba, 2025 alisaini barua kwenda kwa Wakuu wa Mikoa kuhakikisha wanalichukulia zoezi hilo kwa uzito mkubwa.

Alifurahi kusikia kuwa Wakuu wa Mikoa ya Rukwa, Katavi na Tanga wamekuwa mstari wa mbele, hivyo kwa mara nyingine aliwaelekeza Wakuu wa Mikoa 23 iliyobaki kulifanyia kazi jambo hilo na kulichukulia uzito unaostahili.

Kuhusu TARURA, Waziri Shemdoe ameielekeza Taasisi hiyo kuanzia Wilaya ya Lushoto, Mkoa wa Tanga na Makao Makuu kuhakikisha kwenye bajeti inayofuata wanatenga fedha kwa ajili ya barabara ya kwenda kwenye jengo hilo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi nyaraka na eneo kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akisisitiza jambo wakati wa hafla hiyo. 

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga, Bw. Jumanne Muna akitoa utambulisho wa Viongozi na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya makabidhiano hayo. Picha chini ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Lushoto, Mhe. Rose Ngoka.



Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe [katikati waliokaa] ikiwa katika picha ya pamoja na Viongozi mbalimbali [juu na chini] kwenye halfa hiyo.


Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe [katikati waliokaa] ikiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa dini [juu] na Wadau [chini] kwenye halfa hiyo.


Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe [katikati waliokaa] ikiwa katika picha ya pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya Lushoto [juu] na watumishi wa Mahakama [chini] kwenye halfa hiyo. Picha ya pili chini ni Wakandarasi wa mradi wa ujenzi huo.




 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni