Jumatatu, 19 Januari 2026

JAJI KIONGOZI ABAINISHA MAMBO MANNE KUIMARISHA MATUMIZI YA USULUHISHI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani amewataka Majaji, Mahakimu, Wasuluhishi, Wadau na Wananchi kwa ujumla kuzingatia na kutekeleza mambo manne muhimu ili kufikia malengo yaliyokusudiwa katika kuendeleza na kutambua umuhimu wa matumizi ya usuluhishi.

Akizungumza leo tarehe 19 Januari, 2026 katika Hafla ya Utoaji Tuzo kwa Wadau wa Usuluhishi kwa mwaka 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam, Mhe. Dkt. Siyani amesema, Mahakama imeendelea kuchukua hatua mbalimbali na kuweka vipaumbele mahususi vyenye lengo la kuhakikisha mashauri yanayosajiliwa mahakamani, yanakamilika mapema ipasavyo na usuluhishi kama sehemu ya utekelezaji wa takwa la katiba ya nchi yetu katika ibara ya 107A (2), umepewa kipaumbele kikubwa.

“Nimesikia takwimu zilizowasilishwa na Jaji Mfawidhi kuhusu mafanikio ya usuluhishi kwa mwaka 2025, ni dhahiri kwamba Mahakama na wadau wa usuluhishi wamendelea kutumia usuluhishi kama nyenzo madhubuti yenye kuaminika katika utatuzi wa migogoro. Hata hivyo, kwakuzingatia wingi wa mashauri katika nchi yetu, bado kuna nafasi zaidi kwa wananchi kutumia njia hii kutatua migogoro yao,” amesema Jaji Kiongozi.

Mhe. Dkt. Siyani ameyataja mambo manne ya kuzingatia katika kuendeleza matumizi ya Usuluhishi kuwa ni pamoja na kuongeza elimu kwa umma kuhusu usuluhishi, kuwekeza katika mafunzo endelevu, ni muhimu kuwekeza katika mafunzo ya mara kwa mara kwa wapatanishi, Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kuendeleza na kukuza ushirikiano wa wadau, ni kwa kupitia ushirikiano huu wa karibu kati ya Mahakama na Wadau wote.

Akizungumzia kuhusu kuongeza elimu kwa umma kuhusu usuluhishi, Jaji Kiongozi amesema, ni jukumu la Wadau wote wa Mahakama kuwaelimisha wananchi kwamba haki inaweza pia kupatikana kupitia mazungumzo, maridhiano na makubaliano yanayoheshimu maslahi ya pande zote.

Kuhusu suala la kuwekeza katika mafunzo endelevu, Mhe. Siyani ameeleza kwamba, ni muhimu kuwekeza katika mafunzo ya mara kwa mara kwa wapatanishi ili kuimarisha uelewa, mbinu za njia za usuluhishi, kutambua na kushirikiana katika kujenga mifumo yenye ufanisi na mazingira bora ya uendeshaji wa njia za usuluhishi zinazoendana na vigezo vinavyotumika katika upimaji wa mfumo wa utoaji haki wa migogoro ya madai.

Katika jambo hilo, Jaji Kiongozi amekipongeza Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na Kituo cha Usuluhishi kwa juhudi za kuwezesha mafunzo ya njia ya upatanishi kwa Wahe Majaji na Mahakimu katika kuwajengea uwezo wa kufanya usuluhishi.

Katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Mhe. Siyani amewataka Wadau wa Haki kuyazingatia kwa kuwa hayakwepeki katika zama hizi ambapo amesema, “Sote ni mashuhuda wa namna matumizi ya mifumo ya kidijitali yalivyokuwa injini ya mageuzi katika mifumo ya utoaji haki duniani. Uwekezaji katika TEHAMA si hiari, ni muhimu ili kuongeza ufanisi na upatikanaji wa huduma kwa wakati.”

Ameongeza kuwa, Mahakama kupitia mageuzi ya teknolojia, mifumo kama Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) na Usuluhishi Mtandao(Virtual/Online Mediation) yameleta mapinduzi makubwa katika upatikanaji wa huduma za usuluhishi na kwamba matumizi ya teknolojia yamepunguza kwa kiasi kikubwa gharama, muda unaotumika kufika mahakamani, pamoja na nguvu kazi inayohitajika na hivyo kuongeza upatikanaji wa haki bila vikwazo.

Aidha, kuhusu jambo la kuendeleza na kukuza ushirikiano wa wadau, Jaji Kiongozi amesema kuwa, ushirikiano wa karibu kati ya Mahakama na Wadau wote ndio utakaohakikisha kuwa usuluhishi unakuwa njia yenye matokeo endelevu, inayotekelezeka na inayokubalika katika jamii.

Kupitia ushirikiano huu tutaweza kujenga msingi wa kujenga taifa linalothamini mazungumzo, linaloweka mbele maridhiano na linajenga mfumo wa utoaji haki unaotazama utu na maendeleo ya watu wake,” amesisitiza.

Katika hafla hiyo, Mhe. Dkt. Siyani amewajuza Wadau wote wa Mahakama kuwa kutakuwa na Wiki ya Usuluhishi na kuwaomba wadau wote wa usuluhishi na wanufaika wa huduma hizi, kuweka juhudi za pamoja katika kufanikisha wiki hiyo ambayo ni ya kihistoria na inayotarajiwa kutoa fursa nyingi za kutoa elimu ya usuluhishi.

Niwaombe pia wananchi kutumia fursa hii katika kupata elimu na kutatua migogoro kwa njia rahisi na kukuza utamaduni na desturi za kiafrika katika kutatua migogoro nje ya Mahakama kwa njia za maridhiano, hasa kwa kuzingatia uwepo wa Wapatanishi na Wasuluhishi binafsi ambao hivi sasa wanatambulika kisheria,” amesema Jaji Kiongozi.

Kadhalika, Mhe. Dkt. Siyani ametoa wito kwa wadau wote wa mfumo wa utoaji haki, kuchagua njia za usuluhishi kwa mujibu wa sheria, badala ya kupitia mchakato mrefu, wa gharama wa kimahakama unaohitaji kusubiri hukumu ambayo wakati mwingine huongeza maumivu ya mgogoro badala ya kutibu majeraha ya mgogoro kama ilivyo katika njia za usuluhushi ambazo msingi wake mkuu ni maridhiano.

Sambamba na hilo, Mhe. Dkt. Siyani pia wananchi kutumia fursa ya wiki hiyo katika kupata elimu na kutatua migogoro kwa njia rahisi na kukuza utamaduni na desturi za kiafrika katika kutatua migogoro nje ya Mahakama kwa njia za maridhiano, hasa kwa kuzingatia uwepo wa Wapatanishi na Wasuluhishi binafsi ambao hivi sasa wanatambulika kisheria.

Hafla hiyo imebeba kauli mbiu isemayo; 'Kujenga maelewano na kuimarisha ushiriki wa wadau katika upatanishi kwa matokeo endelevu.'



Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akizungumza leo tarehe 19 Januari, 2026 wakati wa Hafla ya Utoaji Tuzo kwa Wadau wa Usuluhishi kwa mwaka 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam.

Picha mbalimbali za Majaji, watumishi wengine wa Mahakama, Wadau  wa Mahakama wakifuatilia hotuba ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (hayupo katika picha) aliyokuwa akiitoa wakati wa Hafla ya Utoaji Tuzo kwa Wadau wa Usuluhishi leo tarehe 19 Januari, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma akizungumza wakati wa Hafla ya Utoaji Tuzo kwa Wadau wa Usuluhishi kwa mwaka 2025 leo tarehe 19 Januari, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Augustina Mmbando akizungumza 
wakati wa Hafla ya Utoaji Tuzo kwa Wadau wa Usuluhishi kwa mwaka 2025 leo tarehe 19 Januari, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Waliopokea tuzo kwenye Hafla ya Utoaji Tuzo kwa Wadau wa Usuluhishi kwa mwaka 2025 iliyofanyika leo tarehe 19 Januari, 2026 kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi kwenye Hafla ya Utoaji Tuzo kwa Wadau wa Usuluhishi kwa mwaka 2025 iliyofanyika leo tarehe 19 Januari, 2026 kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Watoa Mada kwenye Hafla ya Utoaji Tuzo kwa Wadau wa Usuluhishi kwa mwaka 2025 iliyofanyika leo tarehe 19 Januari, 2026 kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji walioshiriki kwenye Hafla ya Utoaji Tuzo kwa Wadau wa Usuluhishi kwa mwaka 2025 iliyofanyika leo tarehe 19 Januari, 2026 kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni