Jumatatu, 19 Januari 2026

JAJI KIONGOZI AKABIDHI TUZO KWA WADAU WA USULUHISHI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, leo tarehe 19 Januari, 2026, amekabidhi Tuzo 26 kwa Wadau wa Usuluhishi baada ya kutambua mchango wao katika kuimarisha matumzi ya usuluhishi kama njia mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Hafla hiyo ya utoaji Tuzo imefanyika kwenye Ukumbi wa Kilimanjaro wa Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania, Naibu Wasajili na Mahakimu wa ngazi mbalimbali na Wadau kutoka Taasisi kadhaa nchini.

Tuzo hizo zimeandaliwa na Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi, kwa kutambua Wadau na Taasisi mbalimbali nchini zinazochangia kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi.

Waliokabidhiwa Tuzo hizo ni Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Naibu Wasajili, Taasisi za Umma na Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, Halmashauri na Manispaa, Ofisi ya Ustawi wa Jamii, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi, Taasisi za Fedha na Wasuluhishi Binafsi.

Utoaji wa Tuzo hizo ulitanguliwa na makala maalum iliyoelezea safari na faida za usuluhishi na kisha kufuatiwa na mada inayosema, ‘Haki kwa Haraka Mapema Ipasavyo; Hatua za Suluhu kabla ya Kesi.’

Mada hiyo iliwasilishwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Dkt. Abdallah Gonzi na kujadiliwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Dkt. Cleophace Morris na Wadau mbalimbali kwa usimamizi wa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliamani Laitaika.

Wadau mbalimbali walitoa uzoefu wao kuhusu masuala ya usuluhishi, akiwemo Katibu Mtendaji wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Bw. George Mandepo, Wakili wa Kujitegemea, Msomi Mpaya Kamara na Msuluhishi Binafsi, Bi. Medeline Kimei.

Wengine ni Msimamizi wa Usuluhishi Malalamiko ya Bima, Bw. Zakaria Muyengi, Msajili wa Malalamiko ya Bima, Bw. Jamal Mwasha na Msuluhishi Malalamiko ya Kibenki, Bw. Ramadhani Mnyonga.

Hii ni mara ya tatu kwa Mahakama Kituo cha Usuluhishi kutoa Tuzo kama hizo kwa Wadau mbalimbali. Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 2024, ikafuatiwa na mwaka 2025.


Wadau mbalimbali wa Usuluhishi [juu na picha mbili chini] wakiwa wameshikilia Tuzo zao baada ya kukabidhiwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.


 Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akipokea kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Tuzo maalum iliyotolewa na Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi. Anayekabidhi Tuzo hiyo ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma. Picha chini akionesha Tuzo hiyo.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara, Mhe. Dkt. Cleophace Morris akipokea Tuzo yake. Picha chini ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Fatuma Khalfan.

Picha chini zinaonesha matukio kadhaa wakati wa utoaji wa Tuzo hizo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni