- Jaji Kiongozi akumbushia njia hiyo muhimu
- Aonesha kukerwa na mapingamizi yanayolenga kuchelewesha haki
Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama,
Dar es Salaam
Uwepo wa vyombo imara na huru
vya utoaji haki ni njia mojawapo ya ulinzi wa amani na utulivu katika jamii
yoyote inayoheshimu misingi ya utawala wa sheria, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu
ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amesema.
Akizungumza kwenye hafla
ya utoaji Tuzo za Usuluhishi jijini Dar es Salaam leo tarehe 19 Januari, 2026,
Mhe. Dkt. Siyani amebainisha kuwa Mahakama ya Tanzania imeendelea kuimarisha
matumizi ya usuluhishi kama njia muhimu ya utatuzi wa migogoro.
‘Kwa upande wangu,
naamini ni muhimu sana kuendelea kukumbushana juu ya hatua hizi na umuhimu wa usuluhishi
katika utatuzi wa migogoro. Kufanya hivyo kutawezesha watu wengi zaidi katika
jamii yetu na wale wanaokuja kuwekeza katika nchi yetu kuona fursa iliyopo
kwenye usuluhishi,’ Jaji Kiongozi amesema.
Mhe. Dkt. Siyani amebainisha
kuwa Ibara ya 107A (2) (d) ya Katiba yaJamhuri ya Muungano wa Tanzania inaitaka
Mahakama kukuza na kuendeleza usuluhishi wakati wa utekelezaji wa jukumu lake
la msingi la utoaji haki.
Amesema kuwa licha ya
kuwa ni matakwa ya kikatiba, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inazungumzia
usuluhishi kama nyenzo muhimu ya kimkakati katika kujenga Taifa lenye uchumi
shindani, jumuishi na imara.
‘Katika uchumi
unaotegemea uwekezaji, ubunifu na kasi ya uzalishaji, usuluhishi unapunguza
muda na gharama za migogoro ya kibiashara, hivyo kuweka mazingira salama na
yenye uhakika kwa wawekezaji na wafanyabiashara,’ amesema.
Akizungumzia upande wa
ustawi jamii, Jaji Kiongozi amebainisha kuwa, usuluhishi unachangia kulinda utu,
kupunguza madhara ya migogoro ya kifamilia, kijamii, ajira na ardhi, na hivyo
kuimarisha mshikamano wa kijamii.
Amesema pia kuwa
usuluhishi ni njia inayotoa nafasi kwa wanawake, vijana na makundi maalum
kushiriki katika kupata haki bila gharama kubwa au vikwazo vya kimuundo.
Kwa upande wa utawala bora,
Mhe. Dkt. Siyani amesema kuwa usuluhishi unajenga imani ya wananchi kwa Taasisi
za utoaji haki kwasababu unategemea uwazi, uadilifu na makubaliano.
‘Usuluhishi hupunguza mlundikano
wa mashauri mahakamani, huongeza ufanisi wa mfumo wa haki na huimarisha dhana
ya uongozi unaozingatia ushirikishwaji na uwajibikaji.
Akizungumzia eneo la ushirikishwaji
wa Wadau wa Usuluhishi, Jaji Kiongozi amesema kuwa Mahakama imeendelea kushirikiana na Wadau wake
katika kukuza na kuimarisha usuluhishi.
Amebainisha kuwa taarifa
za mashauri yanayopitia usuluhishi mahakamani na nje ya Mahakama, pamoja na
mkusanyiko wenye lengo la kutambua michango na mafanikio katika eneo la utoaji
haki kupitia usuluhishi, ni ushuhuda wa kuimarika kwa ushirikishwaji wa Wadau.
‘Kupitia usuluhishi, Wadau
wamefanikiwa kutatua migogoro mingi ikiwemo ile ya ardhi, biashara na ajira kwa
kutumia njia za mazungumzo na maridhiano. Haya yote yanaashiria mtazamo mpya
unaodhihirisha kwamba, migogoro haihitaji kusubiri mabishano mahakamani, hatua
ndefu na za kiufundi zinazoweza kuwanyima watu haki, na matumizi ya gharama kubwa
ili kupata hukumu,’ amesema.
Mhe. Dkt. Siyani ametoa rai,
hasa kwa Aadau, Mawakili wasomi wote, wawe wa Serikali na, au binafsi, na hata
wale walioruhusiwa kutoa msaada wa kisheria, kutoona mbinu za kiufundi, hasa
kupitia mapingamizi ya awali kama njia rahisi ya kumaliza migogoro.
‘Ukweli ni kuwa mengi ya mapingamizi
hayo, hayamalizi migogoro bali yanachelewesha mchakato wa haki. kutenda haki
bila kufungwa kupita kiasi na masharti ya kiufundi yanayoweza kukwamisha haki
kutendeka.
‘Badala yake, wasomi hawa
na jamii kwa ujumla, sasa itambue umuhimu wa usuluhishi na kwamba migogoro yao
inaweza kutatuliwa mapema, haraka na kwa njia inayolinda mahusiano ya kijamii
na kiuchumi,’ amesema Jaji Kiongozi.
Wakati wa hafla hiyo,
jumla ya Tuzo 26, ambazo zimeandaliwa na Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha
Usuluhishi, zimetolewa kwa Wadau mbalimbali wa usuluhishi.
Wadau hao ni Majaji wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Naibu Wasajili, Taasisi za Umma na Serikali, Mawakili
wa Kujitegemea, Halmashauri na Manispaa, Ofisi ya Ustawi wa Jamii, Tume ya
Usuluhishi na Uamuzi, Taasisi za Fedha na Wasuluhishi Binafsi.
Sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania [juu na chini] wakiwa kwenye hafla hiyo.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni