Jumanne, 20 Januari 2026

MCHANGO WA MAHAKAMA KITUO CHA USULUHISHI KWENYE UTATUZI WA MIGOGORO HAUNA SHAKA

  • Yafanikiwa kusuluhisha mashauri yenye thamani ya zaidi ya trilioni moja
  • Jaji Mfawidhi asema usuluhishi nguzo ya ustawi, maendeleo endelevu katika Taifa

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi, imefanikiwa kusuluhisha mashauri 327 yenye thamani ya Shilingi za Kitanzania 1,402,732,991,440.17 kwa mwaka 2025.

Hayo yamebainishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma, kwenye hafla ya utoaji Tuzo za Wadau wa Usuluhishi iliyofanyika jana tarehe 19 Januari, 2026 jijini Dar es Salaam.

Mhe. Maruma alibainisha kuwa mashauri hayo 327 ni kati ya 342 yaliyopokelewa kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na Divisheni ya Ardhi katika kipindi hicho.

‘Idadi hii ilijumuisha migogoro 174 ya ardhi yenye thamani ya Shilingi za Kitanzania 161,071,243,621.51 na migogoro 153 ya madai ya kawaida yenye thamani ya Shilingi za Kitanzania 1,241,157,477,818.66,’ alisema.

Jaji Mfawidhi alibainisha pia kuwa kati ya migogoro hiyo, 47 ilihusisha Taasisi za Mabenki yenye thamani ya Shilingi za Kitanzania 148,119,498,132.26 na migogoro 56 yenye thamani ya Shilingi za Kitanzania 49,431,023,475.35 kutoka Taasisi za kiserikali.

Mhe. Maruma alisema pia kuwa katika kipindi hicho, Mahakama Kuu Kituo cha Usuluhishi ilifanikiwa kwenye upatanishi wa jumla ya mashauri 87 yenye thamani ya Shilingi za Kitanzania110,813,010,662.08 kwa makubaliano ya Shilingi za Kitanzania 36,592,613,760.31, hivyo kuokoa kiasi cha Shilingi za Kitanzania 74,220,396,901.77.

‘Kati ya mashauri hayo, kiasi cha Shilingi za Kitanzania 46,512,751,302 kiliokolewa kwa upande wa migogoro iliyohusisha Taasisi za Serikali kwa kufikia makubaliano ya Shilingi za Kitanzania 2,918,272,174 na kiasi cha Shilingi za Kitanzania 139,743,883,107 kwa migogoro ya kibenki kwa kufikia makubaliano ya Shilingi za Kitanzania 8,375,615,025,’ alisema.

Akizungumzia upande wa ngazi nyingine za Mahakama zilizosalia zikijumuisha Mahakama Kuu, Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya, Jaji Mfawidhi alieleza kuwa jumla ya mashauri 315 yalifanikiwa kumalizika katika hatua ya usuluhishi.

Aidha, alisema kuwa Wadau wa nje ya Mahakama, kupitia Mabaraza ya Kata, Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Maofisa Ustawi wa Jamii, Viongozi wa Dini na Wazee wa Mila, wamefanikiwa kusuluhisha migogoro 537 iliyomalizika kwa njia ya upatanishi.

‘Ukiangalia takwimi hizi utaona kupitia usuluhishi kumewezesha rasilimali hizi ambazo zilikuwa zimeshikiliwa au kuzuiliwa katika migogoro zimeweza kurudi katika mzunguko wa uchumi,’ Mhe. Maruma alisema.

Jaji Mfawidhi alieleza pia kuwa ingawa idadi ya mashauri yaliyomalizika kwa suluhu inaonekana kuwa ndogo, bado inaakisi mwelekeo chanya wa kuendelea kuimarika kwa matumizi ya usuluhishi kama nyenzo muhimu ya utatuzi wa migogoro ndani na nje ya mfumo wa Mahakama.

Alisema kuwa takwimu hizo pia si namba za kwenye karatasi, bali zinatoa tafisiri ya familia zilizookolewa dhidi ya migawanyiko na maumivu ya migogoro ambayo huwa haitibiki kwa nakala za hukumu.

Mhe. Maruma alibainisha kuwa takwimu hizo pia zinaangazia mahusiano ya kazi yaliyorejeshwa, migogoro ya ardhi iliyotamatishwa kwa amani na jamii zilizoepuka mgogoro wa kudumu.

Aidha, kupitia usuluhishi, alisema kuwa gharama nyingi zinazotokana na mgogoro huepukika, ikijumuisha rasilimali fedha na muda zinazotumika katika uendeshaji wa mashauri kupitia utaratibu wa kimahakama.

Alitaja migogoro mingine kama ushikiliaji au uzuiaji wa rasilimali zinazobishaniwa katika mgogoro kwa muda mrefu bila kuwepo katika mzunguko wa kiuchumi na ukwamishaji wa shughuli za kiuchumi kutokana na mazuio ya kisheria ambayo husababisha kudorora kwa uchumi au kuvunjika kwa mahusiano ya kibiashara au kijamii.

‘Madhara haya huweza kuepukika kwa kutatua migogoro kupitia usuluhishi. Takwimu hizi zinathibitisha kwamba usuluhishi ni nguzo ya ustawi na mshikamano na maendeleo endelevu katika Taifa letu,’ alisema Jaji Mfawidhi.

Jumla ya Tuzo 26 zilikabidhiwa kwa Wadau wa Usuluhishi mbalimbali baada ya kutambua mchango wao katika kukuza matumizi ya usuluhishi kama njia mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, aliyemwakilisha Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju.

Waliokabidhiwa Tuzo hizo ni Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Naibu Wasajili, Taasisi za Umma na Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, Halmashauri na Manispaa, Ofisi ya Ustawi wa Jamii, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi, Taasisi za Fedha na Wasuluhishi Binafsi.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Zahra Maruma, akizungumza kwenye hafla ya utoaji Tuzo kwa Wadau wa Usuluhishi jana terehe 19 Januari, 2026 jijini Dar es Salaam.

Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu na Wadau mbalimbali [juu na chini] wakiwa kwenye hafla hiyo.



Sehemu nyingine ya Majaji wa Mahakama Kuu na Wadau mbalimbali [juu na chini] wakiwa kwenye hafla hiyo.




Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu na Wadau mbalimbali [juu na chini] waliokabidhiwa Tuzo kwenye hafla hiyo.



Sehemu nyingine ya Majaji wa Mahakama Kuu na Wadau mbalimbali [juu na chini] waliokabidhiwa Tuzo kwenye hafla hiyo.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni