Jumanne, 13 Januari 2026

MKUTANO MKUU WA TMJA WAANZA DODOMA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Mkutano Mkuu wa Mwaka unaowaleta pamoja Mahakama na Majaji wote nchini umeanza leo tarehe 13 Januari, 2026 katika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mkutano huo wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [TMJA] umefunguliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali na Mahakama. 

Jumla ya wanachama wa TMJA zaidi ya 1,200 wamehudhuria Mkutano huo, ambao ni wa pili kufunguliwa na Mkuu wa Nchi tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka 1984. Mkutano mwingine ulifanyika mwaka 1984 na kuhudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Awamu ya Kwanza, Mwalimu Julius Nyerere jijini Arusha. 

Rais Samia aliwasili kwenye ukumbi wa Mkutano majira ya saa 4.30 asubuhi na kupokelewa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, Rais wa TMJA, Mhe. Elimo Masawe, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Homera na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule.

Wengine ni Amidi wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya.

Baada ya kuwasili, wimbo wa Taifa ulipigwa ukafuatiwa na ule wa Afrika Mashariki, huku Bendi ya Jeshi la Polisi ikiongoza wanachama wa TMJA na watumishi wengine kushiriki kuimba nyimbo hizo.

Baada ya utambulisho uliofanywa na Rais wa TMJA, ilifuata burudani kabambe kutoka Kikundi cha Ngoma za Asili Maheza iliyokonga nyoyo za wanachama kufuatia midundo na uchezaji mahiri uliooneshwa na wanamichezo hao.

Mhe. Masawe pia alitumia fursa hiyo, kabla ya kikundi cha ngoma kutumbuiza, kutoa salamu. Katika salamu zake, Rais wa TMJA alimshukuru Rais Samia kwa kukubali mwaliko wao na kuwa mgeni rasmi kwenye Mkutano huo, ukiwa ni mwaka wa 41 tangu kuundwa kwa chama hicho.

‘Uwepo wako umeonesha uwazi na dhamira ya Serikali unayoiongoza katika kuimarisha uhuru wa Mahakama kama ilivyo kauli mbiu ya Mkutano huu, yaani Jukumu la Mahakama Huru katika Utoaji wa Haki,’ alimweleza Mhe. Dkt. Samia.

Mhe. Masawe alimweleza Rais Samia kuwa chama cha JMTA ni cha kitaaluma chenye malengo mbalimbali, ikiwemo kukuza na kulinda uhuru wa Mahakama kama sharti la msingi na la lazima la utekelezaji wa majukumu ya kimahakama.

Malengo mengine ni kukuza maslahi na ustawi wa wanachama, kudumisha hadhi, heshima na tamaduni za Majaji na Mahakimu, kuongeza na kuendeleza ujuzi, maarifa na uelewa wa Majaji na Mahakimu kuhusu majukumu yao ya kimahakama kupitia tafiti endelevu na elimu ya kitaaluma.

Mengine ni kutoa taarifa na machapisho mbalimbali kuhusu masuala yenye maslahi au yanayowahusu wanachama, kuandaa makongamano na mikutano ya wanachama na kudumisha mahusiano ya karibu kadri inavyowezekana miongoni mwa wananchama na kushirikiana, na inapobidi, kujiunga na vyama au Taasisi nyingine zenye malengo yanayofanana.

Jumla ya mada 12, ikiwemo ‘Jukumu la Mahakama la Mahakama Huru katika Utoaji Haki’ zinatarajiwa kuwasilishwa wakati wa Mkutano huo wa siku tatu na kufuatiwa na Bonanza litakaloshirikisha michezo mbalimbali, ikiwemo Mpira wa Miguu, Mpira wa Pete, Kamba na mingine mingi.

Kama sehemu ya Mkutano huu, wamachama wa TMJA wanatarajia kufanya matendo ya huruma kwenye vituo viwili ambavyo vinahudumia watoto wenye changamoto mbalimbali wanaoanzia umri wa miezi sita hadi miaka 17.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju baada ya kuwasili Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma kwa ajili ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mahakimu na Majaji leo tarehe 13 Januari, 2026. Picha chini akisalimiana na Rais wa Chama hicho, Mhe. Elimo Masawe.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongozana na mwenyeji wake, Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju kuelekea kwenye chumba maalum kilichokuwa kimeandaliwa kabla ya kuelekea katika ukumbi wa mikutano.

Kikundi cha Ngoma za Asili Maheza kikitumbuiza wakati wa Mkutano huo. Picha chini ni Askari akionesha manjonjo huku akiongozwa na Bendi ya Jeshi la Polisi.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan [katikati waliokaa] akiwa katika picha ya pamoja na Meza Kuu. Picha chini akiwa kwenye picha ya pamoja na wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania.



 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni