Jumatano, 14 Januari 2026

Mkutano Mkuu wa Mwaka TJMA 2026

MAJAJI, MAHAKIMU WAPATIWA MAARIFA KUHUSU UHIFADHI WANYAMAPORI, MIAMALA YA KIFEDHA

Na FUSTINE KAPAMA na HALIMA MNETE-Mahakama, Dodoma

Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [TJMA] umeingia siku ya pili leo tarehe 14 Januari, 2026 kwa wanachama kupitishwa kwenye mada kadhaa na wawezeshaji wabobezi ili kuwajengea uelewa kwenye maeneo mbalimbali, ikwemo uhifashi wa wanyamapori, utalii na miamala ya kifedha.

Mada ya kwanza kuwasilishwa kwenye Mkutano huo wa siku tatu, unaofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania [Judiciary Square] jijini Dodoma, ilihusu mafanikio, changamoto na mustakabali wa ulinzi wa wanyamapori Tanzania.

Ofisa Mwandamizi kutoka Shirika la Hifadhi Tanzania [TANAPA] Joachim Tesha, ndiye aliyewasilisha mada hiyo, huku Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Winfrida Korosso, akiwa msimamizi mkuu wa majadiliano.

Kadhalika, wanachama wa TMJA walipitishwa kwenye mada linganifu inayohusu dhana ya uhifadhi-Mamlaka Ngorongoro; mafanikio, fursa na changamoto. Mada hiyo iliwasilisha na Ofisa kutoka kwenye Mamlaka hiyo Usaje Mwambene.

Baada ya mapumziko mafupi, wajumbe wa Mkutano waligawanyika kwenye makundi matatu. Kundi la kwanza linajumuisha Majaji wa Mahakama ya Rufani ambalo lilipitishwa kwenye mada inayohusu mchango wa utalii kwenye uchumi na maendeleo ya nchi.

Mada hiyo iliwasilishwa na Ofisa Mwandamizi kutoka TANAPA July Lyimo, huku Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Rehema Mkuye, akiwa msimamizi mkuu wa majadiliano.

Kundi jingine limejumuisha Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Naibu Wasajili na Wasaidizi wa Sheria wa Majaji. Mada kwenye Kundi hili ilihusu uhifadhi endelevu wa rasilimali ya wanyamapori na mchango wa Mahakama katika uhifadhi.

Mada hii iliwasishwa na maofisa kutoka Mamlaka ya Usimamizi Wanyamapori Tanzania [TAWA] P. Marina na R. Komba, huku Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Ilvin Mugeta akiwa msimamizi wa majadiliano.

Kundi la tatu limehusisha Mahakimu wa ngazi mbalimbali wanaohudumu kuanzia Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo. Wajumbe hawa wamepitishwa kwenye mada kuhusu umuhimu wa misitu na changamoto za uhifadhi.

Mada hiyo iliwasilishwa na David Mungo’ong’o na Dkt. Zainabu Bungwa kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania [TFS], huku Hakimu Mkazi Mkuu na Mkurugenzi wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto [IJA], Mhe. Dkt. Particia Kisinda, akiwa msimamizi mkuu wa majadiliano.

Baadaye mchana, wajumbe wa Mkutano huo walikusanyika pamoja na kupitishwa kwenye mada nyingine inayohusu uendeshaji wa mifuko ya kijamii, fursa, changamoto na mustakabali wake.

Watoa mada walikuwa  Bw. Cosmas Sasi, Bw. James Oigo na Bw. Geofrey Sirika, huku Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Berke Sehel akiwa msimamizi mkuu wakati wa majadiliano.

Jana tarehe 13 Januari, 2026, wanachama wa TJMA walipitishwa kwenye mada tatu, ikiwemo inayohusu jukumu la Mahakama huru katika utoaji haki. Mada hii iliwasilishwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Deo Nangela, huku Amidi wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija akiwa msimamizi mkuu wa majadiliano.

Mada hiyo ilichangiwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Ferdinand Wambali, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Rose Ebrahim na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha, Mhe. Joyce Mkhoi.

Nyingine ilihusu uelewa wa miamala na bidhaa mbalimbali; changamoto zinazotolewa na sekta ya benki na fedha nchini [nafasi ya Majaji, Wasajili na Mahakimu]. Mtoa mada hii alikuwa Bw. Godwin Ngilimi, huku Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Shaban Lila akiwa msimamizi wa majadiliano.

Mada nyingine ilihusu bidhaa ya miamala, changamoto na namna ya kuzishughulikia; mikopo kwa ujumla wake, miamala ya biashara za kimataifa, dhamana mbalimbali za kibenki, uwekezaji katika dhamana na hati fungani na changamoto katika utekelezaji wa amri za Mahakama.

Watoa mada kwenye maeneo hayo walikuwa Bw. Frank Mukoyogo, Bw. Prosper Mwangamila, Bw. Xavery Makwi, Bi. Juliana Kombe na Bw. Paschal Mihayo. Msimamizi wa majadiliano alikuwa Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, alihudhuria uwasilishaji wa mada hizo katika siku ya kwanza baada ya ufunguzi wa Mkutano huo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alifungua Mkutano huo na kuwapongeza Mahakimu na Majaji kwa kazi nzuri wanazozifanya za kuwahudumia wananchi kwenye muktadha mzima wa utoaji haki nchini.

Awali, akizungumza wakati akiwakarisha wanachama kwenye Mkutano huo, Rais wa TMJA, Mhe. Elimo Masawe, alisema kuwa mustakabali wa haki nchini unategemea umoja, maadili na weledi, hivyo Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania kina nafasi muhimu katika kulinda na kuendeleza mhimili wa mahakama.

Mhe. Masawe alieleza kuwa chama hicho ni jukwaa muhimu la kitaaluma linalowaunganisha Majaji na Mahakimu, hivyo kinapaswa kuendelea kuwa sauti ya kulinda uhuru wa Mahakama, hadhi ya Majaji na Mahakimu pamoja na maslahi yao ya kitaaluma na kiustawi.

Alihimiza wanachama wapatao 1,200 waliohudhuria Mkutano huo, na wale ambao hawakupata nafasi kwa sababu mbalimbali, kuzingatia misingi ya haki, uadilifu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Mkutano Mkuu wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania unaendelea kuwa jukwaa muhimu la kutathmini mwenendo wa haki nchini na kuweka mikakati ya kuimarisha taaluma na maadili kwa maslahi mapana ya Taifa.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju [katikati waliokaa] akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watoa mada na wasimamizi wa majadiliano katika Mkutano wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania.

Hakimu Mkazi Mkuu na Mkurugenzi wa Mafunzo wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto [IJA], Mhe. Dkt. Particia Kisinda, akiongoza moja ya jopo wakati wa kuwasilisha mada mbalimbali kwenye Mkutano wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania.

Sehemu ya wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [juu na chini] wakiwa kwenye siku ya pili ya Mkutano Mkuu wa chama hicho.


Sehemu nyingine ya wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [juu na chini] wakiwa kwenye siku ya pili ya Mkutano Mkuu wa chama hicho.


Sehemu nyingine ya tatu ya wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [juu na chini] wakiwa kwenye siku ya pili ya Mkutano Mkuu wa chama hicho.


Sehemu nyingine ya nne ya wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [juu na chini] wakiwa kwenye siku ya pili ya Mkutano Mkuu wa chama hicho.


Sehemu ya nyingine ya tano ya wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [juu na picha mbili chini] ikifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa uwasilishaji wa mada mbalimbali.



Sehemu ya wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [juu na chini] wakichangia mada zilizokuwa zinawasilishwa.



 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni