Alhamisi, 15 Januari 2026

MKUTANO MKUU WA MWAKA TMJA WAHITIMISHWA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [TMJA], uliokuwa unafanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania [Judiciary Square] jijini Dodoma kwa muda wa siku tatu, umehitimishwa leo tarehe 15 Januari, 2026.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, amehitimisha Mkutano huo na kuwashukuru Wanachama waliohamasika kufika Dodoma na kukaa kwa gharama zao. ‘Nimefurahishwa sana na hali hii ya kujitoa kwenu, na huu ndio uzalendo wa ndani katika kusimamia mambo ya Chama na pia ya kitaifa,’ amesema.

Mhe. Masaju ametumia fursa hiyo pia kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kufungua Mkutano huo na kwa maelekezo muhimu yanayohusu uimarishaji wa uhuru wa Mahakama na kuifanya Mahakama kuwa yenye hadhi duniani.

Aidha, Jaji Mkuu alimshukuru Rais Samia kwa utayari wa Serikali kufanyia kazi ushauri wao katika masuala kadhaa yaliyowasilishwa kwake kama alivyoelekeza katika hotuba yake ya ufunguzi na kama inavyodhihirishwa katika taarifa kwa vyombo vya Umma ilivyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu tarehe 13 Januari, 2026.

Hafla ya kufunga Mkutano huo imehudhuriwa na Viongozi wengine wa Mahakama, akiwemo Amidi wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Augustine Mwarija pamoja na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Kabla ya hafla hiyo, Jaji Mkuu, Jaji Kiongozi, Rais wa TMJA, Mhe. Elimo Masawe na Viongozi wengine wa Chama hicho walishiriki kwenye zoezi la upandaji miti katika moja ya eneo linalozunguka jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, kama ishara ya kutunza mazingira.

Wakati wa Mkutano huo, wanachama wa TMJA walipitishwa kwenye mada kadhaa na wawezeshaji wabobezi ili kuwajengea uelewa kwenye maeneo mbalimbali.

Mada hizo ni jukumu la Mahakama huru katika utoaji haki; uelewa wa miamala na bidhaa mbalimbali; changamoto zinazotolewa na sekta ya benki na fedha nchini [nafasi ya Majaji, Wasajili na Mahakimu].

Nyingine ni mafanikio, changamoto na mustakabali wa ulinzi wa wanyamapori Tanzania; dhana ya uhifadhi-Mamlaka Ngorongoro; mafanikio, fursa na changamoto; mchango wa utalii kwenye uchumi na maendeleo ya nchi; uhifadhi endelevu wa rasilimali ya wanyamapori na mchango wa Mahakama katika uhifadhi.

Wajumbe wa Mkutano pia katika makundi mbalimbali walipitishwa kwenye mada inayohusu umuhimu wa misitu na changamoto za uhifadhi na uendeshaji wa mifuko ya kijamii, fursa, changamoto na mustakabali wake.

Mada nyingine zilihusu bidhaa ya miamala, changamoto na namna ya kuzishughulikia na mikopo kwa ujumla wake, miamala ya biashara za kimataifa, dhamana mbalimbali za kibenki, uwekezaji katika dhamana na hati fungani na changamoto katika utekelezaji wa amri za Mahakama.

Kabla ya kuhitimishwa Mkutano huo, wajumbe pia walipitishwa kwenye mada zinazohusu dhana ya kodi kwa ujumla; usikilizaji wa migogoro ya kodi na dhana ya kodi kidijitali na maendeleo ya mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano [TEHAMA] katika usimamizi wa kodi.

Watoa mada kwenye maeneo hayo walikuwa Mhe. Dkt. Deo Nangela, Bw. Joachim Tesha, Bw. Usaje Mwambene, Bw. July Lyimo Bw. Frank Mukoyogo, Bw. Prosper Mwangamila, Bw. Xavery Makwi, Bi. Juliana Kombe na Bw. Paschal Mihayo.

Wengine ni Bw. Godwin Ngilimi, Bw. Frank Mukoyogo, Bw. Prosper Mwangamila, Bw. Xavery Makwi, Bi. Juliana Kombe, Bw. Paschal Mihayo, Bw. David Mungo’ong’o, Dkt. Zainabu Bungwa, P. Marina na R. Komba

Mkutano Mkuu wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania ni jukwaa muhimu la kutathmini mwenendo wa haki nchini na kuweka mikakati ya kuimarisha taaluma na maadili kwa maslahi mapana ya Taifa.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju [katikati] akiwa katika picha ya pamoja na wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [juu na chini] baada ya kufunga Mkutano Mkuu wa Mwaka uliofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Safu ya Uongozi ya Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania.


Sehemu ya Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [juu na chini] ikifuatilia yaliyokuwa yanajiri kwenye hafla ya kufunga Mkutano Mkuu wa Mwaka wa chama hicho.


Sehemu nyingine ya Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [juu na chini] ikifuatilia yaliyokuwa yanajiri kwenye hafla ya kufunga Mkutano Mkuu wa Mwaka wa chama hicho.


Sehemu ya ya tatu Wanachama wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania [juu na picha mbili chini] ikifuatilia yaliyokuwa yanajiri kwenye hafla ya kufunga Mkutano Mkuu wa Mwaka wa chama hicho.



Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akipanda mti kwenye moja ya maeneo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania kama ishara ya kutunza mazingira.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustpher Mohamed Siyani akipanda mti kwenye moja ya maeneo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania kama ishara ya kutunza mazingira.


Rais wa Chama cha Mahakimu na Majaji, Mhe. Elimo Masawe akipanda mti kwenye moja ya maeneo ya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania kama ishara ya kutunza mazingira.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni