Jumamosi, 7 Februari 2026

MAHAKAMA KUU MBEYA YAADHIMISHA SIKU YA SHERIA NCHINI

Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, amewaongoza watumishi wa Mahakama Kuu ya Kanda hiyo pamoja na wananchi wa Mbeya katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini kwa mwaka 2026.

Mhe. Tiganga, ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika maadhimisho hayo, aliambatana na Mgeni Maalum, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomoni Itunda, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Wakili Beno Marisa. Sherehe hizo zilifanyika tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya.

Akitoa salamu za Mkuu wa Mkoa, Mgeni Maalum ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomoni Itunda, aliipongeza Mahakama Kuu ya Mbeya kwa maandalizi mazuri ya maadhimisho hayo. Aidha, aliwahimiza watumishi wa Mahakama kuendelea kusimamia utoaji wa haki kwa wakati na kwa wote, akisisitiza kuwa kufanya hivyo ni kujiwekea hazina ya kudumu mbinguni mbele ya Mwenyezi Mungu.

Kwa upande wake, Mgeni Rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, katika hotuba yake alieleza kuhusu maboresho ya kanuni ngumu yaliyofanywa na Mahakama ya Tanzania kwa lengo la kurahisisha wananchi kupata huduma za Mahakama na kufanikisha upatikanaji wa haki kwa wote kwa wakati.

Mhe. Tiganga aliongeza kuwa Mahakama ina mpango wa kuimarisha na kuongeza matumizi ya mifumo ya TEHAMA ili kurahisisha utoaji wa haki kwa wakati, kupunguza muda wa wananchi kukaa Mahakamani, na kuwezesha usikilizwaji wa mashauri kwa njia ya mtandao pale inapowezekana. Aidha, aliwahabarisha wadau na watumishi wa Mahakama kuwa, kutokana na maboresho hayo, Mheshimiwa Jaji Mkuu anasisitiza kuwa dira ya Mahakama kwa sasa ni “Utoaji wa haki kwa wote na kwa wakati zaidi iwezekanavyo.”

Kwa upande wao, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Mawakili wa Kujitegemea, wote walisisitiza kuwa kaulimbiu ya Siku ya Sheria kwa mwaka 2026 inaakisi ukweli kwamba hakuna maendeleo ya kweli bila kuzingatia misingi ya haki, usawa na uadilifu katika jamii.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na watumishi wa Mahakama, viongozi wa dini na jadi, pamoja na wadau kutoka taasisi mbalimbali wakiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mbeya, Mawakili wa Kujitegemea, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ofisi ya Ustawi wa Jamii Mbeya, Jeshi la Polisi, Idara ya Uhamiaji, na wananchi kwa ujumla.

Mgeni Rasmi na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, akisoma hotuba katika maadhimisho ya Siku ya Sheria Mahakama Kuu Mbeya.

Meza Kuu wakiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Mbeya.

Watumishi na wadau mbalimbali waliokaa mbele ni Mahakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya na Mahakama ya Wilaya, wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya.

Kwaya ya Mahakama Mbeya ikitumbuiza wakati wa maadhimisho hayo.

Mgeni Rasmi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, akikagua gwaride maalum la kuashiria kuanza kwa mpya wa kimahakama 2026.


Mgeni Rasmi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, akikagua gwaride maalum la kuashiria kuanza kwa mpya wa kimahakama 2026.

Meza Kuu ikiongozwa na Mgeni Rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Tiganga (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa Mahakama na Serikali, (wa kwanza kushoto) ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Mussa Pomo, (wa pili kushoto) ni Heshima, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomoni Itunda (wa kwanza kulia) ni Wakili wa Serikali Mkuu, Bw. Iddi Mgeni na (wa pili kulia) ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa.

Mgeni Rasmi ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Mbeya, Wengine (kutoka kushoto walioketi) ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Mussa Pomo, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomoni Itunda (wa pili kushoto), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, Mhe. Victoria Nongwa (wa pili kulia) na Wakili wa Serikali Mkuu kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mbeya. 

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni