Jumanne, 12 Desemba 2017

MAHAKAMA KUU TANGA YAANZISHA MFUMO WA UPATIKANAJI WA MAJALADA KIELEKTRONIKI

Mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Tanga imefanikiwa kuanzisha mfumo wa kielectroniki utakaorahisisha upatikanaji wa majalada pindi yanapotafutwa mahali yanapoifadhiwa (Record centre).

Mfumo huu utasaidia kuboresha huduma zinazotolewa na Mahakama hiyo hasa pale wateja wanapofika na kuhitaji taarifa mbalimbali zinazohusu kesi zao kama vile nakala za hukumu. Kupitia Mfumo huu hivi sasa wateja wanapata nakala za hukumu kwa wakati.

Katika kufanikisha zoezi hili, Mahakama Kuu kanda ya Tanga iliandaa kikosi kazi maalumu na kuwapatia mafunzo kupitia Afisa Tehama wa Kanda hiyo Bi.Amina Ahamad  ambao baada ya mafunzo hayo walisajili majalada kwenye mfumo huo mpya wa kielektroniki.
Afisa Tehama Kanda ya Tanga Bi. Amina Ahmad (kulia) akitoa maelekezo ya kusajili majalada kwa Mfumo wa Kielectroniki kwa Msaidizi wa kumbukumbu,
 Alex Kamwaya.
Tayari zoezi hilo la kusajili majalada limekamilika kwa Mahakama Kuu na Mahakama ya Hakimu Mkazi Tanga. Hivi sasa kikosi maalum cha kutoa mafunzo kinaendelea kutoa mafunzo katika wilaya zote za mkoa huo ili kuhakikisha wilaya zote za wilaya zinaanza kutumia mfumo huo. 

Wakati huo huo, Naibu Msajili wa kanda hiyo Mhe. Adrian Kilimi amesema kanda yake imejipanga kutokuwa na mlundikano wa mashauri. Alisema hivi sasa Mahakama Kuu kanda ya Tanga haina mashauri ambayo ni ya mlundikano.

Katika kuhakikisha hakuna mashauri ya Mlundikano, Naibu Msajili huyo anaeleza kuwa kila mwezi wamekuwa wakiainisha mashauri yote kwa kuonyesha muda uliobaki kufikia mlundikano na hii inakuwa ni alama ya kufanya kazi kama timu katika kanda kwa kushirikiana na wadau ili kuyamaliza kwa wakati.

Baadhi ya watumishi walioshiriki kwenye zoezi la usajili wa majalada kwa Mfumo wakipanga makasha yenye Majalada.
 Msajili wa Mahakama Kuu Mhe. Adrian Kilimi (aliyesimama katikati) akimuelezea Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Tanga Mhe. Iman Aboud (kulia) jinsi kikosi kazi kilivyofanikisha kuingiza majalada kwenye mfumo wa utafutaji wa kielekitroniki. Kushoto ni Afisa Tehema Bi Amina Ahamad. 
 Baadhi ya watumishi walioshiriki kwenye zoezi la usajili wa majalada kwenye mfumo wa Kielekitroniki. Wa pili kulia ni Afisa Tehama Bi Amina Ahamad ambaye ndiye aliyetoa mafunzo hayo. 
 Baadhi ya watumishi walioshiriki kwenye zoezi la usajili wa majalada kwenye Mfumo wakielekitroniki.
Jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Tanga.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni