Ijumaa, 17 Januari 2020

BODI YA UDHAMINI WA TAARIFA ZA MAJUZUU YAANZA KIKAO


Na Magreth Kinabo na Innocent Kansha- Mahakama

Bodi ya Udhamini wa Taarifa ya Majuzuu ya Sheria leo imeanza kikao chake  cha siku mbili cha kuchambua maamuzi ya Mahakama Kuu  na  Mahakama ya Rufani Tanzania kwa ajili ya kumaliza kuandaa  Juzuu la Taarifa za Sheria la mwaka 2018.

Aidha bodi hiyo pia itaandaa  maamuzi kwa ajili ya Juzuu la Taarifa za Sheria la mwaka 2019.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, kinachofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Shule ya Sheria kwa Vitendo, iliyopo Barabara ya Sam Nujoma, jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Jacobs Mwambegele alisema kikao hicho ni cha mara ya kwanza kufanyika katika kipindi cha mwaka huu.

‘Bodi imekutana ikiwa tayari imekwisha andaa Taarifa za Majuzuu ya Sheria ya Mwaka 2007 hadi Mwaka 2013 na kukabidhi Taarifa hizo katika uongozi wa juu wa Mahakama ili kuwezesha kupata Taarifa kamili katika nakala laini na ngumu,’ alisema Mhe. Mwambegele.

Aliongeza kuwa, tayari Bodi hiyo imekamilisha kupitisha maamuzi kwa ajili ya vitabu vya Mwaka 2014 hadi Mwaka 2017.

Jaji Mwambegele alifafanua kuwa Bodi hiyo, kwa sasa inafanya kazi zake kwa njia ya teknolojia zaidi kwa kushirikiana na Idara ya Menenjimenti ya Mashauri ya Mahakama ya Tanzania, ambayo hupokea maamuzi ya Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani (Depository) katika nakala laini kila mwezi na kuishushia Bodi ambayo huyachakata na kuyachambua maamuzi hayo ili kupata maamuzi ambayo yanakuwa na sifa ya kutolewa Taarifa.

Alisema katika kipindi  cha mwaka 2020 Bodi  hiyo, imejipanga kumaliza kuchambua maamuzi kwa ajili ya Kitabu cha Mwaka 2018, 2019 na 2020 ili kuendana na wakati ili  kufikia hatua ya kutoa Taarifa kwa awamu mbili hadi nne katika kila mwaka kuanzia mwaka wa fedha 2020/2021.

Mwenyekiti huyo  alisisitiza kwamba hatua ijayo ya kutoa taarifa za majuzuu kwa awamu inatokana na uwezo mkubwa wa Bodi wa sasa wa kupokea maamuzi mengi kwa njia ya teknolojia.

Bodi hiyo kwa  sasa inafikiwa na Maamuzi ya Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani 3,000  hadi  4,500 kwa uwiano wa maamuzi 300 hadi 400 kwa mwezi kabla ya uchambuzi.

Maamuzi yote yatakayopitiwa na Bodi yatakabidhiwa kwa mzabuni atakaeandaa Taarifa za Majuzuu ya Sheria kwa nakala laini na ngumu. Nakala laini zitawekwa katika mifumo ya kupandisha taarifa za Sheria ya Mahakama ya Tanzania kwa rejea rahisi na nakala ngumu kusambazwa kwa wadau na Taasisi.

Akizungumzia kuhusu faida ya Majuzuu hayo ya Taarifa za Sheria, alisema  husaidia wadau kufuata Maamuzi ya Mahakama za Juu katika kutafuta haki zao na pia Mahakama za chini kufuata misingi ya kisheria iliyowekwa na maamuzi ya Mahakama za Juu.

Faida nyingine za taarifa za majuzuu hayo ni kusaidia Mahakama za Juu kutotofatiana katika misingi ya kisheria (Conflicting Decisions) na kufuata misingi na taratibu za Maamuzi iliyojiwekea.

‘Taarifa hizi za majuzuu ya sheria husaidia pia  katika kuendeleza ufahamu wa kisheria mfano,Ofisi za Mawakili, Taasisi za Elimu ya Sheria, Magereza, Mashirika ya Misaada ya Sheria na Taasisi na Idara Mbalimbali za Sheria, alisisitiza.

Bodi hiyo ina wajumbe 12, ambao ni Majaji kutoka Mahakama ya Rufani, Majaji wa Mahakama Kuu kwa upande wa Bara na Zanzibar, wawakili wa Ofisi ya  Mwanasheria Mkuu wa Serikali wa pande zote mbili. Wajumbe wengine wawakilishi kutoka wanasheria binafsi wa pande hizo,   

Bodi  hiyo hufanya vikao vyake  mara nne kwa mwaka.


Mwenyekiti wa Bodi ya Udhamini  ya Taarifa ya Majuzuu ya Sheria,ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Jacobs Mwambegele (kushoto)  akisisitiza jambo kwenye   kikao hicho.Kulia ni Katibu wa Bodi hiyo, Profesa Hamudi  Majamba.


Baadhi ya wajumbe wakifuatilia kikao hicho.



                       Baadhi ya wajumbe wakifuatilia kikao hicho.



 Baadhi ya wajumbe Bodi ya Udhamini wa Taarifa ya Majuzuu ya Sheria      wakiendelea  na kikao katika ukumbi wa mikutano wa Shule ya Sheria kwa Vitendo, iliyopo Barabara ya Sam Nujoma, jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya wajumbe Bodi ya Udhamini wa Taarifa ya Majuzuu ya Sheria      wakiwa  katika picha   ya pamoja  kwenye  ukumbi wa mikutano wa Shule ya Sheria kwa Vitendo, iliyopo Barabara ya Sam Nujoma, jijini Dar es Salaam.Waliokaa  katikati Mwenyekiti wa Bodi ya Udhamini  ya Taarifa ya Majuzuu ya Sheria,ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Jacobs Mwambegele na wa kwanza kushoto waliosimama ni Kaimu Mratibu wa Bodi hiyo, Mhe. Kifungu Mrisho.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni