Jumanne, 9 Februari 2021

WAZIRI WA HABARI AIPONGEZA MAHAKAMA KWA MABORESHO

 ·      Viongozi wa Serikali wakumbushwa kutekeleza agizo la Rais la kutokalia taarifa

Na Lydia Churi- Mahakama, Morogoro

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Innocent Bashungwa ameipongeza Mahakama ya Tanzania kutokana na maboresho mbalimbali iliyofanya na inayoendelea kufanya katika huduma zake.

Waziri Bashungwa ameyasema hayo leo alipokuwa akizungumza na Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano wa Taasisi mbalimbali za Serikali alipokuwa akifungua Mkutano wa mwaka wa waandaaji wa vipindi vya Redio na Televisheni ulioandaliwa na Shirika la Utangazaji Tanzania TBC mjini Morogoro.

“Mahakama ya Tanzania inafanya kazi nzuri sana ya kuboresha huduma zake na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora”, alisema Waziri Bashungwa.

Alisema hivi sasa wananchi wanashuhudia huduma zikisogezwa karibu zaidi ambapo majengo ya Mahakama yamekuwa yakiendelea kujengwa katika maeneo mblimbli nchini hatua inayomfanya kuupongeza Mhimili huo kwa maboresho hayo.

Waziri wa Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo pia amelipongeza shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kwa kuwakutanisha Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano wa Taasisi za Serikali ikiwemo Mahakama ya Tanzania ili kupata mafunzo yatakayosaidia kuboresha namna ya utangazaji wa shughuli za serikali.

“Serikali inawathamini Maafisa Mawasiliano kwa kuwa ni daraja muhimu sana kati yake na wananchi, hivyo tumieni elimu na weledi wenu kufikisha ajenda muhimu za serikali kwa wananchi ukiwemo Mpango wa Taifa wa maendeleo wa miaka mitano ili wananchi waufahamu vizuri”, alisema.

Naye Katibu Mkuu wa wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbas amewakumbusha viongozi wa Serikali kutekeleza maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli aliyoyatoa Juni 4 mwaka jana ambapo aliwataka viongozi hao kuhakikisha shughuli za Serikali zinatangazwa.

Akitoa mada kwenye Mkutano wa waandaaji wa vipindi vya Redio na Televisheni, Dkt. Abbas Serikali katika kipindi cha pili cha serikali ya awamu ya tano, itafanya tathmini ya utoaji wa taarifa za serikali kwa Viongozi wa Taasisi pamoja na Maafisa Mawasiliano kwani wako watendaji wakuu wa Taasisis ambao ni kikwazo katika utoaji wa taarifa zinazohusu utekelezaji wa shughuli za serikali.

Aidha, Katibu Mkuu huyo na Msemaji wa Serikali amezitaka Taasisi za Serikali kutoa taarifa sahihi na kwa wakati ili wananchi wafahamu shughuli mbalimbali pamoja na mafanikio ya Serikali yao.

Alisema hivi sasa hali ya utoaji wa taarifa za serikali ni nzuri hivyo amewataka Maafisa Mawasiliano wa Serikali kuongeza juhudi, vifaa na kuwa wabunifu ili waweze  kuandaa na kutoa habari zilizofanyiwa utafiti wa kutosha, zenye  takwimu na zinazoonesha Ushahidi wa maendeleo yaliyofikiwa.

Mkutano wa 104 wa waandaaji wa vipindi vya Redio na Televisheni ulioandaliwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) unahudhuriwa na Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano Zaidi ya 80 kutoka Taasisi mbalimbali za Serikali mjini Morogoro.  TBC ilianza kuandaa mikutano ya aina hii tangu miaka ya 1980’s.


Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Innocent Bashungwa 

Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano kutoka Taasisi za Serikali wakiwa kwenye Mkutano wa Mwaka wa waandaji wa vipindi vya Redio na Televisheni ulioandaliwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) mjini Morogoro. Mkutano huo ulifunguliwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Innocent Bashungwa leo. 

Katibu Mkuu wa wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbas akitoa mada kwenye Mkutano huo.

 Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano kutoka Taasisi za Serikali wakiwa kwenye Mkutano huo.
Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano kutoka Taasisi za Serikali wakiwa kwenye Mkutano huo.

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni