Jumanne, 16 Machi 2021

KITUO MAALUM KUSHUGHULIKIA MASHAURI YA MIRATHI NA FAMILIA KUANZISHWA JIJINI DAR ES SALAAM

Na Lydia Churi-Mahakama

Mahakama ya Tanzania inatarajia kuanzisha kituo Maalum kitakachoshughulikia mashauri yanayohusu mirathi na masuala ya kifamilia (ndoa na talaka) kwa lengo la kusogeza na kurahisisha utoaji wa huduma za kimahakama kwa wananchi.

Akiwasilisha mada mbele ya wajumbe wa Kamati ya kudumu ya bunge ya katiba na Sheria, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Messeka Chaba aliwaambia wajumbe hao kuwa kituo hicho kinajengwa wilayani Temeke jijini Dar es salaam na ujenzi wa jengo hilo uko katika hatua za ukamilishwaji.

Kwa mujibu wa Mhe. Chaba, Mahakama imeamua kuanzisha kituo hicho maalum (One Stop Centre) kufuatia kuwepo kwa idadi kubwa ya mashauri yanayohusiana na masuala ya Mirathi, Ndoa na Talaka. Utafiti uliofanywa na Mahakama katika mwaka wa fedha wa 2017/2018 ulionesha kuwa kulikuwa na jumla ya mashauri 5072 yanayohusu masuala hayo ambapo mashauri ya mirathi pekee yalikuwa ni 3474 na familia 1598 katika Mkoa wa Da es Salaam.

Alisema huduma hiyo itaanza mara baada ya taratibu za kisheria kukamilika na kutangazwa rasmi na mamlaka husika. Aidha, mchakato wa kuandaa kanuni (Rules) ikiwa ni pamoja na kanuni za uendeshaji wa kituo hicho (The One Stop Centre Operationalization Rules, 2021) sambamba na Mwongozo wa utendaji kazi (Operational Manual for One Stop Centre) tayari zimeandaliwa na zinafanyiwa kazi.

 

Mhe. Chaba alizitaja faida za kuanzishwa kwa kituo hicho kuwa ni kupatikana kwa huduma ya kusikiliza na kutoa uamuzi katika mashauri ya mirathi, ndoa na talaka na usimamizi wa mali za marehemu ndani ya siku saba (7) na kusaidia kuwaleta pamoja wadau wa haki ndani ya jengo moja wakiwemo ofisi ya Mwanansheria mKuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Mawakili wa kujitegemea, watoa msaada wa kisheria, watendaji wa madhehebu ya dini na ustawi wa jamii.


Alisema Mahakama za Mwanzo na Wilaya zitakuwa na mamlaka ya kusikiliza mashauri ya mirathi, ndoa na talaka katika kituo hiki katika mkoa mzima wa Dar es salaam. Aliongeza kuwa hatua hii itachochea kuifikia haki kwa haraka na wakati.

Faida nyingine zitakazotokana na kuanzishwa kwa kituo hiki ni kuokoa muda na  kupunguza gharama za uendeshaji wa mashauri kwa wadaawa, pamoja gharama za kutafuta Mawakili na watoa msaada wa kisheria.

Kuanzishwa kwa kituo hicho pia kutapunguza ucheleweshaji wa kumalizika kwa mashauri ya ndoa, talaka, mirathi na usimamizi wa mali za marehemu na kutoa hamasa na kupanua wigo wa matumizi ya rasilimali katika uendeshaji wa mashauri ya aina hii.

Mahakama ya Tanzania kupitia Mpango Mkakati wake wa miaka mitano (2015/16 - 2019/20) unaokwenda sambamba na Dira ya Taifa ya Maendeleo (2025) iliweka malengo ya kujenga majengo ya Mahakama ambayo yatatumika kama Vituo Jumuishi vya Utoaji haki (Intergrated Justice Centre) kwa lengo la kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi na kurahisisha utoaji haki. Katika kuhakikisha haki  inapatikana kwa wakati, Mahakama iliona umuhimu wa kuanzisha kituo kimoja Jumuishi cha Utoaji Haki (One Stop Centre) kitakachoshughulikia mashauri ya mirathi na familia.

Kituo kimoja Jumuishi cha Utoaji Haki ni jengo maalum lililobuniwa na kujengwa kwa ajili ya kutoa huduma zote za usikilizwaji wa mashauri ya familia, mirathi, ndoa na usimamizi wa mali za marehemu. Kituo hiki kitajumuisha ngazi za Mahakama ya Mwanzo, Wilaya, Hakimu Mkazi na Mahakama Kuu pamoja na ofisi za wadau wote muhimu wanaoshughulika na mashauri ya aina hii kukaa ndani ya jengo moja ili kutekeleza majukumu yao ya utoaji haki.

 

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba akisikiliza hoja za wajumbe  wa Kamati ya kudumu ya bunge ya katiba na Sheria walipokutana na ujumbe wa  Mahakama ya Tanzania. Kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Bw. Mathias Kabunduguru na kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Najma Murtaza Giga. 
Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Messeka Chaba akiwasilisha Mada kuhusu uanzishwaji wa Kituo Kimoja Jumuishi cha Utoaji Haki (One Stop Centre) kitakachoshughulikia Mirathi na masuala ya familia mbele ya wajumbe  wa Kamati ya kudumu ya bunge ya katiba na Sheria walipokutana na ujumbe wa  Mahakama ya Tanzania. 
Baadhi ya wajumbe wa kamati ya kudumu ya bunge ya Katiba na Sheria wakifuatilia mada walipokutana na ujumbe wa  Mahakama ya Tanzania. 



 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni