Ijumaa, 16 Aprili 2021

SHIRIKIANENI NA MAHAKAMA ILI KUIFIKISHA KWENYE AZMA YA KUTOA HAKI KWA WAKATI: JAJI MKUU

 Na Lydia Churi-Mahakama, Arusha

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewaomba wadau wa Mahakama kushirikiakiana na Mhimili huo ili kusaidia kuufikisha kwenye azma yake ya kutoa haki kwa wakati.

Akifungua Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na wadau mkoani Arusha, Jaji Mkuu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume hiyo amesema mchango wa wadau ni nguzo muhimu katika mafanikio ya Mahakama hivyo amewaomba kushirikiana kwa dhati na Mahakama ili kuwezesha Mhimili huo kutekeleza jukumu lake la msingi la kutoa haki kwa wakati.

“Ushirikishwaji wa wadau ni jambo muhimu na Mahakama inalizingatia hilo ili kuweza kutekeleza majukumu yake ya upatikanaji wa haki kwa urahisi”, alisema Jaji Mkuu.

Baadhi ya wadau wa Mahakama ni pamoja na Polisi, Magereza, Uhamiaji, Takukuru, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Mkemia Mkuu, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea.

Aidha, Jaji Mkuu alisema Mahakama imesimamia nguzo tatu muhimu katika kutekeleza jukumu lake la msingi ambapo kupitia nguzo ya kwanza imeweza kujibadilisha na kufuata utawala bora, uwajibikaji na usimamizi wa rasilimali ili shughuli za utoaji ziwe endelevu.

Alisema kupitia nguzo ya pili ya Mpango Mkakati wake wa miaka mitano, Mahakama imejipanga kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati. Aliongeza kuwa nguzo ya tatu ya Mpango huo ni kuimarisha imani ya wananchi kuhusu Mahakama yao na mifumo ya utoaji haki.

“Ili tuweze kutoa haki kwa wakati, imani ya wananchi ni jambo la muhimu na tunalitathmini sana, wananchi ni chimbuko la mamlaka zote yaani Serikali, Bunge na Mahakama”, alisisitiza.

Naye Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Eliezer Feleshi akielezea matarajio ya Mahakama kwa wadau alisema Mahakama inapenda kuona wapelelezi wakitumia njia za kisayansi katika kufanya kazi yao na kuondokana na upelelezi wa kimazoea. Alitoa mfano wa matumizi ya vipimo vya DNA katika mashauri ya jinai na kuongeza kuwa Sheria inaruhusu matumizi hayo.

Jaji Kiongozi alisema wapelelezi hawana budi kushirikiana na Mahakama ili kukamilisha upelelezi wa mashauri kwa haraka na inatarajia kuona matumizi ya adhabu mbadala kwenye makosa ya jinai mepesi ili kupunguza msongamano wa wafungwa na mahabusu magerezani.

Aidha, Jaji Kiongozi alisema suala la Maafisa Ustawi wa Jamii kuwepo mahakamani hasa kwenye mashauri yanayohusu Watoto ni muhimu na amesisitiza suala hili kwa kuwa hivi sasa halifanyiki kwa kiwango kinachotakiwa.

Kuhusu uhusiano wa Mahakama na wadau wake, Dkt. Feleshi amesema ni mzuri na hauna budi kuendelezwa. Aliongeza kuwa kwa wale wadau wasiotimiza wajibu wao ipasavyo, Mahakama itaendelea kuwaweka hadharani ili Umma na wale wanaotafuta haki waweze kuwabaini.  

Tume ya Utumishi wa Mahakama inaendelea na ziara katika Mikoa ya Arusha na Manyara kwa lengo la kuitangaza na kutoa elimu kwa wadau wa Mahakama wakiwemo wajumbe wa kamati za Maadili za Mikoa na Wilaya zinazowajumuisha wakuu wa Mikoa na wakuu wa Wilaya.


Baadhi ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Arusha waliohudhuria Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na Watumishi hao uliofanyika kwenye ukumbi wa Hazina Ndogo mkoani Arusha jana.

Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha wakiwa kwenye Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na Watumishi wa kanda hiyo jana mkoani Arusha. Kushoto ni Mhe. Mohamed Gwae na kulia ni Mhe. Robert Kassim.  
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Eliezer Feleshi (kushoto) na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Bw. Mathias Kabunduguru wakiwa kwenye Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na wadau mkoani Arusha,
Baadhi ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Arusha waliohudhuria Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na Watumishi hao uliofanyika kwenye ukumbi wa Hazina Ndogo mkoani Arusha jana.

Baadhi ya Watumishi wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Arusha waliohudhuria Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na Watumishi hao uliofanyika kwenye ukumbi wa Hazina Ndogo mkoani Arusha jana.


Wadau wa Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye Mkutano kati yao na Tume ya Utumishi wa Mahakama uliofanyika jana katika ukumbi wa Hazina Ndogo mkoani Arusha jana.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni