Jumamosi, 17 Aprili 2021

WAJIBIKENI KATIKA MAENEO YENU YA KAZI; KABUNDUGURU

Na Mary Gwera, Mahakama

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Mathias Kabunduguru ametoa rai kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama nchini kuendelea kuwajibika ipasavyo katika maeneo yao ya kazi ikiwa ni pamoja na kuwa na usimamizi thabiti wa bajeti ili kufanikisha mipango mbalimbali ya Mahakama inayolenga kuboresha huduma ya utoaji haki nchini.

Akifunga rasmi Mafunzo Elekezi ya Utunzaji Kumbukumbu kwa Watendaji hao leo Aprili 17, 2021 katika Chuo cha Mipango jijini Dodoma, Mtendaji Mkuu aliwahakikishia washiriki hao kuwa katika kutekeleza shughuli mbalimbali bajeti ya Mahakama ya mwaka wa fedha wa 2021/2022 imezingatia mahitaji muhimu ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao ya utoaji haki kwa wananchi.

“Ni matumaini yangu mtaongeza bidii na kujitoa zaidi na zaidi ili kufanikisha majukumu ya kuhakikisha kuwa huduma za Mahakama zinapatikana kwa wakati unaostahili kwa mujibu wa taratibu na viwango vinavyokubalika,” alisema Bw. Kabunduguru.

Aidha, Mtendaji Mkuu aliongeza kuwa pamoja na utekelezaji wa majukumu ya kimkakati aliwataka Maafisa hao wa Mahakama kuendelea  kusimamia na kuhamasisha matumizi bora ya TEHAMA kila mmoja kwa eneo lake.

“Mahakama inatarajia kuanza utekelezaji wa mpango mkakati mpya ambapo katika mkakati huo imepanga kuongeza matumizi ya huduma za ki-elektroniki kwenye shughuli za Mahakama,” alisisitiza.

Hali kadhalika, aliwakumbusha Washiriki wa Mafunzo hayo kuendelea kusimamia miongozo inayotolewa na Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) ili kuwa na udhibiti bora wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA iliyopo Mahakamani.

Kwa upande wake, Msajili Mkuu Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma aliwakumbusha washiriki wa Mafunzo hayo kushirikiana katika kazi kwa kuwa wote wanajenga nyumba moja.

“Shirikianeni kutekeleza azma ya utoaji haki kwa wakati, bila kusahau kutekeleza kwa wakati maagizo yanayotolewa na Viongozi ili kusonga mbele,” alisema Mhe. Chuma.

Msajili Mkuu aliongeza kwa kuwataka Wasajili na Watendaji hao kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili watumishi walio chini yao ili kuwapa motisha ya kufanya kazi zaidi.

Katika mafunzo hayo Washiriki walipitishwa katika mada mbalimbali ikiwemo uhusiano na umuhimu uliopo baina ya utunzaji kumbukumbu, matumizi ya majalada na uandishi wa nyaraka mbalimbali, usajili wa mashauri kwa mfumo wa kielektroniki.

Nyingine ni usimamizi na ukaguzi wa Mahakama, usimamizi wa masuala ya fedha na kumbukumbu zake kupitia mfumo mpya wa ‘MUSE’ na mifumo ya ndani na usimamizi wa bajeti.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Mathias Kabunduguru akizungumza na Naibu Wasajili na Watendaji walioshiriki katika Mafunzo Elekezi ya Utunzaji kumbukumbu (hawapo pichani) alipokuwa akifunga rasmi mafunzo hayo  yaliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mipango jijini Dodoma.
Baadhi ya Washiriki wa Mafunzo hayo wakimsikiliza Mhe. Mgeni rasmi.
Msajili Mkuu, Mahakama ya Tanzania akizungumza jambo na washiriki wakati wa hafla fupi ya kufunga mafunzo hayo.
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha akizungumza jambo katika Mafunzo hayo.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Mathias Kabunduguru akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Naibu Wasajili walioshiriki katika mafunzo, kushoto ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma na kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw. Leonard Magacha.
Picha ya pamoja; meza kuu na Washiriki.
Picha ya pamoja na sehemu ya Watendaji wa Mahakama walioshiriki katika Mafunzo hayo.
Meza Kuu katika picha ya pamoja na sehemu ya Wawezeshaji wa Mafunzo hayo (waliosimama nyuma), wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji, Mahakama ya Tanzania, Bw. Erasmus Uisso, wa pili kushoto ni Mhasibu Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Fanuel Tiibuza, wa tatu ni Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Ndani, Bw. Anipenda Lupaya na wa kwanza kulia ni Mkurugenzi wa Kumbukumbu na Nyaraka, Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula.
Meza Kuu katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Sekretariet ya Mafunzo hayo. Aliyesimama wa kwanza kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo-Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu.













Hakuna maoni:

Chapisha Maoni