Jumanne, 20 Aprili 2021

MAHAKIMU WATAKIWA KUWA NA NIDHAMU NA KUZINGATIA MAADILI YA KAZI ZAO

 Na Lydia Churi-Mahakama, Manyara

Jaji Mkuu wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka Mahakimu wote nchini kuwa na nidhamu na kutekeleza majukumu yao ya utoaji haki kwa kuzingatia Maadili. 

Akizungumza na Watumishi wa Mahakama wakiwemo Mahakimu katika ziara ya ya Tume hiyo mkoani Manyara, Jaji Mkuu amesema majukumu ya Hakimu ni makubwa kwa jamii na kutokana na majukumu hayo jamii hufuatilia mwenendo wao hivyo amewaasa kuwa na nidhamu ya hali ya juu ili kujenga imani ya wananchi kwa Mhimili huo.

“Ukiwa na changamoto ya kutokuwa na nidhamu utatembea na rekodi yenye dosari wakati wote hivyo zingatieni suala la kuwa na nidhamu ya hali ya juu”, alisema Jaji Mkuu.

Alisema suala la Maadili ni muhimu kwa Maafisa wa Mahakama pamoja na watumishi wote wengine wa Mhakama hivyo aliwataka watumishi hao kuzisoma na kuziishi kanuni za Maadili ili kujenga taswira chanya ya Mhimili wa Mahakama. Aliongeza kuwa Tume hiyo iliandaa Kanuni za Maadili kwa Maafisa wa Mahakama zilizoanza kutumika Novemba 20, mwaka jana.

Kuhusu suala la utendaji kazi, Jaji Mkuu alisema Mahakama ya Tanzania imepewa pongezi na wadau wake kwa kutokana na kuweka vigezo vya kupima utendaji kazi na kujitathmini kwa watumishi wake hasa Majaji na Mahakimu.

“Majaji na Mahakimu wamewekewa vigezo vya kupima utendaji kazi wao ambapo kila Jaji hutakiwa kusikiliza na kumaliza mashauri 220 kwa mwaka, Hakimu wa Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya mashauri 250 kwa mwaka na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo mashauri 260 katika kipindi cha mwaka mwaka mmoja”, alifafanua Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu pia aliwapongeza watumishi wa Mahakama ya Tanzania kwa kutekeleza vema maboresho ya huduma za Mahakama kupitia Mpango Mkakati wa miaka mitano wa Mahakama (2015/16-2019/21). Alisema maboresho yaliyofanyika yameleta mabadiliko ya kimtazamo katika utoaji wa huduma na mabadiliko ya huduma zinazotolewa na Mahakama.

Alisema Mahakama imefanikiwa kutekeleza dhana ya utoaji haki unaomsikiliza na kumjali Mteja, utafiti uliofanywa na Taasisi ya Repoa, kuhusu kuridhika kwa mteja kutokana na namna Mahakama inavyotoa haki  ulionesha kuwa asilimia 57 ya wananchi walirishwa na huduma hizo mwaka 2015 na asilimia 70 waliridhishwa na huduma za Mahakama mwaka 2019”, alisema.

Tume ya Utumishi wa Mahakama imemaliza ziara katika Mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara iliyokuwa na lengo la kuitangaza na kutoa elimu kwa wadau wa Mahakama wakiwemo wajumbe wa kamati za Maadili za Mikoa na Wilaya zinazowajumuisha wakuu wa Mikoa na wakuu wa Wilaya.

Tume ya Utumishi ya Mahakama imeundwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 112 kwa lengo la kusimamia mambo muhimu yanayohusu Mhimili wa Mahakama. Wajumbe wa Tume hiyo ni pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania (Mwenyekiti), Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji moja wa Mahakama ya Rufani anayeteuliwa na Rais, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, na wajumbe wengine wawili wanaoteuliwa na Rais.

Baadhi ya kazi za Tume hiyo ni pamoja na kumshauri Mhe. Rais katika uteuzi wa Majaji wa Mahakama Kuu, kumshauri Rais kuhusu masuala ya nidhamu, mishahara na maslahi ya Majaji, na kushauri kuhusu ajira za Mahakimu na kusimamia nidhamu yao.

Jaji Mkuu wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kufika kwenye ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara kumtembelea kabla ya kuanza vikao vya Tume ya Utumishi wa Mahakama mkoani humo. kulia ni Mkuu huyo wa Mkoa Bw. Joseph Mkirikiti.
Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald Ndika (katikati) na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi (kulia) wakiwa ofisini kwa Mkuu wa Mkoa wa Manyara Bw. Joseph Mkirikiti (kushoto) wakati Jaji Mkuu alipomtembea akiwa katika ziara ya Tume ya Utumishi wa Mahakama mkoni humo.

Wadau wa Mahakama wakiwa katika Mkutano kati yao na Wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama. Waliokaa mbele ni Watumishi wa Mahakama ya Tanzania. Kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma Mhe. Ilvin Mugeta, Katikati ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Sharmila Sarwatt na kulia ni Katibu Msaidizi wa Jajimi Mkuu Mhe. Venance Mlingi.  




 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni