Jumatano, 8 Septemba 2021

KABUNDUGURU AKABIDHI RASMI OFISI KWA MRITHI WAKE

-Atoa rai kwa Watumishi wa umma kujituma kwa manufaa ya Taifa

Na Mary Gwera, Mahakama

Mtendaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Mathias Kabunduguru leo amemkabidhi rasmi Ofisi Mtendaji Mkuu mpya wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel aliyeapishwa Agosti 21, 2021 baada ya kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kushika wadhifa huo.

Akizungumza kabla ya makabidhiano hayo yaliyofanyika leo Septemba 08, 2021, Bw. Kabunduguru ametoa wito kwa Watumishi wa Mahakama na Watumishi wa umma kwa ujumla kufanya kazi kwa kujituma kwa maendeleo ya Taifa.

“Harakati za kujenga Taifa zinahitaji ushiriki wa Watumishi wake ili kufikia azma ya maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla, hivyo natoa wito kwa watumishi walioko kazini kuwajibika ipasavyo ili kujenga Taifa,” alisema.

Alisema kuwa Utumishi wa umma umelenga katika kutoa huduma kwa umma, hivyo ni muhimu watumishi kuendelea kuwahudumia vyema wananchi.

 Kwa upande wa Mahakama, Mtendaji Mkuu huyo mstaafu alimuhakikishia Mtendaji Mkuu wa Mahakama kuwa Mahakama ipo katika hali nzuri huku akimuomba kuendeleza maboresho yaliyopo na ambayo yapo kwenye michakato mbalimbali.

Naye Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Ole Gabriel alimshukuru Bw. Kabunduguru kwa mapokezi mazuri, vilevile kumpongeza kwa kazi nzuri ya kutumikia Taifa na Mahakama katika utumishi wake.

“Napenda nikushukuru Kaka yangu kwa mapokezi mazuri na zaidi ya yote nikushukuru kwa kazi nzuri kwa Mahakama, nami nikuhakikishie kuwa sikuja hapa kutengua torati bali kukamilisha torati, pale mlipoishia watangulizi wangu nami nitaendeleza,” alisema Mtendaji Mkuu.

Aliongeza pia atashughulikia yale yote aliyoelekezwa na Mhe. Rais kuhusu kuboresha maslahi ya watumishi, mirathi ikiwa ni pamoja na kuboresha mazingira ya kufanyia kazi, matumizi ya TEHAMA Mahakamani na mengineyo.

Nae Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma amemuhakikishia kumpa ushirikiano Mtendaji Mkuu wa Mahakama, vilevile amemshukuru Bw. Kabunduguru kwa utumishi wake mahakamani na kumuomba kutosita kutoa msaada kwa Mahakama pale atakapohitajika.

Prof. Elisante Ole Gabriel ni Mtendaji Mkuu wa tatu wa Mahakama ya Tanzania tangu kuanzishwa kwa nafasi hiyo ndani ya Mhimili huo kwa mujibu wa Sheria ya Uendeshaji wa Mahakama Namba 4 ya mwaka 2011. Mtendaji Mkuu wa Kwanza alikuwa ni Mhe. Balozi Hussein Athuman Kattanga (Sasa Katibu Mkuu Kiongozi) ambaye alifuatiwa na Bw. Mathias Kabunduguru ambaye amestaafu kwa mujibu wa sheria.

Aliyekuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Mathias Kabunduguru (kulia) akikabidhi nyaraka za Ofisi kwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama  ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel Ofisini kwake Mahakama ya Rufani Jijini Dar es Salaam leo Septemba 08, 2021.

Aliyekuwa Mtendaji Mkuu Mstaafu, Bw. Kabunduguru (kulia) akitoa neno wakati wa hafla fupi ya makabidhiano ya ofisi yaliyoshuhudiwa na baadhi ya Wakurugenzi na Wakuu wa Vitengo wa Mahakama pamoja na Waandishi wa Habari waliohuddhuria. Kushoto ni Prof. Elisante Ole Gabriel akimsikiliza kwa umakini.

Mtendaji Mkuu akizungumza jambo mara baada ya kukabidhiwa rasmi ofisi na Mtangulizi wake, Bw. Mathias Kabunduguru.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Martin Chuma akitoa neno la shukrani mara baada ya hafla hiyo ya makabidhiano.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania,Prof. Elisante Ole Gabriel ( aliyeketi katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi wa Menejimenti ya Mahakama mara baada ya hafla fupi ya makabidhiano ya Ofisi ya Mtendaji Mkuu, wengine ni (kulia) Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Martin Chuma na kushoto ni aliyekuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama Bw. Mathias Kabunduguru.

Mtendaji Mkuu Mstaafu, Bw. Kabunduguru (kushoto) akiagana na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Martin Chuma (kulia) mara baada ya hafla ya kukabidhi Ofisi, anayeshuhudia (katikati) ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Ole Gabriel.  

(Picha na Innocent Kansha, Mahakama)







Hakuna maoni:

Chapisha Maoni