Ijumaa, 15 Oktoba 2021

TUTAJENGA MAHAKAMA ILIYO HURU NA INAYOAMINIKA-JAJI KIONGOZI SIYANI

Na Lydia Churi na Stanslaus Makendi, Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani, amewataka watumishi wote wa Mahakama kote nchini kufanya kazi kwa uadilifu ili kujenga Mahakama iliyo huru na inayoaminika kwa Watanzania.

Mhe. Siyani alitoa wito huo hivi karibuni katika hafla fupi ya makabidhiano ya ofisi yaliyofanywa na mtangulizi wake, Mhe. Jaji Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi, katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kilichopo jijini Dodoma.

“Hili suala la uadilifu tutalisimamia kikamilifu. Yapo mambo mengi ambayo yanapaswa kufanyika ili watu wawe na imani na Mahakama na maamuzi tunayoyatoa yasiwe na mashaka,”alisema na kusisitiza kuwa ili kujenga Mahakama inayoaminika lazima iwe huru huku watumishi wote wakifanya kazi kwa uadilifu mkubwa.

Jaji Kiongozi alisema, “Uwe umekula kiapo au hujala kiapo. Kwa kuwa tu mtumishi wa Mahakama lazima kila mmoja wetu awe mwaminifu.  Mtendaji Mkuu wa Mahakama anajua, kabla hata sijateuliwa, hata nyinyi wa Dodoma mnajua. Hatutafanya mchezo kwenye suala la uadilifu kwa sababu tunaamini tukiwa na watumishi waadilifu tutaifikia dira yetu.”

Mhe. Siyani alimshukuru mtangulizi wake kwa kazi kubwa iliyofanyika. Hata hivyo, alibainisha kuwa kuna kazi nyingine kubwa ya kufanya ili kuhakikisha wanajenga Mahakama ambayo sio tu inatimiza dira yake, lakini inayoaminika kwa Watanzania.

Akizungumza kuhusu usikilizaji wa mashauri, Jaji Siyani alimtaka kila mtumishi kwa nafasi yake kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza ndoto ambayo Mahakama imejiwekea. Alibainisha kuwa kuna takribani mashauri 8,000 ambayo yamepevuka, kwa maana yamepita ukomo wa muda ambao Mahakama imejiwekea kuyamaliza.

“Msajili Mkuu yupo, Msajili wa Mahakama Kuu yupo, hili ni eneo ambalo tunapaswa kulifanyia kazi. Lazima tuwe na muda ambao tutajiwekea wenyewe na hatutarajii baada ya hapo kuwa na mashauri ya mrundikano, na hili linawezekana kwa sababu tulipotoka tulikuwa na mashauri mengi zaidi ya haya. Takwimu zinaonyesha kwamba tunakoelekea kuna mafanikio, hivyo hatuwezi kurudi nyuma,” alisema.

Kwa upande wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dodoma aliyokuwa akifanya kazi kama Jaji Mfawidhi kabla ya uteuzi wake, Jaji Kiongozi alielezea furaha yake kwa kuiacha Kanda hiyo ikiwa na takwimu nzuri za usikilizaji wa mashauri.

Kwa mujibu wa Jaji Siyani, alipofika kuhudumu katika Kanda hiyo kulikuwa na wastani wa mashauri 1,200, lakini mpaka anakabidhi ofisi kwa Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. George Masaju, kulikuwepo na mashauri 835. “Idadi ya mashauri yanayokwisha ni kubwa kuliko yale yanayosajiliwa. Jaji Masaju kazi unayo kuhakikisha kwamba mwenendo huo haubadiliki, isipokuwa tunaongeza kasi,” alisema.

Jaji Siyani aliahidi kuendeleza kasi iliyoachwa na mtangulizi wake, Dkt Feleshi na kwamba kazi kubwa aliyoifanya haitapotea. Hivyo, aliwashukuru Watumishi wa  Mahakama Kuu, Kanda ya Dodoma, kwa ushirikiano mkubwa waliompa, ambao pengine ndiyo uliosababisha aonekane kuwa anafaa kushika nafasi hiyo mpya.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, alimpongeza Jaji Kiongozi mpya kwa kuteuliwa kushika nafasi hiyo na kuahidi kumpa ushirikiano wa kutosha ili kuimarisha maslahi ya watumishi na kuweka ukaribu wa kazi za kimahakama na zile zisizo za kimahakama kwa lengo moja la kuharakisha utoaji wa haki kwa wananchi.

Alimuomba pia kuendelea kutengeneza mfumo imara wa kuimarisha maadili kwa watumishi wote wa Mahakama ya Tanzania. “Naomba nikiri wazi kwamba sina uvumulivu na uzembe. Ningetamani yale maagizo ya Mhe. Rais aliyotupatia kusimamia maadili katika kazi tunayatekeleza,” alisema.

Kwa upande wake, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, naye aliahidi kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Jaji Kiongozi kwa kuwa yeye kama msimamizi mkuu wa uendeshaji wa mashauri atakuwa naye bega kwa bega ili kuhakikisha Mahakama zote zinatekeleza jukumu lake la msingi la utoaji haki kwa manufaa ya umma.

Katika hatua nyingine, Mhe.  Jaji Siyani amewaasa watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (Integrated Justice Centre – Dodoma) kutekeleza majukumu yao kwa weledi, bidii na ubunifu.

Akizungumza katika hafla ndogo ya kuagana na watumishi wa Kituo hicho iliyofanyika hivi karibuni Mahakamani hapo, Jaji Siyani pia aliwataka kuzingatia maadili wakati wa kuwahudumia wananchi na hivyo kutekeleza kwa vitendo azima ya utoaji wa haki kwa wakati.

"Nitaendelea kufuatilia kwa ukaribu utendaji kazi wa Mahakama zote za Kanda ya Dodoma. Hivyo, ninawataka muwe makini muda wote katika kazi, mtoe huduma bora kwa wateja huku mkizingatia Maadili ya Utumishi wa Umma,” alisema.

Baada ya nasaha hizo Kiongozi  huyo aliwashukuru watumishi wote wa Mahakama za Kanda ya Dodoma kwa ushirikiano na utendaji kazi uliochagiza kupungua kwa mrundikano wa mashauri Mahakamani na kuwataka kuendelea na bidii hiyo katika kazi zao.

Watumishi wa Mahakama Kuu katika Kanda hiyo waliandaa hafla fupi kwa ajili ya kuagana naye kufuatia kuteuliwa kwake Oktoba 08, 2021 na Mhe.Rais Samia Suluhu Hassan kuwa Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Katika hatua nyingine, Jaji Siyani amewasili katika ofisi yake leo iliyopo Mahakama Kuu jijini Dar es Salaam na kupokelewa na watumishi waandamizi wa Mahakama hiyo, akiwemo Jaji aliyekuwa anakaimu nafasi hiyo, Mhe, John Mgeta. Viongozi wengine waliokuwepo ni Jaji Mfawidhi wa  Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe, Amir Mruma, Jaji Ilvin Mugeta, Jaji Zahra Maruma, Jaji Leila Mgonya na Jaji Said Kalunde, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Msajili wa Mahakama Kuu na Naibu Msajili Mwandamizi, Kanda ya Dar es Salaam.

Akizungumza katika hafla hiyo fupi, Mhe. Jaji Siyani aliwashukuru wote kwa mapokezi ambayo hakuyategemea na kubainisha kuwa kile alichokiona kinaashiria dhana nzuri ya ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu yaliyo mbele yao. Alisema kuwa kama wakifanikiwa kutekeleza dira waliyojiwekea watakuwa wamefanikiwa wote, Hivyo amewaomba Majaji, Wasajili na watumishi wa kada zote kushirikiana na kuendelea kuchapa kazi kwa bidii.

Aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma Mhe. Mustapher Siyani (Kwa sasa Jaji Kiongozi) akiwasili viwanja vya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki – Dodoma mara baada ya shughuli za kuapishwa kwake kukamilika Oktoba 11, 2021.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akizungumza na watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma (baadhi hawapo pichani) katika hafla fupi ya kuagana na watumishi hao.

Sehemu ya watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki wakimsikiliza Mhe. Jaji Siyani wakati wa hafla hiyo.
DAR ES SALAAM: Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akizungumza na baadhi ya Wahe. Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania pamoja baadhi ya Watumishi wa Mahakama Kuu alipowasili leo Ofisini kwake Mahakama Kuu-Dar es Salaam.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani, akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na Wahe. Majaji, Wasajili na Watendaji wa Mahakama Kuu mara baada ya kuwasili ofisini kwake leo Oktoba 15, 2021.

(Picha na Mary Gwera, Mahakama)



 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni