Na Faustine Kapama na Lydia Churi, Mahakama
Mahakama
ya Tanzania imepongezwa na Benki ya Dunia kwa uwekezaji mkubwa iliyofanya
katika kutoa huduma mbalimbali za kimahakama kwa kupitia Teknolojia ya Habari
na Mawasiliano (TEHAMA).
Hayo
yamebainshwa leo tarehe 25 Novemba, 2021 na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof.
Ibrahim Hamis Juma kwenye hafla ya kuwaapisha Naibu Wasajili 27 wapya, uapisho
ambao uliyofanywa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher
Siyani.
“Sisi
tumefanya uwekezaji mkubwa sana katika teknolojia. Mkurugenzi wa Benki ya Dunia
alipotutembelea juzi alishangazwa na hatua kubwa ambayo tumepiga. Yeye anatoka
nchi ya Indonesia lakini anasema atatuma watu waje wajifunze kutoka kwetu,”
Mhe. Prof. Juma aliwaeleza viongozi mbalimbali waliohudhuria uapisho huo.
Hata hivyo,
alielezea wasiwasi wake kama mtu huyo akija siku hiyo akakutana na kiongozi ambaye
mapinduzi hayo ya teknolojia yamempita. “Ni kiongozi, ni Naibu Msajili, lakini
haelewi Mahakama tunakwenda wapi, yule atatoka na hisia kwamba sisi sio
wakweli. Kwa hiyo uwekezaji mkubwa
tulioufanya katika maeneo ya TEHAMA lazima tuuedeleze,” alisisitiza.
Hivyo, Jaji
Mkuu aliwataka Naibu Wasajili hao kuwa injini na moyo kwenye maendeleo ya TEHMA
kwa kuwa wote wanafahamu dunia inakokwenda na kwa kuzingatia kasi ya madadiliko na kwa
kiasi gani teknolojia inavyoweza kuwabadilisha.
Mhe.
Prof. Juma pia alielezea kufurahishwa na maendeleo makubwa ambayo yamefikiwa na
Mahakama ya Tanzania katika usajili wa mashauri kwa njia ya mtandao (e-filing),
hatua ambayo ni chanya na imepokelewa vizuri na wananchi kwa ujumla. “Hivi sasa
e-filing ni kama asilimia 100. Hata wananchi wanakubali kwamba mashauri yasajiliwe
kwa njia ya mtandao, Sasa kuna nafasi ya kuendeleza kwa vile wananchi wanataka
zaidi,” alisema.
Aliyataja
maeneo mengine ambayo yamekonga nyoyo za viongozi wa Benki ya Dunia ni
usikilizaji wa mashauri kwa Mkutano Mtandao (Video Conference) hatua ambayo imesaidia
sana hasa wakati wa janga la ugonjwa wa Uvico-19 na pia uwekezaji ambao
umefanywa kwenye mfumo wa kupandisha hukumu za Mahakama (Tanzill).
“Wote
mnafahamu Uamuzi hasa wa Mahakama ya Rufani kila siku unapotoka hupandishwa
kwenye mtandao. Kwa upande wa Mahakama Kuu, tumefanya utafiti kuna Majaji wengine
wamemaliza kutoa hukumu zao, lakini hazipandishwi, Hapa huwezi kumlaumu Jaji, yeye
akishamaliza inabaki kazi ya Msajili. Kama hakuna upandishwaji, Msajili
Mkuu atawafuata ninyi,”aliwaambia Naibu Wasajili hao.
Jaji Mkuu
pia alitumia nafasi hiyo kuwapa ushauri kwa upole kabisa viongozi hao juu ya mambo mbalimbali ambayo wanatakiwa
kuzingatia wanapotekeza majukumu yao mapya katika muktadha mzima wa utoaji haki
kwa wananchi.
Aliwaona Naibu
Wasajili hao kama madaraja unganishi, ambalo linaunganisha watumishi wa
Mahakama na viongozi, wadau wa shughuli za kimahakama na pia huunganisha
viongozi wa Mahakama na maelekezo na sheria mbalimbali zinazotungwa na
kuhakikisha zinafika kwa wahusika.
“Shughuli
zenu ni muhimu sana katika uboreshaji wa shughuli za Mahakama. Nyinyi kama viongozi
katika masjala ndiyo taswila ya Mahakama, kwa sababu mtu anapofika kwa mara ya
kwanza, kituo cha kwanza mara nyingi ni masjala. Ingawa katika Vituo Jumuishi
tutakuwa na wale watakaopokea na kuelekeza wapi pa kwenda, lakini hadi kufikia
sasa ni masjala ndiyo kituo cha kwanza,”alisema.
Jaji Mkuu
alisema kuwa kwa sababu wao ndio wasimamizi wa hizo masjala chochote
kinachotokea pale huwa kinaashiria uongozi wao. Alitoa mfano wa lugha ambayo
inaweza kutumika katika kumhudumia mwananchi kama ikiwa ni ya kistaarabu ni Msajili
ndiye atakuwa anajenga ustarabu katika hiyo masjala. Hivyo, alibainisha kiuwa
yote yanayofanyika katika masjala yanamchango mkubwa katika upatikanaji wa haki
na yanaumuhimu katika kujenga imani ya wananchi.
“Wakati mwingine
mwananchi anajenga imani siku ya kwanza anayofika mahakamani. Akipokelewa
vizuri anakuwa na imani kuwa anaenda kupata haki. Lakini akifika siku ya kwanza
anakutana na sura au dalili za rushwa, anapokutana na lugha kali ya
kutisha hiyo ndiyo picha atakayoondoka
nayo mahakamani,” alisema.
Jambo lengine
ambalo Mhe. Prof. Juma alisisitiza ni uwepo wa mahusiano mazuri kati ya Naibu
Msajili na watumishi wengine waliopo chini yake ambapo kuna maelekezo ambayo
hutolewa na vingozi wa ngazi za juu lakini huishia kwa wasajili pekee bila
wengine kujua.
“Utakuta kuna
barua, maelekezo na nyaraka mbalimbali ambazo zinatoka kwa viongozi kama Majaji
Wafawidhi, Jaji Kiongozi na zingine zinatoka kwa Msajili Mkuu na tunadhani ni
barua zetu wenyewe. Hakikisha waliochini yako wanelewa hayo maelekezo mara barua
na nyaraka zinapofika kwako,” aliwaambia Naibu Wasajili hao.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akifafanua jambo alipokuwa anaongea na Naibu Wasajili 27 wapya mara baada ya kuapishwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani leo tarehe 25 Novemba, 2021 jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya Naibu Wasajili 27 wapya wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma mara baada ya kuapishwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani leo tarehe 25 Novemba, 2021.
Sehemu ya Naibu Wasajili 27 wapya wakichukua kumbukumbu muhimu wakati Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alipokuwa anaongea nao.
Sehemu nyingine ya Naibu Wasajili 27 wapya wakimsikilza Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.
Naibu Wasajili wengine (juu na chini) wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na kuchukua kumbukumbu muhimu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni