Na Faustine Kapama, Mahakama-Lushoto
Jaji
Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani amewataka Naibu
Wasajili na Watendaji wa Mahakama nchini kushirikiana kwa karibu na kuacha
kugombea fito na madaraka wakati wa kutekeleza majukumu ya utoaji haki kwa
wananchi.
Mhe. Siyani
ametoa wito huo leo tarehe 29 Novemba, 2021 wakati anafungua mafunzo elekezi ya
siku tano kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama yanayofanyika katika Chuo
cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).
“Usimamizi
wa utekelezaji wa majukumu yote yanayosaidia katika utoaji wa haki umo mabegani
mwenu. Mkiwa wamoja, imara na madhubuti katika kazi zenu, tutaifikia dira yetu
kwa haraka zaidi, vinginevyo safari yetu itakuwa ndefu. Nitumie fursa hii
kusisitiza ushirikiano, upendo, kuheshimiana na kusaidiana baina yenu ili kazi
iendelee. Msiende kugombea madaraka,” alisema.
Kwa mujibu
wa Jaji Kiongozi, makoti ya uongozi waliyovikwa na Watanzania wanapaswa
kuyatumia vizuri ili kuwaletea maendeleo, hivyo umoja miongoni mwa viongozi ni
muhimu katika mafanikio ya aina yoyote. Alibainisha kuwa kwa kuwa viongozi hao
wanajenga nyumba moja, hakuna sababu ya kugombea fito, hivyo ni budi kuwa kitu
kimoja.
Mhe.
Siyani aliwakumbusha viongozi hao jambo jingine muhimu linalohusu uhuru wa
Mahakama, huku akibainisha kuwa uhuru unaokusudiwa sio ule wa kuifanya Mahakama
ya Tanzania kuwa kisiwa. “Sisi tumekasimiwa jukumu la kusimamia haki nchini na
uhuru wetu ni kwenye kuamua juu ya haki za watu. Uhuru huo unapaswa kulindwa
kwa kusudi la kujenga na sio kubomoa. Ni vema kila mmoja wetu akaheshimu na
akaulinda uhuru huo lakini pia kuheshimu mipaka ya mihimili mingine,” alisema.
Jaji Kiongozi
alibainisha pia kuwa Mahakama inatekeleza Mpango Mkakati wake wa Miaka Mitano
wenye nguzo kuu tatu ambazo ni Utawala, Uwajibikaji na Matumizi ya Bora ya
Rasilimali; Upatikanaji wa haki sawa kwa wote na kwa wakati; na Kujenga taswira
chanya na Kurejesha imani ya wananchi kwa Mahakama. Hivyo, aliwasihi katika
utendaji wao kuzingatia nguzo hizo zote kwa uaminifu, bidii na uadilifu, kila
mmoja kwa nafasi yake na kuonya kuwa matokeo ya kazi za kila mmoja wao yatapimwa
kwa kutumia nguzo hizo tatu.
Mhe.
Siyani alisema kuwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mahakama ina wajibu wa kutoa haki kwa wote na kwa wakati kama inavyoelezwa
katika Ibara ya 107A na ili kuweza kutekeleza majukumu ya utoaji
haki vema viongozi wote hawana budi kuwa na uelewa wa kutosha juu ya masuala ya
sheria na haki kwa ujumla. Alikumbushia kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Ibrahim
Hamis Juma mara kwa mara amekuwa akisisitiza kuwa watumishi wote wa Mahakama
wanatakiwa kuwa na ujuzi na uelewa wa kutosha wa majukumu yao na nafasi zao.
“Hivyo,
ni kwa muktadha huo mafunzo haya yameandaliwa ili kuweza kutimiza hitaji la
kikatiba Pamoja. Binafsi nimepata nafasi ya kupitia ratiba yenu ya mafunzo kwa siku
tano zijazo. Nimefurahi kuona kuwa mada zilizopo katika ratiba hiyo zinalenga
kutukumbusha yatupasayo kufanya ili kutimiza nguzo hizo tatu za Mpango Mkakati,”
Jaji Kiongozi alisema.
Akitoa neno
la shukrani, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma alishukuru
uongozi wa Mahakama na Chuo kwa ujumla kwa kuwezesha mafunzo hayo, huku akiahidi
kwa niaba ya Naibu Wasajili na Watendaji kutekeleza maelekezo yote aliyoyatoa
Jaji Kiongozi katika kuwatumikia Watanzania wakati wakitekeleza majukumu yao ya
utoaji haki kwa umma.
“Tutafanya
yote tutakayoweza kwa kadri tutakavyojaliwa kuweza kutimiza malengo ya
kitaasisi. Migongano( baina ya viongozi) inaweza kuwepo, kama ambavyo hata
kwenye vitabu vya dini wanasema majaribu hayanabudi kuja, ila ole wake
ayaletaye,” alionya Mhe. Chuma.
Akitoa
neno la salamu kabla ya Jaji Kiongozi kufungua mafunzo hayo, Mtendaji Mkuu wa Mahakama
ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel alibainisha kuwa Mahakama ya Tanzania
ni Mhimili mkubwa, hivyo kuwa na watu sahihi, wenye taaluma sahihi na wabobezi
sahihi ni jambo la msingi sana, hivyo hawatapoteza chochote katika kuwekeza
katika uelewa wa watu. Alimhakikishia Jaji kiongozi kuwa sio kwa Naibu Wasajili
tu na Wakurugenzi Wasaidizi waliojiunga hivi karibuni, bali pia Mahakama itaendelea
kutoa mafunzo kwa kada zote.
“Nimeshaongea
na Mkuu wa chuo watengeneze program fupi ya mafunzo kwa ajili ya makatibu
muhtasi, watunza kumbukumbu na pia madereva wetu ambao wakati sisi tumelala
kwenye magari wao wanatuendesha masaa yote, angalau nao waje Lushoto ili waweze
kufurahia kazi zao wanazofanya. Nina amini hilo litafanyika,” alisema.
Katika mafunzo
hayo, mada mbalimbali zitawasilishwa na waezeshaji waliobobea katika maeneo
mbalimbali, akiwemo Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel,
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, Jaji Mkuu Mstaafu
,Mohamed Chande Othman, Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. January
Msoffe, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Katarina Revocati na watendaji
wengine waandamizi wa Mahakama.
Miongoni
mwa mada zitakazowasilishwa kwenye mafunzo hayo zinajumuisha Uongozi wa
Kimkakati, Stadi za Uongozi na Uwezo wa Kukabili Mabadiliko, Wajibu wa
Mahakama, Utamaduni wake na Uhusiano wake na Mihimili Mingine ya Dola, Sheria
ya Uendeshaji wa Mahakama na Uboreshaji unaofanywa na Mahakama, Maadili ya
Watumishi wa Umma na Maadili ya Kimahakama, Usimamizi wa fedha na Manunuzi ya
Umma pamoja na Usimamizi wa Nyaraka.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akizungumza wakati wa ufunguzi mafunzo elekezi ya siku tano kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA). Ufunguzi wa mafunzo hayo umefanyika leo tarehe 29 Novemba, 2021.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel akisisitiza jambo wakati akitoa salamu zake kabla ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani kufungua mafunzo elekezi ya siku tano kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).
Msajili Mkuu wa Mahakama, Mhe Wilbert Chuma akitoa neno la shukrani mara baada ya Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani kufungua mafunzo elekezi ya siku tano kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).
Wajumbe wa meza kuu wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe wa Sekretarieti ya IJA na Makatibu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni